Elimu /Maisha : Wasichana Wanne wa Tanzania Wapelekwa kupata Mafunzo ya Uongozi na Utamaduni wa Afrika Mashariki na Kati - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


18 Jan 2017

Elimu /Maisha : Wasichana Wanne wa Tanzania Wapelekwa kupata Mafunzo ya Uongozi na Utamaduni wa Afrika Mashariki na Kati



Wasichana wanne wa Tanzania wakiaga kwa kupungia mikono huku wakiwa na Bendera ya Taifa waliyokabidhiwa na Kamishna Mkuu wa Chama cha Tanzania Girl Guides (TGGA), Symphorosa Hangi katika hafla ya kuwaaga kwenda Uganda ambako watakutana na wenzao 31 kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati katika mafunzo ya uongozi na utamaduni katika nchi hizo. Hafla hiyo ilifanyika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, Dar es Salaam juzi. Kutoka kulia ni Farida Mjoge,Elizabeth Betha, Edna Chembele na Ummy Mwabondo. (PICHA, HABARI NA RICHARD MWAIKENDA;KAMANDA WA MATUKIO BLOG)

Kamishna Mkuu wa Chama cha Tanzania Girl Guides (TGGA), Symphorosa Hangi (kushoto) akiwakabidhi wasichana wanne, Bendera ya Taifa katika hafla ya kuwaaga kwenda Uganda ambako watakutana na wenzao 31 kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati katika mafunzo ya uongozi na utamaduni katika nchi hizo. Hafla hiyo ilifanyika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, Dar es Salaam juzi. Kutoka kulia niElizabeth Betha, Edna Chembele, Farida Mjoge na Ummy Mwabondo.


Na Richard Mwaikenda

WASICHANA wanne wameondoka kwenda Uganda kwenye programu maalumu ya kubadilishana uzoefu wa mafunzo ya uongozi na utamaduni.


Wakifika Uganda wataungana na wenzao 31 kutoka nchi nane za Afrika Mashariki na Kati, ambapo watapigwa msasa wa mafunzo hadi Januari 25, mwaka huu watakapotawanywa kwenda nchi mbalimbali.


Wasichana hao wanachama wa Chama cha Tanzania Girl Guids (TGGA),waliondoka Uwanja wa Ndege wa Kimaitafa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, juzi kwa Ndege ya Kenya Airways, baada ya kukabidhiwa Bendera ya Taifa na Kamishna Mkuu wa Tgga, Symphorosa Hangi.


Wasichana hao 35 watagawanywa katika nchi hizo nane ambapo nchini wataletwa watatu kutoka katika baadhi ya nchi hizo, kuja kujifunza masuala ya uongozi na utamaduni.


Akizungumza wakati wa kuwaaga wasichana hao, Kamishna Mkuu wa Tgga, Hangi alisema lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wasichana ili wawe viongozi bora wa baadaye katika nchi zao ikiwemo pia kujiamini na kujithamini.


Alitaja nchi zitakashiriki kwenye programu hiyo ambayo kwa hapa nchini ilianza mwaka jana, kuwa ni; Tanzania, Kenya, Uganda, Zambia, Rwanda, Burundi, Zimbabwe na Afrika Kusini.


Alisema kuwa watakapokuwa kwenye nchi hizo husika, kila mmoja ataishi maisha ya kujitegemea kwa kwenda vijijini kuishi na wananchi na kuzungumza nao kuhusu mambo mbalimbali ya maisha ikiwemo uongozi, utamaduni, kujiamini na kujithamini. Gharama za kwenda katika nchi hizo hufahiliwa na Taasisi ya FK Norway ambayo huwapatia nauli, fedha za malazi, posho na masuala ya afya.


Alisema kuwa watakaporejea nchini Julai mwaka huu, watapaswa kutoa mrejesho wa waliojifunza huko, ili usaidie kuwaelimisha wasichana wengine nchini.

Kamishna akiwakabidhi nyaraka mbalimbali za kazi

Ni furaha iliyoje

Wakipiga picha na baadhi ya wafanyakazi wa TGGA



Wakipiga picha na dereva wa TGGA,Juma Rashid

Kamishna akiagana na mmoja wa wasichana hao

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad