WAHITIMU WA CHUO CHA BIASHARA (CBE) WATAKIWA KUJIAJIRI WENYEWE - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


24 Nov 2012

WAHITIMU WA CHUO CHA BIASHARA (CBE) WATAKIWA KUJIAJIRI WENYEWE


Katibu mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Bi. Joyce Mapunjo akizungumza na wahitimu 2882 wa Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es salaam (CBE) wakati wa mahafali ya 47 ya Chuo hicho yaliyofanyika katika viwanja vya Mnazi mmoja jana jioni Jijini Dar es salaam na kuwataka kutumia elimu yao  kujiajiri na kuwa chachu ya maendeleo nchini.
Kaimu Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es salaam (CBE) Bw. Athman Ahmed  (kulia) akitoa taarifa kuhusu mahafali ya 47 na maendeleo ya chuo hicho kwa mgeni rasmi wa mahafali hayo Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Bi. Joyce Mapunjo (katikati).
Baadhi ya wahitimu wa  shahada ya Masoko katika Chuo cha Biashara Dar es salaam wakiweka kofia zao sawa mara baada ya kumalizika kwa tamko la kuwatuku shahada hiyo.
Wahitimu wa mahafali ya 47 ya Chuo cha CBE wakifuatilia masuala mbalimbali yaliyokua yakiendelea wakati wa mahafali hayo katika viwanja vya Mnazi mmoja jijini Dar es salaam.
Baadhi ya wananchi na wapiga picha wa kujitegemea waliohudhuria mahafali ya 47 ya Chuo cha CBE sehemu ya Dar es salaam wakiendelea kufuatilia matukio mbalimbali wakati wa sherehe hizo.(Picha na Aron Msigwa – MAELEZO).
Na. Aron Msigwa –MAELEZO.
 Wahitimu wa  Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es salaam wametakiwa kutumia fursa na elimu waliyoipata wakati wa masomo yao kujiajiri wenyewe badala ya kusubiri kuajiriwa ili kupunguza ongezeko kubwa la vijana wasio na ajira mitaani.
Akizungumza na wahitimu 2882 wa fani mbalimbali wa chuo hicho wakati wa mahafali ya 47 yaliyofanyika jana jioni jijini Dar es salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Bi. Joyce Mapunjo amewataka vijana hao kutumia elimu yao kujiajiri wenyewe na kutengeza  ajira kwa vijana wengine wanaohangaika kutafuta kazi kila kukicha. 
Amewataka wahitimu hao kuwa mfano wa kuigwa katika jamii na kutumia elimu yao kutatua matatizo mbalimbali yanayoikabili jamii na kuwaasa kujiepusha na vitendo vya uhalifu, anasa na kujikinga na maambukizi ya  VVU.
Kuhusu kukisaidia chuo hicho Bi. Joyce amesema kuwa serikali itaendelea kukisaidia chuo hicho kifedha ili kiweze kutimiza malengo mbalimbali kiliyojiwekea na kutoa wito kwa viongozi wa chuo hicho kuongeza ubunifu katika kutafuta vyanzo mbalimbali vya mapato ya chuo hicho.
Aidha amesema  kuwa ongezeko la wahitimu  wa kike kwa asilimia 49  katika fani mbalimbali katika chuo hicho ni jambo la kujivunia na kuwapongeza wakufunzi wa chuo hicho kwa kazi nzuri  wanayoifanya ya utoaji wa elimu bora.
Naye kaimu mkuu wa Chuo hicho Bw. Athman Ahmad amewapongeza wahitimu hao waliotunukiwa vyeti katika fani 30 na kuwataka kutumia ipasvyo elimu waliyoipata kwa manufaa ya taifa kwa kufanya kazi kwa bidii na kuepuka tama ya kutaka kupata utajiri kwa muda mfupi pindi wanapofanikiwa kujiajiri au kuajiriwa.
“Nawaomba muwe wavumilivu na mjiepushe na vitendo vya kihalifu na kutaka kupata utajiri kwa kipindi kifupi, najua ninyi ni vijana na mnatamani vitu vingi kwa wakati mmoja cha msingi mfanye kazi kwa bidii, uaminifu na kuepuka tamaa zinazoweza kuwafanya muingie katika vitendo viovu” amesema.
Bw. Ahmad amesema licha ya chuo hicho kukabiliwa na changamoto ya udogo wa eneo na uchakavu wa miundombinu pia kina kabiriwa na uhaba wa walimu 20 kuongezea idadi ya 80 waliopo sasa na tayari juhudi mbalimbali zinaendelea kufanyika ili kuboresha huduma za elimu chuoni hapo na kuondoa tatizo la uhaba wa madarasa na walimu.
Amesema chuo hicho kina muda mrefu tangu mwaka 1965 na tayari majengo yake hayana uwezo wa kuchukua wanafunzi wengi kutokana na idadi kubwa ya wanafunzi na mwamko mkubwa wa watanzania katika masuala ya elimu jambo linalowafanya kulazimika kukodi madarasa nje ya chuo.
“Chuo kilipoanzishwa mwaka 1965 kilikua na wanafunzi 30 na leo hii kwa eneo la Dar es salaam tuna wanafunzi takribani 9000  hili ni jambo linalohitaji uboreshaji wa miundombinu na uongezaji wa majengo mapya ili kukabiliana na changamoto hiyo” amesema Bw. Ahamad .
Kaimu mkuu wa chuo hicho amefafanua kuwa hivi sasa chuo kina mkakati wa kuongeza mafunzo ya  shahada ya uzamili na kuongeza majengo ya madarasa katika kampasi zote 3 za Dar es salaam, Dodoma na Mwanza.
“Jambo hili tuko makini nalo na sasa  kazi ya uchoraji wa michoro na juhudi za kutafuta fedha wakiwemo wafadhiri zinaendelea kufanyika ili kuweza kukamilisha mipango hiyo.
Mahafali hayo ya 47 yaliyofanyika jana jioni katika viwanja vya Mnazi mmoja jijini Dar es salaam yalihudhuriwa na wananchi kutoka maeneo mbalimbali na viongozi wa Bodi ya Chuo hicho wakiongozwa na Prof. Mathew  Luhanga kutoka Chuo kikuu cha Uhandisi na Teknolojia cha Chuo kikuu cha Dar es salaa  na yatafuatiwa na mahafali mengine katika kampasi ya Dodoma tarehe 1 na tarehe 8 mwezi Desemba katika kampasi ya Chuo cha Elimu ya Biashara Mwanza .

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad