Michezo : Filbert Bayi ndani ya Jumba la Wanariadha Nguli (Legends) Duniani Nchini Ufaransa - Wazalendo 25 Blog

Glory to Story.

Habari Mpya

PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0784 643 633


PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0676 643 633

12 Aug 2024

Michezo : Filbert Bayi ndani ya Jumba la Wanariadha Nguli (Legends) Duniani Nchini Ufaransa

Shirikisho la Riadha la Dunia (World Athletics - WA) mnamo Jumanne usiku Agosti 6, 2024 liliandaa hafla ya tatu ya Museum of the World Athletics (MOWA) ambapo mwanariadha nyota waTanzania Filbert Bayi alijumuishwa rasmi kwenye jumba la makumbusho ya wanariadha nguli (legends) duniani ya shirikisho hilo.

- Kwa Kiingereza; ‘Filbert Bayi has been indicted in the Hall of Fame of World Athletics in the MOWA.

Hafla hiyo, iliyoandaliwa na Rais wa Shirikisho hilo Lord Sebastian Coe, imefanyika ukumbi wa Monnaie de Paris Museum, jijii Paris kama sehemu ya Michezo ya Olympic ya Paris 2024 kwa heshima ya Bayi kwa kushikilia rekodi mbili za riadha za dunia, ambazo zimeorodheshwa katika Makumbusho ya MOWA yaliyoko mjini Monaco nchini Ufaransa.

Lord Sebastian Coe, ambaye ni bingwa wa dunia wa mbio za kati wa zamani, tayari alishatangaza kujumuishwa kwa Bayi katika MOWA kabla ya uzinduzi wa makumbusho hayo Machi 11, 2021 mjini Monaco, ambapo Bayi alikuwa ni mmoja wa nyota wa riadha dunia walioalikwa kuhudhuria hafla ya uzinduzi huo.

Filbert Bayi, ambaye kwa sasa ni Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki ya Tanzania (TOC), amepewa heshima hiyo kwa kuwa mmoja wa wanariadha nyota  waliovunja rekodi mbili za dunia wakati huo jambo ambalo halikuwa rahisi kutokana na ushindani mkali uliokuwapo pamoja na wanariadha hodari.

Mafanikio makubwa zaidi ya Bayi yanatajwa kuwa kwenye  fainali ya mita 1500 katika Michezo ya Jumuiya ya Madola ya 1974 huko Christchurch, New Zealand, aliposhinda medali ya dhahabu mbele ya mwanariadha wa New Zealand John Walker na Mkenya Ben Jipcho.

Katika ushindi huo, Bayi aliweka rekodi mpya ya dunia ya dakika 3 32.16 s, iliyoidhinishwa na IAAF kama 3:32.2, na Walker akaenda chini ya rekodi ya zamani ya dunia iliyowekwa na Mmarekani Jim Ryun.

Mchuano huo wa Bayi na John walker hadi leo unatajwa kama moja ya mbio kubwa zaidi za 1500 m wakati wote.

Baada ya Bayi kuweka rekodi hiyo ya dunia ya mita 1500 mwaka 1974, mwaka mmoja baadaye (1975)  katika Mashindano ya ‘Dream Mile’ huko Kingston Jamaica akavunja rekodi ya maili moja iliyokuwa inashikliliwa na huyo huyo Jim Ryun.

Bayi pia alivunja rekodi ingine ya kuwa mmiliki kwa muda wa miaka 48 wa rekodi ya ubingwa wa 1500m ya Michezo ya Jumuiya ya Madola ambayo hatimaye ilikuja kuvunjwa mwaka 2022 kwenye michezo hiyo huko Birmingham, Uingereza.

Kwenye michezo hiyo ya Birmingham Bayi ndiye aliyepewa heshima ya kumvalisha medali ya dhahabu Ollie Hoare wa Australia aliyeshinda na kuvunja rekodi yake ya dakika 3:32.2 wa kutumia dakika 3:30.12

Mafanikio mengine ya Bayi yalikuwa Katika michezo ya Olympic ya Moiscow Urusi mwaka 1980 ambapo alishinda fedha katika mita 3,000 kuruka vikwazo (Steeple Chase).

Filbert Bayi katika akiwa na picha yake itakayowekwa kwenye makumbusho hayo wakati wa hafla  maalumu ya Shirikisho la Riadha la Dunia (World Athletics - WA) lililofanyika Jumanne usiku Agosti 6, 2024  ya kumjumuiisha rasmi mwanariadha huyo nyota waTanzania Filbert Bayi kwenye makumbusho ya wanariadha nguli (legends) duniani (MOWA)  ya shirikisho hilo yaliyoko mjini Monaco, Ufaransa 

Filbert Bayi akiwa na Kutoka Kushoto: Marc Schwartz, Mwenyekiti & Mkurugenzi Mtendaji wa Monnaie de Paris Museum, Lord Sebastian Coe na  Billy Mills (USA) mshindi wa 1964 Tokyo Olimpiki mbio za mita 10000. 

Filbert Bayi akiwa na Rais wa Shirikisho la Riadha Duniani  (World Athletics - WA) Lord Sebastian Coe wakati wa  hafla  maalumu ya Shirikisho hilo lililofanyika Jumanne usiku Agosti 6, 2024  ya kumjumuiisha rasmi mwanariadha huyo nyota waTanzania Filbert Bayi kwenye makumbusho ya wanariadha nguli (legends) duniani (MOWA)  ya shirikisho hilo yaliyoko mjini Monaco, Ufaransa 

1 comment:


PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0784 643 633