Teknolojia : Waajiri Waaswa kutumia mfumo wa Kidigitali kuwasilisha Madai ya Fidia WCF - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


28 Sept 2023

Teknolojia : Waajiri Waaswa kutumia mfumo wa Kidigitali kuwasilisha Madai ya Fidia WCF

 

NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID

WAAJIRI kote nchini wamehimizwa kutumia TEHAMA kuwasilisha taarifa kuhusu mfanyakazi aliyepata Ajali, Ugonjwa au Kifo kilichotokana na kazi aliyoajiriwa kwa mujibu wa mkataba wa ajira yake,  ili kurahisisha mchakato wa malipo ya fidia.

Wito huo umetolewa  hivi karibuni na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidida kwa Wafanyakazi, (WCF), Dkt. John Mduma,  wakati akifungua semina kwa maafisa rasilimali na maafisa usalama na afya mahali pa kazi wa mkoa wa Dar es Salaam.

Alisema, kwa majukumu waliyonayo maafisa hao kutoka kwenye kampuni wanazoziwakilisha, wao ni kiungo muhimu kati ya mwajiri na WCF, na kwamba Mfuko, umehakikisha unarahisisha utoaji wa huduma ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia na kwa sasa huduma zote zinapatikana mtandaoni kupitia (portal.wcf.go.tz).

“Uzoefu wetu unaonyesha uptake ipo ya kutosha ya huduma zetu na hasa huduma zinapatikana mtandaoni, ni rai yangu kuendelea kuwahimiza kutumia mitandao inayotoa huduma za WCF,  na sit u kurahisisha utoaji huduma, lakini pia kupunguza gharama na muda na hivyo kuharakisha utoaji wa malipo ya Mafao ya fidia.” Alisisitiza.

Alisema Mfuko upo kwa nia ya kuwaondolea watu watakaopata madhila yatokanayo na kazi, madhara ya kijamii, kiuchumi na hasa kuchangia katika kuhakikisha kwamba kipato cha wanaopatwa na madhara haya hakiyumbi kama ambavyo sera inavyoelekeza.

Aidha,  Dkt. Mduma alisema, serikali ilianzisha Mfuko huo ili ubeba jukumu la kumuhudumia mfanyakazi aliyeumia au kuugua kutokana na kazi, huku  mwajiri yeye abaki na jukumu la uzalishaji na kusimamia uendelevu wa biashara zake na hivyo kuchangia ukuaji wa uchumi wanchi.

“Tunaamini kwa kuyatenganisha haya tuko kwenye model nzuri ya hifadhi ya jamii kwenye eneo la Fidia kwa Wafanyakazi kuliko ilivyokuwa hapo awali kabla ya kuanzishwa kwa Mfuko.” Alibainisha.

Akizungumzia kuhusu yale yaliyofundishwa kwenye semina hiyo, Mkurugenzi wa Huduma za Tathmini WCF, Dkt. Abdulsalaam Omar, alisema washiriki wamejifunza namna ya kutoa taarifa za ajali au magonjwa yatokanayo na kazi kwa njia ya mtandao ikiwemo kutuma madai, lakini pi walijifunza kuhusu masuala ya usalama na afya mahali pa kazi ikiwemo jinsi ya kubaini vihatarishi maeneo ya kazi.

Kwa upande wao, washiriki wameipongeza WCF kwa utaratibu huo wa kuendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali kuhusu elimu ya fidia kwa wafanyakazi.

Bi. Zainab Jereko, ambaye ni mshiriki, aliwaasa  waajiri kuzingatia usalama na afya mahali pa kazi, ambapo alisema inagawa WCF ipo kwa ajili ya kutoa fidia, lakini hiyo haiondoi wajibu wa waajiri kuzingatia usalama na afya  mahali pa kazi unakuwepo.

Bi. Jereko pia alisifu mfumo wa kufungua madai kupitia mtandao, “umekuwa na msaada mkubwa kwa waajiri kwani umerahisisha utoaji taarifa lakini pia umeondoa usumbufu na upotevu wa muda  wa kwenda ofisi za WCF ili kutoa taarifa.” Alisema Bi. Jereko.

“Pamoja na yote niliyojifuzna nimefurahia sana namna Mfuko ulivyoweka mifumo ya kisasa ya utoaji taarifa kwa njia ya mtandao endapo itatokea ajali eneo la kazi.” Alisema mshiriki mwingine Bw.Goodlove Bugenyi.

Kwa mujibu wa Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi, mwajiri yoyote Tanzania Bara anawajibika kujisajili katika Mfuko.

Mwajiri anaweza kujisajili katika Mfuko kwa njia ya mtandao (portal.wcf.go.tz) au kwakujaza Fomu za usajili (WCR-1 na WCR-2) na kuziwasilisha kwenye ofisi ya Mfuko iliyopo karibu nae au ofisi za idara ya kazi.

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidida kwa Wafanyakazi, (WCF), Dkt. John Mduma
Mkurugenzi wa Huduma za Tathmini WCF, Dkt. Abdulsalaam Omar
Meneja Tathmini Vihatarishi mahali pa Kazi, Bi. Naanjela Msangi, akitoa 'darasa' kuhusu hatua mbalimbali za kuchukua ili kubaini vihartarishi vinavyoweza kupelekea ajali au magonjwa mahali pa kazi.
Baadhi ya washiriki
Baadhi ya washiriki
Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidida kwa Wafanyakazi, (WCF), Dkt. John Mduma (kushoto) akimkabidhi kitendea kazi, Bi. Secillia Assey, huku Meneja Tathmini Vihatarishi mahali pa Kazi, Bi. Naanjela Msangi, akishuhudia.  

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad