Matukio : Mtu mmoja auwawa kwa Tuhuma za wizi wa Kuku, Mwanza - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


28 Jan 2017

Matukio : Mtu mmoja auwawa kwa Tuhuma za wizi wa Kuku, Mwanza



MTU mmoja Mkazi wa Kijiji cha Kanyelele , Safari Bungate (51) ameuawa na kundi la watu waliojichukulia sheria mkononi kwa kumpiga mtu huyo mawe na fimbo sehemu mbalimbali za mwili wake baada ya kuiba kuku katika nyumba ya mmiliki wa kuku, Tetema mathias (40), mkulima na mkazi wa kijiji cha Kanyelele, kitendo ambacho ni kosa kisheria.


Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Naibu, Kamishina, Ahmed Msangi amesema tukio hilo limetokea Januari 26 mwaka huu majira ya saa nne usiku katika kijiji cha Kanyelele tarafa ya Usagara Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza.


Taarifa hiyo inadaiwa kuwa mwenye nyumba, Tetema Mathias akiwa amelala na familia yake, alikuja mtu/marehemu akaingia ndani kupitia dirishani na kuiba kuku mmoja, ndipo wakati alipokuwa anataka kuondoka Mathias alimuona na kuanza kupiga yowe ya mwizi akiomba majirani waje wamsaidie kumkamata huku akimkimbiza barabarani.


Hata hivyo taarifa ilidai kuwa watu/ majirani waliamka na kufanikiwa kumkamata marehemu akiwa na kuku amemshikilia kisha wakaanza kumpiga kwa mawe na fimbo sehemu mbalimbali za mwili wake kitendo kilichosababisha mtu/ marehemu huyo kupoteza fahamu na baada ya muda mchache alifariki dunia.


Taarifa ya Kamanda Msangi amesema raia wema walitoa taarifa polisi ndipo askari walifika eneo la tukio na kukuta mtuhumiwa wa wizi akiwa tayari amefariki dunia na mwili wa marehemu tayari umefanyiwa uchunguzi na daktari na kukabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya mazishi.


Jeshi la Polisi linamshikilia Tetema Mathias kwa mahojiano zaidi kuhusiana na tukio hilo. Naibu, Kamishina Msangi ametoa wito kwa wakazi wa Jiji na Mkoa wa Mwanza, akiwataka kuacha tabia ya kujichulia sheria mkononi kwani ni kosa la jinai, aidha anawataka wananchi pindi wanapomkamata mhalifu wamfikishe katika vyombo vya sheria ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yake.


Pia Naibu Kamishina Msangi amesema Januari 26 majira ya saa 06:00 asubuhi na kuendelea jeshi la polisi mkoa wa Mwanza linaendesha operesheni ya kukamata waendeshaji wa vyombo vya moto hasusani waendesha pikipiki (bodaboda) ambao hawafuati sheria, kanuni na taratibu za usalama barabarani. Aidha katika operesheni hii askari watakuwa wakikamata magari na waendesha pikipiki ambao hawana leseni, madereva na abiria wasio vaa kofia ngumu, kubeba abiria zaidi ya mmoja kwenye pikipiki (mshikaki), kukunja namba za usajili wa pikipiki, kuendasha wakiwa wamelewa na kutoboa au kuongeza ukubwa wa mafla. (exhaust), vitendo ambavyo ni kosa kisheria.


Aidha operesheni hii rasmi imekuja baadaya kutokea kwa matukio kadhaa ya ajali ambazo zimepelekea wananchi wengi kupoteza maisha na wengine kupata ulemavu wa kudumu, jeshi la polisi mkoa wa Mwanza kupitia kikosi cha usalama barabarani baada ya kuliona hilo lilianza kutoa elimu kupitia vyombo vya habari, kufanya vikao na vikundi vya waendesha bodaboda pamoja na kutoa elimu ya usalama barabarani kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.


Jeshi la Polisi baada ya kubaini hilo liliandaa gari maalumu la matangazo ambalo lilipita maeneo yote ya jiji la mwanza kwa muda wa siku tatu likiwataadharisha waendeshaji wa vyombo vya moto juu kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za usalama barabarani, lakini pia juu ya kufanyika kwa operesheni ya kukamata madereva/ abiria wa vyombo vya moto ambavyo vitakuwa vimekiuka sheria ya usalama barabarani.


Operesheni tayari imeanza kufanyika katika maeneo yote ya jiji la Mwanza, tayari askari wamefanikiwa kukamata pikipiki 217 na bajaji 27, ambazo zilikutwa na makosa mbalimbali ya usalama barabarani.


Aidha abiria 31 wa pikipiki wamekamtwa kwa kushindwa kuvaa kofia ngumu pindi walipokuwa wanaendeshwa barabarani, aidha taratibu za kuwafikisha mahakamani madereva na abiria ambao walipatikana na makosa ya usalama barabarani zinaendelea.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad