Kilimo Kwanza : Mzee Malecela amuomba Mkuu wa Mkoa Dodoma Kufufua zao la Zabibu - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


9 Jul 2016

Kilimo Kwanza : Mzee Malecela amuomba Mkuu wa Mkoa Dodoma Kufufua zao la Zabibu


Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu Mzee John Samwel Malecela amemuomba Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Jordan Rugimbana kufufua zao la Zabibu Mkoani humo kwa kuzishughulikia changamoto zinazodidimiza kilimo cha zao hilo.

Mzee Malecela pia amemtaka Mheshimiwa Rugimbana kutekeleza agizo la Mheshimiwa Rais Magufuli la kuondoa Tatizo la njaa Mkoani Dodoma kwa  kuzifuatilia skimu zote za kilimo zinazolegalega na zile zilizokosa uongozi imara.

Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki walipoambatana na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Jordan Rugimbana kwenye ziara ya kukagua skimu ya umwagiliaji ya zabibu ya Chinangali II yenye jumla ya ekari 1,250 iliyopo Chamwino ambayo kwa sasa inalegalega na kumtaka Mkuu wa Mkoa kuingilia kati kunusuru skimu hiyo inayokabiliwa na changamoto za kukosa uongozi imara na uendeshaji wa kilimo usio zingatia kanuni za kilimo bora.

Aliitaka serikali kusaidia wakulima wa chama cha CHABUMA wanaomiliki skimu hiyo ya zabibu ya Chinangali ili waweze kuanzisha kiwanda cha kusindika mchuzi wa zabibu na kusema kuwa kufanya hivyo kutawaepusha wakulima wa zabibu dhidi ya wafanyabiashara walanguzi wanaowalalia wakulima wakati wa mavuno ya zabibu.

Katika hatua nyingine, Mzee Malecela amemtaka Mheshimiwa Rugimbana kuondoa tatizo la njaa kwenye Mkoa wa Dodoma kwa kufufua skimu zote zilizokufa na zile zinazolegalega Mkoani hapa ili ziweze kuzalisha chakula na ametaka mkazo mkubwa uwekwe kwenye kilimo cha umwagiliaji kwa kuwa Mkoa wa Dodoma una maji mengi chini ya ardhi.

Amesema serikali inaingia gharama kubwa sana kuanzisha skimu za umwagiliaji lakini nyingi zinakosa ufuatiliaji na uongozi imara matokeo yake zinakufa akitolea mfano skimu ya Mgangalenga iliyopo Mpwayungu Chamwino yenye zaidi ya Ekari 20,000. Kwa mujibu wa Katibu Tawala msaidizi wa Uchumi na Uzalishaji Bi. Aziza Mumba amesema Mkoa wa Dodoma una skimu za umwagiliaji zipatazo mia tatu (300).

Mkuu wa Mkoa Mheshimiwa Rugimbana amekubali ushauri huo na kuahidi kuufanyia kazi kwakuwa agizo la kuondoa njaa ni moja ya maagizo aliyopewa na Mheshimiwa Rais Magufuli. Amesema kwanza atakua mlezi wa skimu ya zabibu ya Chinangali, na kuwa atafanya jitihada za kutafuta wafadhili kwa lengo la kuwezesha mradi wa kiwanda cha kusindika mchuzi wa zabibu.

Pamoja na   kutembelea skimu hiyo ya Chinangali, Mkuu wa Mkoa ameahidi atazitembelea skimu zote mia tatu (300) ili kubaini changamoto za kila skimu na kuahidi kuzitafutia ufumbuzi ili zote ziweze kuzalisha kisasa na kusaidia katika jitihada za kuondoa tatizo la njaa.

Rugimbana amesema tayari ameshaunda kikosi kazi kwa ajili ya kushughulikia masuala ya uzalishaji katika miradi ya Kilimo na Mifugo na moja kati ya jukumu kubwa alilokipa kikosi kazi hiko ni kubaini changamoto za skimu hizi za umwagiliaji, kuhakikisha kinakua nazo karibu na kuzijengea uwezo ikiwa ni pamoja na kuimarisha uongozi wa skimu hizo zote na uzalishaji kwa ujumla.
Waziri Mkuu na Makamu wa kwanza wa Rais mstaafu Mzee John Samwel Malecela akiwa ameongozana na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Jordan Rugimbana wakisalimiana na Viongozi wa skimu ya Umwagiliaji ya zabibu iliyopo Chinangali II Chamwino wakati walipotembelea skimu hiyo mwishoni mwa wiki.
Afisa Kilimo Wilaya ya Chamwino Ndg. Godfrey Mnyamale akiwasilisha taarifa ya mradi wa skimu ya Umwagiliaji wa zabibu ya Chinangali II kwa mkuu wa Mkoa wa Dodoma Jordan Rugimbana na Mzee Malecela (hawapo pichani) wakati walipotembelea skimu hiyo mwishoni mwa wiki. Wengine ni viongozi wa skimu hiyo.
Waziri Mkuu na Makamu wa kwanza wa Rais mstaafu Mzee John Samwel Malecela akimweleza Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Jordan Rugimbana (kushoto) changamoto zinazo didimiza kilimo cha Zabibu Dodoma na kumtaka kufanya kila awezalo kufufua zao hilo sambamba na kuondoa tatizo la njaa Dodoma wakati viongozi hao walipotembelea skimu ya Umwagiliaji wa zabibu ya Chinangali II mwishoni mwa wiki.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Jordan Rugimbana akiahidi kufufua zao la zabibu Mkoani humo na kuondoa tatizo la njaa kwa kufufua skimu zote za umwagiliaji zinazolegalega na kukosa uongozi imara wakati akizungumza na viongozi wa skimu ya umwagiliaji wa Zao la zabibu iliyopo Chinangali II Chamwino mwishoni mwa wiki.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Jodan Rugimbana na Waziri Mkuu na Makamu wa kwanza wa Rais mstaafu Mzee John Samwel Malecela wakikagua mitambo ya kusukuma maji kwenye skimu ya Umwagiliaji ya zabibu iliyopo Chinangali II Chamwino wakati viongozi hao walipotembelea skimu hiyo mwishoni mwa wiki, wengine ni viongozi wa skimu hiyo.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Jodan Rugimbana na Waziri Mkuu na Makamu wa kwanza wa Rais mstaafu Mzee John Samwel Malecela wakikagua miundombinu ya maji kwenye skimu ya Umwagiliaji ya zabibu iliyopo Chinangali II Chamwino wakati viongozi hao walipotembelea skimu hiyo mwishoni mwa wiki, wengine ni viongozi wa skimu hiyo.
Waziri Mkuu na Makamu wa kwanza wa Rais mstaafu Mzee John Samwel Malecela na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Jodan Rugimbana wakikagua shamba la zabibu la Chinangali II Chamwino linalotumia teknolojia ya Umwagiliaji wa matone wakati viongozi hao walipotembelea skimu hiyo mwishoni mwa wiki, wengine ni viongozi wa skimu hiyo.
Waziri Mkuu na Makamu wa kwanza wa Rais mstaafu Mzee John Samwel Malecela akimuonesha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Jodan Rugimbana jinsi tatizo la fangasi linavyoshambulia zao la zabibu wakati wakikagua shamba la zabibu la Chinangali II Chamwino wakati viongozi hao walipotembelea skimu hiyo mwishoni mwa wiki, wengine ni viongozi wa skimu hiyo.
Sehemu ya Skimu ya zabibu ya Chinangali II iliyopo Chamwino inayotumia teknolojia ya umwagiliaji wa matone, kwa sasa skimu hiyo na nyingine baadhi Mkoani humu zinalegalega kutokana na kukabiliwa na Changamoto kadhaa wa kadhaa ambazo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Jordan Rugimbana ameahidi kuzitafutia ufumbuzi.
Sehemu ya kitalu cha kuzalisha miche kwenye Skimu ya zabibu ya Chinangali II iliyopo Chamwino, kwa sasa skimu hiyo na nyingine baadhi Mkoani humu zinalegalega kutokana na kukabiliwa na Changamoto kadhaa wa kadhaa ambazo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Jordan Rugimbana ameahidi kuzitafutia ufumbuzi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad