ELIMU KWA WOTE :SHULE YA SEKONDARI YA WAMA-NAKAYAMA YAPATA MSAADA WA DOLA LAKI MOJA UDHAMINI WA WANAFUNZI WA KIKE KATIKA SHULE HIYO - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


29 Jan 2014

ELIMU KWA WOTE :SHULE YA SEKONDARI YA WAMA-NAKAYAMA YAPATA MSAADA WA DOLA LAKI MOJA UDHAMINI WA WANAFUNZI WA KIKE KATIKA SHULE HIYO


Na Anna Nkinda – Maelezo
Taasisi ya Fursa ya  Elimu (Opportunity Education Foundation) ya nchini Marekani imetoa mchango wa dola za kimarekani laki moja kwa ajili ya udhamini wa wanafunzi wa kike ambao ni yatima na wanaotoka katika mazingira hatarishi katika shule ya Sekondari ya WAMA-Nakayama iliyopo wilaya ya Rufiji mkoani Pwani.
Fedha hizo ambazo ni zaidi ya shilingi milioni mia moja na  sitini na mbili  zitaweza  kuwasomesha wanafunzi 75 kwa kipindi cha mwaka mzima kwa kuwapatia malazi, chakula, sare za shule, viatu, shajara, vitabu na mahitaji mengine ya kila siku ya mwanafunzi.

Hayo yamesemwa jana na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) ambao ndiyo wamiliki wa shule hiyo wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa mradi wa laptop ndogo (tablets computer) uliofanyika shuleni hapo jana.  
Mama Kikwete pia alimpongeza  Joe Ricketts ambaye ni mwanzilishi na mtendaji mkuu wa Fursa ya  Elimu kwa moyo wa upendo alionao na dhamira ya kuisaidia jamii ya watanzania kwa kutambua kwamba kupata elimu bora kwa wanafunzi wote ni ufunguo wa kuwa na afya bora, uchumi imara, miundombinu bora na ya kutosha, jamii yenye uelewa jambo ambalo litasababisha ustadi wa taifa kunasonga mbele.
Mwenyekiti huyo wa WAMA alisema , “Kwa mantiki hiyo ningependa kusema kwamba kukosekana kwa fursa ya kumpatia mtoto wa kike elimu bora ni kulikosesha taifa fursa ya maendeleo kwani kadri mtoto wa kike anavyopata elimu ndivyo anavyoweza kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi na ataweza kuboresha uzazi wa mpango, afya ya mtoto na kujiongezea kipato”.
Akizungumzia kuhusu mradi wa laptop ndogo (tablets) ambapo shule hiyo ilipata 61  Mama Kikwete  aliiomba Taasisi hiyo na wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kuangalia uwezekano wa kuongeza mitaala ya mafunzo ya kitanzania ili iwasaidie wanafunzi kumudu masomo wanayofundishwa darasani halikadhalika kuandaa mkakati wa kuzifikia shule zilizopo pembezoni ambazo zinakuwa na uhaba wa walimu.
“Ninawaasa walimu na wanafunzi wa shule hii na kupitia wanafunzi wa shule zitakazofaidika na mpango huu kutumia vifaa hivi kwa mahitaji ya masomo kama ilivyokusudiwa na siyo kupoteza muda kwa michezo isiyo na manufaa. Napenda mjione kama watu wenye bahati ambao mmepata fursa ya kipekee ambayo wanafunzi wengi nchini hawana, mvitunze vifaa hivi ili viwafae wanafunzi wengine watakaokuja baada yenu”, alisisistiza Mama Kikwete.
Kwa upande wake Ricketts alisema kwa mara ya kwanza alikuja nchini mwaka 2006 wakati anaelekea   Serengeti alikuta mwalimu mmoja anafundisha wanafunzi zaidi ya miamoja aliamua  kuanzisha  mahusiano na shule hiyo ambayo aliwapelekea vifaa mbalimbali vya kufundishia. 
Alisema lengo la  kuanzishwa kwa Taasisi yake ni kutoa msaada wa kielimu ikiwa na nia ya kufanya upatikanaji wa elimu bora kwa wanafunzi kutoka nchi zinazoendelea ili wale wanaotoka katika familia maskini waweze kusoma na kupata ajira pale watakapokuwa wamemaliza masomo yao na hivyo kujikwamua na hali ngumu ya maisha. 
“Vijana wadogo wanategemea kupata elimu bora kwa kuwa  elimu kwa wanafunzi imegawanyika katika sehemu mbili ambazo ni technolojia na mwanafunzi mwenyewe kukuwa na kukomaa kiakili ili aweze  kufanya vizuri katika masomo yake.
Kama mradi huu utafanikiwa walimu watakuwa na mwamko mkubwa wa kufundisha na nitahakikisha kuwa zinapatikana laptop ndogo (tablets) za kutosha kwa ajili ya kusomea nchini kwani matokeo ya maisha ya watoto  wetu yanategemea elimu wanayoipata” , alisema Ricketts.
Taasisi ya Fursa ya  Elimu ilianzishwa mwaka 2005 na kusajiliwa nchini mwaka 2006 walianza kufanya kazi na shule moja ya msingi na hadi kufikia sasa  shule 434 zikiwemo za Sekondari 33 zimenufaika kwa kupata vitabu, DVD na zana za kufundishia.
Kwa shule za sekondari wanatoa mwongozo wa mwalimu ambao unamuongoza kirahisi jinsi ya kuwafundisha wanafunzi , laptop ambazo zinamasomo yaliyorekodiwa ambayo ni ya sayansi, hesabu, kiingereza na maarifa ya jamii ,projecta na Televisheni ambazo zinasaidia kuonyesha masomo na vitabu na video inawasaidia wanafunzi kujifunza somo la kiingereza kwa njia ya kusikiliza na kusoma.
Wanafunzi watakaonufaika na program hiyo ni wa kidato cha pili kutoka  shule za Sekondari Ilboru,(Arusha) Mzumbe (Morogoro),  Msalato, (Dodoma),FidelCastro (Pemba), WAMA - Nakayama (Pwani), shule ya Sekondari ya wavulana Bwiru (Mwanza), J Ossian (Bukoba), Laureatte
(Zanzibar), Notredame (Arusha) na Tusiime (Dar es Salaam).

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad