MICHEZO TANZANIA : LOWASSA ATAKA TIJA KATIKA MICHEZO YOTE - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


29 Jan 2014

MICHEZO TANZANIA : LOWASSA ATAKA TIJA KATIKA MICHEZO YOTE





Waziri Mkuu Mstaafu na Mbunge wa Jimbo la Monduli,Mh. Edward Lowassa 
 Dar es Salaam. Mwenyekiti Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Edward Lowassa amesema juhudi anazofanya Rais Jakaya Kikwete katika kuinua sekta ya michezo nchini bado mafanikio yake hayaridhishi.

Kutokana na hali hiyo, Lowassa ameitaka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuchukua hatua za makusudi ili kuhakikisha tija inapatikana kwenye sekta hiyo ya michezo na kuwanufaisha vijana.

Lowassa alisema hayo katika hafla fupi ya kumuaga Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Juma Nkamia.

Hafla hiyo iliandaliwa na kamati hiyo ya mambo ya nje na ilifanyika kwenye Ofisi ndogo za Bunge, jijini Dar es Salaam, ambapo Nkamia alikuwa ni miongoni mwa wajumbe wa kamati hiyo kabla ya kuchaguliwa kuwa Naibu Waziri.

“Rais Kikwete atakumbukwa kwa jitihada zake alizofanya katika kuwekeza kwenye michezo, lakini bado hakuna mafanikio yaliyotarajiwa, Jamali Malinzi alikuja kwangu nina imani ana nia ya kuendeleza soka,” alisema Lowassa.

Aliongeza,“ Ingawa watu wengine walihoji ujio wake kwangu, lakini mimi naona mwelekeo wa maendeleo chini ya uongozi wake, naomba wizara yako iwe karibu na vyombo vinavyosimamia michezo,” alisisitiza Lowassa.

Naye Mjumbe wa Kamati hiyo, Suzan Lyimo alisema suala la michezo bado liko nyuma sana hususan upande wa wanawake hivyo akamwomba Nkamia kuhakikisha anatafuta mbinu mbadala za kuzisaidia timu za taifa.

Kwa upande wake, Nkamia alisema amekutana na viongozi wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT) kwa lengo la kuzungumza ni jinsi gani timu za taifa zitaweza kusaidiwa kwa njia zozote zile.

“Tukitegemea wadhamini hatuwezi kufika, kwani nao wadhamini wanaangalia maeneo ambayo yatawalipa hivyo sisi wenyewe lazima tuangalie ni njia zipi zinaweza kusaidia timu zetu zote za taifa,” alisema Nkamia. Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad