Miundombinu: Japan Yaipiga Jeki Tanzania Ujenzi wa Barabara za Mzunguko Jijini Dodoma - Wazalendo 25 Blog

Glory to Story.

Habari Mpya

PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0784 643 633


PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0676 643 633

Thursday 17 October 2024

Miundombinu: Japan Yaipiga Jeki Tanzania Ujenzi wa Barabara za Mzunguko Jijini Dodoma

Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba na Balozi wa Japan nchini Tanzania Mhe. Yasushi Misawa wakisaini mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 68.5 kwa ajili ya kugharamia mradi wa ujenzi wa barabara za mzunguko za ndani za jiji la Dodoma, katika hafla ilyofanyika jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba na Balozi wa Japan nchini Tanzania Mhe. Yasushi Misawa wakibadilishana mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 68.5 kwa ajili ya kugharamia mradi wa ujenzi wa barabara za mzunguko za ndani za jiji la Dodoma, katika hafla ilyofanyika jijini Dar es Salaam.

Na Farida Ramadhani, WF, Dar es Salaam
JAPANI, kupitia Shirika lake la Ushirikiano wa Kimataifa (JICA), imeipatia Tanzania msaada wa yen bilioni 4.07 sawa na shilingi bilioni 68.5 za Tanzania kwa ajili ya kutekeleza mradi wa ujenzi wa Barabara ya mzunguko wa ndani katika Jiji la Dodoma.
Mkataba wa Msaada huo umetiwa Saini katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jijini Dar es Salaam, kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha ambaye pia ni Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-maamry Mwamba kwa upande wa Tanzania, Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mhe. Yasushi Misawa na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Japan (JICA), Hitoshi Ara.

Akizungumza baada ya kusaini mkataba huo, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, alisema kuwa Mradi huo utahusisha upanuzi wa barabara kutoka njia mbili hadi nne kuanzia mzunguko wa barabara ya Bahi hadi Image na ujenzi wa barabara mpya ya njia nne kuanzia mzunguko wa barabara ya Image hadi mzunguko wa barabara ya Makulu.

“Mradi wa Ujenzi wa Barabara za Mzunguko wa Ndani ya Jiji la Dodoma, unaendana na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2021/22 – 2025/26) wenye maudhui ya kufikia ushindani na viwanda kwa ajili ya maendeleo ya watu ambao unalenga kuongeza ufanisi na uzalishaji kwa kutumia rasilimali zilizopo” alisema Dkt. Mwamba.

Dkt. Mwamba alisema mikataba hiyo ni mwendelezo wa ushirikiano imara kati ya Tanzania na Japan ambapo Tanzania imenufaika na ufadhili wa Japan kwa njia ya misaada na mikopo nafuu katika maeneo ya sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, maji, afya, nishati, usafirishaji na maendeleo ya miji, usimamizi bora wa fedha za umma pamoja na elimu.

Kwa upande wao, Balozi wa Japan Nchini Tanzania, Mhe. Yashushi Misawa na Mwakilishi Mkazi wa (JICA), Bw. Hitoshi Ara, walisema kuwa mradi huo ni muhimu kwa maendeleo ya nchi kwa kuwa Dodoma ni Jiji ambalo lipo katika korido ya katikati ambayo inazidi kuwa muhimu kama njia kuu ya uchumi unaokua kwa kasi Afrika Mashariki.

Walisema kupitia mkataba hiyo Japani itajenga takribani kilomita 3.1 za Barabara ya mzunguko na kupanua takribani kilomita 3.4 za Barabara ndani ya Jiji la Dodoma ambazo zitasaidia kuzuia magari makubwa kuingia mjini ili kukabiliana na athari za kimazingira.

Waliahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania na kubaninisha kuwa mikataba hiyo ni ishara tosha ya uhusiano mzuri uliopo kati yq nchi hizo mbili.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Dkt. Charles Msonde , alisema Wizara hiyo itasimamia kikamilifu fedha hizo na kuhakikisha mradi huo unatekelezwa kama ilivyopangwa.

Alisema kuwa mradi huo unatarajiwa kutatua changamoto mbalimbali za miundombinu katika Jiji la Dodoma kwa kuwa baada ya Serikali kuhamia katika Jiji hilo mahitaji ya miundombinu mbalimbali ikiwemo barabara yameongezeka.

Alitaja baadhi miradi iliyotekelezwa kwa kushirikiana na Japan ikiwemo Daraja la Gerezani, upanuzi wa Barabara ya Bagamoyo pamoja na ujenzi wa Daraja la Rusumo.
Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Dkt. Natu Elmaamry Mwamba na Balozi wa Japan nchini Tanzania Mhe. Yasushi Misawa wakionesha mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 68.5 kwa ajili ya kugharamia mradi wa ujenzi wa barabara za mzunguko za ndani za jiji la Dodoma, baada ya kuisaini katika hafla ilyofanyika jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba na Mwakilishi Mkazi wa (JICA), Bw. Hitoshi Ara wakipeana mikono baada ya kusaini mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 68.5 kwa ajili ya kugharamia mradi wa ujenzi wa barabara za mzunguko za ndani za jiji la Dodoma, katika hafla ilyofanyika jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba akizungumza baada ya kusaini mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 68.5 kwa ajili ya kugharamia mradi wa ujenzi wa barabara za mzunguko za ndani za jiji la Dodoma, katika hafla ilyofanyika jijini Dar es Salaam.
Balozi wa Japan nchini Tanzania Mhe. Yasushi Misawa akizungumza baada ya kusaini mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 68.5 kwa ajili ya kugharamia mradi wa ujenzi wa barabara za mzunguko za ndani za jiji la Dodoma, katika hafla ilyofanyika jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba na Balozi wa Japan nchini Tanzania Mhe. Yasushi Misawa wakiteta jambo baada ya kusaini mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 68.5 kwa ajili ya kugharamia mradi wa ujenzi wa barabara za mzunguko za ndani za jiji la Dodoma, katika hafla ilyofanyika jijini Dar es Salaam.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikali, Wizara ya Fedha – Dar es Salaam)

No comments:

Post a Comment