Mfuko wa Jamii : Wastaafu wanaolipwa na Hazina Wasiohakikiwa kuondolewa kwenye Malipo ya Pensheni - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


7 Feb 2017

Mfuko wa Jamii : Wastaafu wanaolipwa na Hazina Wasiohakikiwa kuondolewa kwenye Malipo ya Pensheni


Na Benny Mwaipaja-WFM, Mtwara


WIZARA ya Fedha na Mipango, imesema kuwa wastaafu wanaolipwa na Wizara hiyo ambao hawatahakikiwa wataondolewa kwenye orodha ya malipo ya pensheni kwa kuwa watakuwa wamekosa sifa.


Kauli hiyo imetolewa Mjini Mtwara na Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali Msaidizi, Bw. Stanslaus Mpembe, wakati wa uzinduzi wa uhakiki wa wastaafu wanaolipwa pensheni zao na Wizara hiyo katika Mikoa ya Lindi na Mtwara.


Alisema kuwa lengo la uhakiki huo ni kuiwezesha Wizara kuhuisha taarifa za wastaafu ili kupata kanzidata (database) iliyo sahihi, kuwatambua wastaafu na kuiwezesha serikali kulipa wastaafu wanaostahili.


“Kwa kuwa zoezi hilo ni la lazima na kwa wale wastaafu ambao hawajahakikiwa kwa sababu mbalimbali katika mikoa ambayo uhakiki umekamilika watalazimika kufika katika ofisi za Hazina katika mikoa husika na kujiandikisha na baada ya uhakiki kukamilika wataelekezwa utaratibu utakaotumika kuwahakiki” aliongeza Bw. Mpembe


Aidha Bw. Mpembe alisisitiza wastaafu hao kufika wenyewe na sio kutuma wawakilishi, wakiwa na nyaraka zote muhimu zikiwemo barua ya tuzo la kustaafu, barua ya kustaafu au kupunguzwa kazini, nakala ya hati ya malipo ya kiinua mgongo au mkupuo, barua ya ajira ya kwanza, kitambulisho cha pensheni, barua ya kuthibitishwa kazini, kadi ya benki na picha mbili ndogo zilizopigwa hivi karibuni.


Akijibu kuhusu malalamiko ya pensheni ndogo kwa wastaafu, Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali Msaidizi, Bw. Stanslaus Mpembe, amesema kuwa watakapo kamilisha zoezi la uhakiki wataandaa taarifa namna zoezi zima lilivyo endeshwa na kuiwasilisha kwa uongozi wa juu wa Wizara, likiwemo suala hilo la malalamiko ya pensheni ya wastaafu.


Kwa upande wa wastaafu kutoka taasisi mbalimbali za Serikali wanaolipwa na Wizara ya Fedha na Mipango wameiomba Serikali iwaongezee viwango vya pensheni wanavyo lipwa ili waweze kujikimu kimaisha kutokana na hali ya maisha kuwa ngumu.


Akitoa maoni katika zoezi la uhakiki wa wastaafu linaloendelea katika mkoa wa Lindi na Mtwara, Mstaafu David Christopher Mtakula, amesema utaratibu wa kuhakiki taarifa za wastaafu ni njia nzuri ili kujiridhisha kuwa wanaolipwa ndio wanaostahili.


Zoezi hili la uhakiki linaloendelea katika mikoa ya Lindi na Mtwara lilianza Oktoba 20, 2016 katika mkoa wa Pwani na limeshafanyika katika mikoa 23 ya Tanzania Bara ambayo ni Mbeya, Iringa, Njombe, Ruvuma, Songwe, Katavi, Rukwa, Morogoro, Dodoma, Singida, Arusha, Kilimanjaro, Manyara, Tanga, Mwanza, Kagera, Mara, Shinyanga, Simiyu, Geita, Kigoma na Tabora.


Mkaguzi wa ndani wa Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara, Bw. Hussein Mussa, pamoja na maafisa wengine wakiendelea na zoezi la uhakiki wa wastaafu wanaolipwa na Wizara ya Fedha na Mipango, mkoani Mtwara. 


Baadhi ya Wastaafu wanaolipwa na Wizara ya Fedha na Mipango, wakikagua nyaraka zao muhimu kabla ya kufika katika dawati la huduma kwenye zoezi la uhakiki linaloendelea mkoani Mtwara

Afisa TEHAMA Mwandamizi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Jacqueline Nyamugali (wa kwanza kushoto) akiwa na maafisa wengine, wakitoa maelekezo kuhusu nyaraka muhimu za mmojawapo ya wastaafu wanaolipwa na Wizara ya Fedha na Mipango wakati wa zoezi la uhakiki linaloendelea mkoani Mtwara.

Kaimu Mhasibu Mkuu Pensheni, Scolastica Mafumba, akikagua nyaraka na kutoa maelekezo muhimu kwa mmojawapo ya wastaafu wanaolipwa pensheni na Wizara ya Fedha na Mipango waliofika kuhakikiwa mjini Mtwara.

Mkaguzi wa ndani wa Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Bi. Imelda Mmbaga akimhudumia mmoja wa wastaafu wanaolipwa na Wizara ya Fedha na Mipango, wakati wa zoezi la uhakiki linaloendelea katika mikoa ya Lindi na Mtwara Mtwara.

Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali Msaidizi, Bw. Stanslaus Mpembe, akiongea na waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini kuhusiana na zoezi zima la uhakiki wa wastaafu wanaolipwa na Wizara ya Fedha na Mipango linaloendelea katika mikoa ya Lindi na Mtwara.


(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-WFM)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad