Matukio : Mhe. Said Meck Sadick apiga marufuku utoaji wa vibali vya malori ya mizigo yenye uzito wa zaidi ya tani 10 kuingia katikati ya jiji - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


3 Mar 2016

Matukio : Mhe. Said Meck Sadick apiga marufuku utoaji wa vibali vya malori ya mizigo yenye uzito wa zaidi ya tani 10 kuingia katikati ya jiji

Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Saidi Mecki Sadiki akizungumza na wajumbe wa Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Dar es salaam kwenye kikao cha kwanza cha Bodi hiyo kwa mwaka 2016. Kulia ni Zungu Azzan na Kushoto ni Bw. Edward Otieno Kaimu Katibu Tawala wa mkoa huo.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala Bw.Isaya Mngurumi akichangia jambo kuhusu uboreshaji wa miundombinu ya barabara katika Manispaa yake wakati wa Kikao cha kwanza cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Dar es salaam.
Mkuu wa Wilaya ya Temeke Sophia Mjema akichangia jambo wakati wa wakati wa Kikao cha kwanza cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Dar es salaam kwa mwaka 2016.
Baadhi ya Wabunge wa jiji Dar es salaam wakifuatilia kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Dar es salaam. Kutoka kulia ni Mhe. Bonnah Kalua - Mbunge wa Segerea, Mhe. Faustine Ndugulile - Mbunge wa Kigamboni, Mhe. Zungu Azzan – Mbunge wa Ilala na Mhe. Abdallah Mtolea – Mbunge wa Temeke.
Meneja wa Wakala wa Barabara Mkoa wa Dar es salaam Muhandisi Julius Ndyamkama akitoa ufafanuzi kwa wajumbe wa kikao cha Bodi ya Barabara mkoa wa Dar es salaam kuhusu miradi ya ujenzi wa Barabara inayosimamiwa na Wakala hiyo. Picha na Aron Msigwa – MAELEZO.

Na. Aron Msigwa – MAELEZO.

Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Saidi Mecki Sadiki amepiga marufuku utoaji wa vibali vya malori ya mizigo na magari yenye uzito wa zaidi ya tani 10 kuingia katika barabara zote zinazosimamiwa na Manispaa za jiji la Dar es salaam zilizojengwa kwa kiwango cha lami kufuatia barabara hizo kuharibika kwa kipindi kifupi kutokana uzito jambo linaloisababishia Serikali hasara. 

Aidha, ameziagiza manispaa za jiji hilo kuweka alama za barabarani zinaonyesha zuio kwa magari yote yenye uzito wa zaidi ya tani 10 kupita kwenye barabara hizo ili wamiliki na madereva watakaokiuka agizo hilo wachukuliwe hatua kali za kisheria. 

Akizungumza na wajumbe wa Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Dar es salaam kwenye kikao cha kwanza kwa mwaka 2016 Mhe. Sadiki Meck Sadiki amesema kuwa Manispaa za jiji hilo zinatenga fedha nyingi za kujenga barabara mpya na kufanya matengenezo ya zile zilizopo ambazo nyingi zinaharibiwa na malori ya mizigo.

Amefafanua kuwa matumizi hayo mabaya ya barabara kwa kiasi kikubwa yanachangiwa na ukiukwaji wa sheria za barabarani ambapo malori makubwa ya mizigo huegesha na kuziba maeneo ya waenda kwa miguu jambo linalowanyima haki wananchi kutumia maeneo yaiyotengwa kwa ajili yao.

Amesema baadhi ya magari yenye uzito wa tani 40 hudiriki kupita kwenye barabara za huduma (Service road), madaraja na wakati mwingine maeneo ya waenda kwa miguu jambo linalosababisha uvunjaji wa kingo za barabara na milingoti ya taa za barabarani na kuongeza kuwa vitendo hivyo vinaisababishia Serikali hasara kutokana na gharama ya matengenezo.

“Kuanzia leo katika mkoa wangu ni marufuku kutoa vibali vya magari yenye uzito wa zaidi ya tani 10 kuingia kwenye barabara zetu, tunataka barabara zetu zidumu, hatuwezi kuvumilia vitendo vya watu wachache wanaokiuka sheria za barabarani kuharibu barabara zetu, lazima tuchukue hatua Manispaa zinajitahidi kujenga bararaba lakini hazidumu” Amesisitiza Mhe. Sadiki.

Amesema barabara zinazosimamiwa na Manispaa za Dar es salaam zina uwezo wa kuhimili uzito wa tani 10 na kubainisha kuwa kwa kipindi kirefu malori ya tani 40 yamekuwa yakipita kwenye barabara hizo na kuzifanya manispaa kunajenga barabara hizo kila mwaka. 

Mhe. Sadiki amesema kuwa ipo haja ya mamlaka zinazohusika na miundombinu ya barabara katika jjiji la Dar es salaam kwa kuwatumia wataalam wa sheria kuanza kuangalia uwezekano wa wamiliki wa vyombo vinavyosababisha uharibifu wa miundombinu ya barabara kulipa gharama za uharibifu huo.

Kuhusu ulinzi na Usalama watumiaji wa barabara za jiji amelitaka Jeshi la Polisi kuendelea kuchukua hatua na kufanya Operesheni dhidi ya madereva wa pikipiki (Bodaboda) na Bajaji wanaopitisha vyombo vyao vya usafiri kwenye njia za waenda kwa miguu na kusababisha usumbufu na ajali za mara kwa mara kwa wananchi wanaotumia njia hizo.

Pia amezitaka Manispaa za jiji hilo kushirikiana na Wakala wa Barabara (TANROADS) mkoa wa Dar es salaam kusimamia maeneo yote yanayotakiwa kujengwa miundombinu ya Barabara ili yasivamiwe na wananchi pamoja na kuwachukulia hatua wananchi wanaofanya biashara katika maeneo yasiyoruhusiwa ya hifadhi za barabara na njia za waenda kwa miguu. 

‘‘Ninaiagiza manispaa ya Kinondoni kuondoa wafanyabishara wote walioko eneo la kituo cha kuzalishia umeme Ubungo, eneo lile ni hatari kwa usalama na maisha yao, kukaa pale ni kinyume cha sheria’’ Amesisitiza.

Aidha, amesema mwaka 2016 mkoa wa Dar es salaam umetenga jumla ya Shilingi bilioni 343.5 ikilinganishwa na shilingi Biliobi 266.6 zilizotengwa mwaka mwaka 2015/2016 kutekeleza ujenzi na matengenezo ya barabara katika maeneo mbalimbali ya jiji hilo lengo likiwa kupunguza msongamano wa magari. 

Kuhusu Kikao hicho cha kwanza cha Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Dar es salaam kwa mwaka 2016 amesema pamoja mambo mengine kimepokea na kujadili tarrifa  utekelezwaji wa ujenzi wa miradi ya barabara kwa mwaka 2015/2016 pamoja na kupokea Mpango wa matengenezo ya barabara kwa mwaka 2016/2017.

Ametoa wito kwa wakazi wa jiji la Dar es salaam kuzingatia usafi wa mazingira kwa kulinda miundombinu ya barabara na kuepuka kutupa taka kwenye  mifereji  ya kupitisha maji ili kuzuia mlipuko wa magonjwa ukiwemo ugonjwa wa Kipindupindu.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad