Makala : Uhuru Kenyatta Anatumia Mbinu Zile zile Alizotumia Moi katika Utawala Wake - Wazalendo 25 Blog

Glory to Story.

Habari Mpya

PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0784 643 633


PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0676 643 633

Thursday 12 March 2015

Makala : Uhuru Kenyatta Anatumia Mbinu Zile zile Alizotumia Moi katika Utawala Wake

Uhuru na MoiRais Uhuru Kenyatta na Rais Mstaafu Daniel arap Moi walipokutana ikulu, Nairobi Agosti 1, 2013. Picha/PSCU 

Na BENSON MATHEKA

Kwa Mukhtasari
Serikali ya Jubilee imejitokeza kuwa marudio ya utawala wa miaka 24 wa Rais Mstaafu Daniel arap Moi na chama chake cha KANU. Wadadisi wanasema kuwa licha ya Rais Uhuru Kenyatta na Naibu William Ruto kujidai kuwa wanaongoza serikali ya kidijitali, wamezama katika mbinu ambazo hazilingani na kauli mbiu hiyo yao.


SERIKALI ya Jubilee imejitokeza kuwa marudio ya utawala wa miaka 24 wa Rais Mstaafu Daniel arap Moi na chama chake cha KANU.
Hii ni kutokana na mbinu ambazo watawala wa Jubilee wanatumia kuongoza nchi, ambazo zinalandana pakubwa na za utawala wa Moi aliyestaafu miaka 12 iliyopita.
Wachanganuzi wa siasa wanasema sababu kuu ya mbinu za utawala wa Moi na Kanu kujirudia ni kuwa viongozi wa Jubilee, Rais Uhuru Kenyatta na Naibu wake William Ruto walikuwa wanafunzi watiifu wa Moi kuhusu siasa na uongozi, na hivyo si ajabu wanatumia mtindo sawa na aliotumia katika utawala wake.
Wadadisi wanasema kuwa licha ya Rais Kenyatta na Bw Ruto kujidai kuwa wanaongoza serikali ya kidijitali, ukweli ni kuwa wamezama katika mbinu ambazo hazilingani na kauli mbiu hiyo yao.
Mbinu ambazo Jubilee imekopa kutoka kwa KANU ni pamoja na:
KUZIMA UHURU WA VYOMBO VYA HABARI
Katika utawala wa Moi, yalikuwa makosa makubwa kwa vyombo vya habari kukosoa serikali ama kufichua maovu na udhaifu wake. Wanahabari waliofanya hivyo waliandamwa vikali na hata kutupwa jela. Sheria za kudhibiti vyombo vya habari zilikuwa kali na Wakenya hawakuwa na uhuru wa kuamua habari ambazo wangetaka kupata. Vyombo huru vya habari vilinyimwa kibali na kwa muda mrefu KBC ndiyo pekee iliyopeperusha habari, nyingi yazo zikiwa kuhusu Moi na mawaziri wake.
Katika utawala wa Jubilee, mambo yamejirudia kwa Serikali kutumia mbinu mbalimbali kuzima uhuru wa vyombo huru vya habari. Thibitisho la majuzi kabisa ni hatua ya kuzimwa kwa televisheni nne kuu huru za NTV, QTV, KTN na Citizen. Hatua hii imehakikisha kuwa sauti huru, upinzani na wakosoaji wa serikali hawana nafasi ya kuwasilisha jumbe zao kwa wananchi.
Ishara nyingine ya kuzima uhuru wa habari ilijitokeza kwenye sheria tata za usalama ambazo zina vipengele vya kuwekea breki vyombo vya habari katika kufichua na kuripoti mambo fulani.
Mbali na sheria hizo, kuna sheria nyingi za mawasiliano na za kudhibiti vyombo vya habari zinazotoa adhabu kali.
Masuala haya yameonekana kurudisha nyuma mafanikio makubwa ya uhuru wa vyombo vya habari yaliyopatikana chini ya utawala wa Rais Mstaafu Mwai Kibaki, ambaye alihakikisha ukadamizaji wa vyombo vya habari ulioshuhudiwa chini ya utawala wa Moi umekomeshwa.

KUKADAMIZA MASHIRIKA YA KIJAMII.
Katika miaka 24 ya utawala wa Moi, mashirika ya kijamii yalichukuliwa kama adui kwa kukosoa serikali. Viongozi wa mashirika hayo waliandamwa usiku na mchana hasa enzi za kutetea utawala wa vyama vingi. Kwa kukandamiza mashirika haya, sauti ya mwananchi wa kawaida ilizimwa huku mashirika mengi yakipigwa marufuku serikali.
Chini ya kipindi cha miaka miwili, Serikali ya Jubilee inajaribu mbinu za kila aina kukabiliana na mashirika ya kijamii kwa kupiga marufuku baadhi yao ikisema kwamba hayakuwa yametimiza masharti yanayohitajika.
Pia kuna sheria ambazo zimependekezwa za kuzima mashirika hayo, jambo ambalo wadadisi wanasema ni katika juhudi za Jubilee kuzima wakosoaji wake. Kwa kufanya hivi, wadadisi wanasema Jubilee itakuwa imeua demokrasia na kurudisha nchi enzi za utawala wa kiimla.

AHADI TUPU ZA KUKABILI UFISADI
Serikali ya Moi ilikuwa mstari wa mbele kutumia kila aina ya hafla kuwaonya maafisa wafisadi katika serikali kwamba wangefutwa kazi wakipatikana, lakini vitendo vilikuwa vichache mno. Kadri Moi alivyoapa kupambana na ufisadi, ndivyo wanasiasa na maafisa wakuu walivyoutekeleza bila kuchukuliwa hatua za kisheria. Kashfa za mabilioni ya pesa ikiwemo ya kihistoria ya Goldenberg zilikuwa matunda ya ufisadi huo, mashirika ya kiserikali na taasisi za kifedha ziliporomoka kutokana na viwango vya juu vya ufisadi na hatimaye uchumi wa nchi karibu uporomoke kabisa. Wanasiasa na watu mashuhuri walitumia pesa walizopora kufungua akaunti za benki na kuwekeza nchi za ng’ambo kuficha maovu yao.
Wataalamu wa uchumi na watetezi wa haki za binadamu wanasema sawa na serikali ya Moi, Rais Kenyatta amemwiga Moi kwa kutoa ahadi kila uchao za kupambana na ufisadi, lakini bila kuchukua hatua zozote. Maafisa waliohusishwa na kashfa mbalimbali wangali wanashikilia nyadhifa za juu katika serikali huku Tume ya Kupambana na Ufisadi (EACC), Idara ya Polisi na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) wakisema wanaendeleza uchunguzi, ambao matunda yake hayaonekani.
Ufisadi umerudi katika taasisi nyingi, jambo linalonyima serikali mapato huku wafanyabiashara wakubwa wakubwa wakikwepa kulipa kodi. Japo serikali ya Jubilee imekuwa ikiapa kuwafuta kazi maafisa wafisadi, kufikia sasa waliotajwa hawajachukuliwa hatua na hali inaendelea kwenye mkondo sawa na ilivyokuwa chini ya Moi.

KUBADILISHA SHERIA KIHOLELA
Ilikuwa kawaida kwa serikali ya Moi kutumia bunge kubadilisha baadhi ya vifungu vya sheria ili kutimiza malengo ya muda mfupi au iliyohisi ilikuwa kizingiti kuafikia malengo ya serikali na ya kibinafsi bila kujali maslahi ya mwananchi wa kawaida. Kwa sababu ya kuwa na idadi kubwa ya wabunge wa KANU, mabadiliko hayo yalipita kwa urahisi na athari zake kujitokeza baadaye.
Kwa miaka miwili ambayo imekuwa mamlakani, Serikali ya Jubilee imependekeza mabadiliko kadhaa tata ya kisheria, ikiwemo sheria za mawasiliano na usalama ambazo upinzani na baadhi ya wanaharakati walipinga. Hata hivyo serikali imetetea mabadiliko ya kisheria ikisema yanalenga kuimarisha huduma na usalama kwa Wakenya.

KUVURUGIKA KWA SEKTA YA KILIMO
Chini ya uongozi wa Moi, sekta ya kilimo, ambayo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa Kenya, ilivurugika. Kilio kilitanda kote miongoni mwa wakulima wa kahawa, chai, sukari na wafugaji wa ng’ombe wa maziwa. Bei zilishuka na hata malipo kukosekana, hali iliyofanya uzalishaji wa mazao kushuka kwa kiwango kikubwa hivi kwamba hadi sasa sekta ya kilimo ingali chini. Viwanda vya mazao ya kilimo vilifungwa kwa mfano KCC cha maziwa na KMC cha nyama huku mashirika ya wakulima yakiporomoka.
Kibaki alipochukua uongozi 2003 alifanya bidii kuinua kilimo kwa kufufua viwanda vya bidhaa za kilimo, mashirika ya wakulima na kuweka sera za kuwatia wakulima moyo kama vile kupunguza viwango vya ushuru wa pembejeo na mazao.
Lakini chini ya utawala wa Jubilee, sekta ya kilimo imeonekana kurudia hali ya enzi za Moi ambapo ushuru wa juu kwa pembejeo na bidhaa za kilimo umerudi, uingizaji wa bidhaa za kigeni kama vile sukari kimagendo umeongezeka na sasa sekta za chai, sukari, kahawa miongoni mwa zingine zinakumbwa na matatizo si haba ya gharama za juu za uzalishaji, bei duni kwa mazao na hatari ya sekta hizi kuporomoka. Kilio cha wakulima wapunguziwe viwango vya ushuru na kuwepo kwa sera za kuhakikisha wananufaika na bidii yao.

HAFLA NYINGI ZA RAIS
Chini ya utawala wa chama cha Kanu, Moi alikuwa akiongoza hafla nyingi karibu siku moja. Wapinzani walimlaumu kwa kuingilia kazi ambazo angeachia mawaziri au maafisa wa vyeo vya chini kama alivyofanya Kibaki chini ya utawala wake wa miaka 10. Kitengo cha habari cha Rais kilihakikisha hafla hizo zilipewa umuhimu na vyombo vya habari.
Viongozi wa Jubilee wamerejelea mtindo huo ambapo Rais Kenyatta amekuwa akiongoza hafla mbalimbali karibu kila siku, ambazo zinagharimu pesa nyingi za mlipa ushuru kutokana na maandalizi yake ya hadhi.

POLISI WENYE NGUVU KUPITA KIASI
Chini ya utawala wa Moi, maafisa wa polisi waliogopewa kama shetani kwani walihangaisha raia jinsi watakavyo. Utawala wa sheria ulikuwa kama ndoto kwa wengi na Wakenya hawakuwa na uhuru wa kuendelea na shughuli zao kwa njia huru. Polisi na maafisa wa ujasusi waliwaandama watu waliohisi walikuwa tisho kwa serikali.
Katika kurudisha hali ya enzi hizo, serikali ya Jubilee imechukua hatua zinazolenga kuhakikisha polisi na maafisa wa ujasusi wanaweza kusikiliza mawasiliano ya watu binafsi, kuwapa kibali cha kuzuiliwa washukiwa kwa muda mrefu bila kuwashtaki miongoni mwa masuala mengine.
UKABILA KUONGEZEKA SERIKALINI
Serikali ya Moi ililaumiwa pakubwa kwa kupalilia ukabila kwa kuwapa kazi watu kutoka baadhi ya jamii. Kutokana na hili, watu waliohitimu walikosa kazi kwa sababu ya makabila yao.
Japo kuna sheria ya kuhakikisha usawa katika nyadhifa za serikali, Jubilee imelaumiwa kwa kutenga baadhi ya jamii nchini katika uteuzi na uajiri wa maafisa wa serikali huku jamii mbili zikichukua idadi kubwa ya ajira za juu serikalini na katika taasisi za umma.

KUTEMBELEWA IKULU
Ilikuwa ni kawaida kwa Moi kutembelewa Ikulu na wajumbe na wafanyabiashara kutoka maeneo mbalimbali ya nchi. Hii ni mbinu iliyopingwa vikali na upinzani ukitilia shaka lengo la ziara hizo. Mtindo huu ulimalizika chini ya utawala wa Kibaki ambaye ilikuwa nadra kutembelewa na wajumbe Ikulu.
Chini ya Jubilee ziara za Ikulu zimerudi ambapo Rais Uhuru Kenyatta amekuwa akipokea wajumbe kutoka maeneo tofauti au vikundi vya watu Ikulu.
swahilihub@ke.nationmedia.com

No comments:

Post a Comment