Matukio : TIMUN Yaagizwa kutizama Mustakabali wa Dunia - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


23 May 2017

Matukio : TIMUN Yaagizwa kutizama Mustakabali wa Dunia


Vijana kutoka mataifa mbalimbali waliokusanyika katika Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN), mjini Arusha wametakiwa kuchambua masuala yaliyopo mbele yao kwa makini ili kutoa jawabu kwa matatizo ya dunia yanayohitaji ushiriki wao.

Kauli hiyo imetolewa na mwakilishi wa serikali katika mkutano huo Ngusekela Karen Nyerere, Ofisa anayeshughulikia dawati la Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Aliwataka vijana wanaoshiriki TIMUN kuhakikisha wanaangalia kwa makini mambo yanayogusa nchi zao na kuyatafutia ufumbuzi kwa kuwa ndio njia pekee ya kutekeleza malengo endelevu ya dunia ambayo yanahitaji ushirikiano wa ndani na wa kimataifa.

TIMUN ambayo kirefu chake ni Tanzania International Model United Nations hufanyika kila mwaka na ujumbe mbalimbali na mwaka huu ujumbe wa TIMUN ni: “kuwawezesha vijana katika diplomasia na uongozi”
Picha juu na chini ni Ofisa wa dawati la Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ngusekela Karen Nyerere akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN-2017) unaofanyika kwenye Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) mjini Arusha.

TIMUN huandaliwa na Shirikisho la vijana wa Umoja wa Mataifa (YUNA) taasisi ya vijana isiyotengeneza faida inayotangaza shughuli za Umoja wa Mataifa na kushirikisha vijana katika utekelezaji wa shughuli hizo.

Aidha aliwashukuru waandazi wa mkutano huo kubwa unaofanana na Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa (General Assembly) wenye lengo la kukutanisha vijana kujadili mustakabali wa malengo ya dunia.

Alisema vijana wana nafasi muhimu katika utekelezaji wa malengo hayo ya maendeleo endelevu jukumu ambalo dunia imejipa kwa miaka 15 hadi mwaka 2030.

Pamoja na kuwashukuru Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST) kwa kukubali kuwa mwenyeji wa kambi hiyo, hali iliyoonesha kwamba wanajali vijana, mwakilishi huyo wa serikali alisema kwamba Tanzania ipo tayari kusukuma mbele ajenda ya ushirikishaji vijana katika maendeleo endelevu kwa kuwa inaamini juu ya hilo.



“Wakati serikali inafanyakazi kwa karibu na taasisi nyingine kuhakikisha kwamba malengo ya maendeleo yanatekelezeka, baraza la vijana ambalo litakutana litakuwa na kazi kubwa ya kutengeneza sauti ya pamoja namna ya kukabiliana na changamoto zilizopo”

Alisema kwamba malengo ya dunia ambayo yapo 17 yanagusa kila sehemu ya maisha na hivyo ni vyema kama vijana watatoka na majibu ya maswali yanaoumiza vichwa kuhusu malengo hayo hasa mazingira na dunia endelevu.

Aliwataka vijana kutumia nafasi yao vyema katika jukwaa hilo kwani maisha ya watu bilioni 7 duniani wanategemea namna ambavyo wanajengwa na vijana, wenye mchango muhimu wa kulinda mazingira na kuhakikisha maendeleo endelevu.
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN-2017), unaofanyika katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) mjini Arusha

Awali Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez alisema kwamba zaidi ya vijana elfu 20 nchini Tanzania wamefunzwa malengo endelevu ya dunia, toka ulipofanyika uzinduzi Juni, 2016.

Akizungumza katika hafla ya kambi ya mwaka huu ya Tanzania International Model United Nations (TIMUN), inayofanyika katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST), Bw. Rodriguez alielezea kufurahishwa na idadi hiyo ya vijana waliohamasishwa na kusema kwamba malengo ya maendeleo endelevu 2030 yanahitaji kila mmoja kushiriki.

Aidha alielezea umuhimu wa ushiriki wa vijana katika masuala ya maendeleo kutokana na uwingi wao hapa nchini. Asilimia 67 ya watu nchini ni vijana.
Mkutano ukiendelea katika ukumbi wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) jijini Arusha.

Bw. Rodriguez alishukuru machampioni kwa kuwezesha vijana wenzao kutambua malengo endelevu ya dunia na kuwataka kuendelea kufanya vizuri zaidi katika kuwashawishi vijana wenzao kuelewa na kushiriki katika malengo hayo.

“Nataka kuwatafadhalisha kwamba huu ni mwanzo tu, kuna mengi ya kufanya. Kama Umoja wa Mataifa, tunawataka wote mshiriki, si tu katika kuelimisha kuhusu malengo haya ya dunia, lakini pia katika kuangalia mwenendo wa maendeleo hayo katika jamii na namna yanavyotekelezwa. Tukio kama hili la TIMUN linasaidia kuongeza uwezo wa kufikia malengo ya dunia,” alisema Bw. Rodriguez.

Vijana 50 wa kwanza machampioni walifunzwa mwaka jana katika TIMUN 2016. Kwa sasa kuna vijana machampioni 500 nchini Tanzania ambao wamepeleka ujumbe kwa vijana wenzao 20,000.
Mratibu wa Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN 2017), Tajiel Urioh akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo unaoendelea jijini Arusha.

Ujumbe ambao umekuwa ukisambazwa na machampioni kwa wenzao umeelezwa kulenga kuchochea hamasa ya kuelewa malengo kwa ajili ya maendeleo.

“Kama watu hawatajua malengo ya maendeleo endelevu, hawataweza kufanya malengo hayo kuwa ya kweli,” aliusema ujumbe huo Gloria Nassary, ambaye ni mmoja kati ya vijana 50 waliopewa mafunzo ya kwanza ya kuwa machampioni wa malengo ya dunia.

Naye Tajiel Urioh ambaye ni Mratibu wa Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN 2017), pamoja na kusisitiza amani kama sehemu muhimu ya kusukuma mbele utekelezaji wa malengo 17 ya maendeleo endelevu aliwahimiza vijana kutokata tamaa katika kuhimiza utekelezaji wa malengo hayo.
Ofisa wa Mawasiliano NUNV anayeshughulikia tovuti na mitandao ya kijamii katika ofisi ya Ofisi ya Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini, Edgar Kiliba akiendesha kipindi cha maswali na majibu wakati wa Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN 2017) unaoendelea jijini Arusha kwenye ukumbi wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) jijini Arusha.

Alisema bila amani kuanzia katika ngazi ya familia, uwezekano wa kutekeleza malengo hayo unakuwa mgumu kwa kuwa kuna uhusiano mkubwa kati ya amani na utekelezaji wake.

Alisema amani ni kionjo muhimu cha maendeleo kinapokosekana hata jukumu la vijana kulinda mazingira kwa ajili ya maendeleo endelevu halitawezekana.

Alisisitiza kulinda mazingira kwa ajili ya maendeleo na kufikiwa kwa malengo ya Umoja ya Mataifa ambayo ni malengo ya dunia katika kuimarisha ustawi wa jamii na kuinua uchumi .

Urioh katika mazungumzo yake alisema suala la uchafuzi wa mazingira ni suala gumu na mtambuka na kwamba mabadiliko ya tabia nchi yanayosababishwa na kuvurugwa kwa tabaka la ozoni halihusu Ulaya pekee, ambao wanachafua bali kila mmoja duniani; akiongeza kuwa mwishoni mwa siku wanaoathirika ni zaidi nchi zinazondelea akitolea mfano nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara.
Championi wa Malengo ya dunia (Global Goals) nchini, Rio Paul akitoa maoni katika Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN-2017) unaoendelea jijini Arusha.

Alisema suala la kukabilina na mabadiliko ya tabia nchi si kutulia bali kuwajibika kutekeleza wajibu ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba hakuna uharibifu wa mazingira unaofanyika katika taifa la Tanzania.

Alisema vijana wanaweza kufanya zaidi ya yale ambayo kwa sasa wameyafanya katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu kwa kuhakikisha kwamba wana elimu ya kutosha kuhusu malengo hayo na kushirikiana kuyatekeleza kwa kuangalia changamoto mbalimbali ambazo wanazipatia majibu.

Alisema lengo la malengo hayo ni kusaidia jamii vivyo hivyo vijana nao wanatakiwa kujitoa mhanga kuhakikisha kwamba jamii inaendelea kustawi na kuendelea kwa manufaa ya kizazi kijacho.
Mmoja wa washiriki kutoka nchini Uingereza akiuliza swali kwa Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa (hayupo pichani) wakati wa ufunguzi wa mkutano huo.

Aliwataka vijana kutafuta majawabu ya mambo yanayoikabili dunia kwa namna ya busara na kitaalamu zaidi huku wakizingatia diplomasia.

Septemba 2015, wanachama 193 wa Umoja wa Mataifa walikubaliana juu ya malengo mapya ya dunia, malengo ya maendeleo endelevu.

Malengo hayo yanatarajiwa kufanyiwa kazi katika kipindi cha miaka 15 ijayo na kuleta mabadiliko makubwa katika jamii, uchumi na mazingira kwa namna ya kuwa endelevu.
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akiteta jambo na Mwenyekiti wa Shirikisho la vijana wa Umoja wa Mataifa (YUNA) nchini, Jacqueline Kamwamu wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN-2017) unaoendelea mjini Arusha. Kushoto ni Mratibu wa Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN 2017), Tajiel Urioh

Wakati akiwa Arusha, Mratibu pia alifuatilia matokeo ya mafunzo yaliyofanyika Novemba mwaka jana katika chuo kikuu cha Tumaini Makumira yaliyofanywa kwa pamoja kati ya Umoja wa mataifa na Jumuiya ya Ulaya.

Katika mafunzo hayo machampioni 80 walifunzwa wakiwemo wanachuo 30 kutoka Taasisi ya Uhasibu ya Arusha (Institute of Accountancy Arusha -IAA).

Mkutano huo umefadhiliwa Umoja wa Mataifa (UN), Serikali, Covenant Bank, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST) pamoja PIU.
Katibu wa dawati la Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ngusekela Karen Nyerere akijibu baadhi ya maswali kutoka kwa washiriki (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa mkutano huo.
Pichani juu na chini ni sehemu ya washiriki kutoka ndani na nje ya nchi wanaohudhuria Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN-2017) unaoendelea mjini Arusha.










Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez (kulia) akisalimiana na Kaimu Makamu Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST) anayeshughulikia Fedha, Mipango na Utawala, Dr. Musa Chacha (kushoto) baada ya kuwasili ofisini kwa Makamu Mkuu wa Taasisi hiyo, Prof. Karoli Njau (katikati) jijini Arusha.
Makamu Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST) Prof. Karoli Njau akiwa kwenye mazungumzo ofisini kwake na Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez (wa pili kulia) aliyeambatana na Mkuu wa Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa nchini, Hoyce Temu (wa kwanza kulia), Ofisa wa dawati la Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ngusekela Karen Nyerere, Ofisa wa Mawasiliano na Ushirikiano NUNV kutoka Ofisi ya Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Didi Nafisa pamoja na Ofisa wa Mawasiliano NUNV anayeshughulikia tovuti na mitandao ya kijamii katika ofisi ya Ofisi ya Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini, Edgar Kiliba.

Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akikabidhi Makamu Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST) Prof. Karoli Njau kitabu chenye taarifa na ripoti mbalimbali za Umoja wa Mataifa baada ya kufungua Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN-2017) unaoendelea mjini humo.
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akiwa na mwenyeji wake Makamu Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST) Prof. Karoli Njau wakieleka kwenye eneo maalum la kupiga picha kwenye taasisi hiyo.
Meza kuu kwenye ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN-2017) katika picha ya pamoja.
Meza kuu katika picha ya pamoja na waandaaji wa TIMUN 2017.
Picha ya pamoja na washiriki wa TIMUN 2017 kutoka nje ya Tanzania.
Picha ya pamoja na washiriki wa kambi ya TIMUN 2017 inaoendelea jijini Arusha.

Mkuu wa Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa nchini, Hoyce Temu (wa pili kushoto) katika picha ya pamoja na washiriki wa TIMUN 2017 akiwemo Mshiriki wa taji la Miss Tanzania 2014, Sitti Mtemvu (katikati).

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad