Matukio /Betting : Mzazi Atakayemruhusu Mtoto Wake Kushiriki Kamari Kushtakiwa-Naibu Waziri - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


8 Feb 2017

Matukio /Betting : Mzazi Atakayemruhusu Mtoto Wake Kushiriki Kamari Kushtakiwa-Naibu Waziri



 

Na: Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma

Mtu yeyote atakaye ruhusu mtoto chini ya miaka 18 kushiriki, kuingia au kukaa karibu na eneo la mchezo wa kubahatisha (kamari) anahesabiwa kufanya kosa.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Ashatu Kijaji ameyasema hayo leo Bungeni, Mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge Viti Maalum Asha Abdullah Juma juu ya kuongezeka kwa maduka ya kucheza Kamari yanayojulikana kama Jack Pot katika miji mingi hapa nchini hivyo kusababisha uvunjifu wa maadili na nguvu kazi ya vijana.

“Michezo yote ya kubahatisha ikiwemo kamari (slots machines) inaendeshwa kwa mujibu wa sheria ya Bodi ya Michezo ya kubahatisha namba 4 ya mwaka 2003, sura 41 pamoja na Kanuni zake,” alifafanua Dkt. Kijaji.

Aliendelea kwa kusema kuwa, kwa mujibu wa sheria hiyo hakuna mtu au taasisi inayoruhusiwa kuendesha biashara ya michezo ya kubahatisha bila kuwa na leseni kutoka Bodi ya Michezo ya kubahatisha pamoja na vibali vingine vinavyotolewa na mamlaka nyingine za biashara.

Vile vile sheria hiyo inakataza watoto wenye umri chini ya miaka 18 kushiriki, kuingia, kukaa au kuzururazurura karibu na maeneo ya michezo ya kubahatisha.Aidha mtu yoyote ambaye atamruhusu mtoto chini ya miaka 18, kushiriki, kuingia au kukaa karibu na eneo la mchezo wa kubahatisha anahesabika kufanya kosa na anastahili kulipa faini ya shilingi 500,000 au kifungo kisichopungua miezi mitatu au vyote kwa pamoja.

Dkt. Kijaji amesema kuwa ikiwa kosa hilo litafanywa na mwendesha mchezo wa kubahatisha, Bodi inamamlaka ya kumfutia leseni.Hivyo basi, wajibu wa Serikali ni kuzuia watoto na vijana walio chini ya miaka 18 kucheza michezo ya kubahatisha.Pia, Dkt. Kijaji ametoa rai kwa wazazi na walezi kuwazuia vijana wao kucheza michezo ya kubahatisha pale wanapoona kuwa uchezaji wao unakuwa na matokeo hasi.

Hata hivyo amesema kuwa, michezo hiyo inaendeshwa kwa mujibu na sheria kama shughuli nyingine. Jambo la msingi ni kuhakikisha kuwa, wanaoendesha michezo hiyo wanazingatia sheria na kanuni zilizowekwa pamoja na wazazi, walezi na jamii kuhakikisha vijana wanazingatiia mila na desturi zinazolinda maadili ya Kitanzania wanapokuwa wanajishughulisha na shughuli halali za kiuchumi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad