Matukio : Serikali Imedhamiria kumaliza migogoro ya Ardhi, Simiyu - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


7 Jan 2017

Matukio : Serikali Imedhamiria kumaliza migogoro ya Ardhi, Simiyu



Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka (kushoto) akiwa na Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa wa Simiyu kupitia CCM, Mhe. Leah Komanya wakizungumza na wananchi wa Wilaya ya Meatu katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kituo cha Mabasi cha Mjini Mwanhuzi kwa lengo la kusikiliza na kutatua kero mbalimbali za wananchi wilayani humo.
 


Na Stella Kalinga, Simiyu
Serikali Mkoani Simiyu imedhamiria kwa mwaka 2017 kutatua na kuondoa migogoro yote ya ardhi ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara kwa wananchi wa mkoa huo.
Akitoa ufafanuzi wa namna ya kutatua kero hiyo wakati wa mkutano wake na wananchi wa jimbo la Meatu ,Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka alisema kuwa amechoshwa kusikia na kuona migogoro ya ardhi inayojitokeza ndani ya mkoa wake, hivyo mwaka 2017 ndio utakuwa mwisho wa kero hizo.
Mtaka amesema kuwa kamwe hawezi kukubali kuona migogoro hiyo inaendelea hivyo wananchi na watendaji wa idara ya ardhi wanapaswa kila mmoja ajue utaratibu sahihi wa utoaji na ununuaji wa ardhi ili kuepusha sintofahamu zinazojitokeza.
“ Mwaka huu wa 2017 ni mwaka ambao mimi mkuu wa Mkoa wa Simiyu nimeamua kusimamia, kusikiliza na kutatua kero zote za ardhi…nataka ndani ya kipindi hichi ifikie mahali migogoro ya ardhi kwa mkoa wa Simiyu inakuwa sio kipaumbele chetu…" alisema Mtaka.
Aidha, Mtaka alieleza kuwa anataka watendaji wa idara ya ardhi kuhakikisha wanafanya kazi zao kwa umakini na kuweka kumbukumbu za kimaandishi katika kila mgogoro unaotatuliwa kwani kuna baadhi ya wananchi wamekuwa wakiibua mgogoro hiyo upya pindi kunapotokea mabadiliko ya viongozi katika maeneo yao.
Sambamba na hilo pia amewataka wananchi wote wa mkoa wa Simiyu kutovamia maeneo ya Taasisi za Serikali na endapo wapo ambao wako ndani ya maeneo hayo waondoke mara moja kabla serikali haijawachukulia hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kubomolewa kwa nyumba zao.  


Hata hivyo katika kikao hicho kulibainika kuwepo na tatizo la watendaji wa ardhi kutoa umiliki wa kiwanja kimoja kwa zaidi watu wawili hali ambayo inasababisha mgongano mkubwa baina ya wananchi hao, ambapo wananchi wote walioonekana kupata tatizo hilo waliahidiwa kupewa viwanja mbadala na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu.


Michael Stephano mkazi wa Meatu amesema kuwa amefurahishwa sana na mfumo wa mkuu wa Mkoa kusikiliza kero za wananchi , kwani kwa kufanya hivyo wananchi watapata haki zao stahiki ambazo hapo awali walikuwa hawazipati.
 

“tunamshukuru sana mkuu wa Mkoa wetu…kitendo anachokifanya kwa kweli kimetupa nguvu ya kujua wapi tunapata haki zetu pale tunapoona tumeibiwa haki hiyo…sambamba na hilo ametusaidia mwongozo na kutatua kero za ardhi na ninaamini mpaka kuisha mwaka huu kero nyingi zitakuwa zimeisha…Alisema Stephano.  

Kwa upande wake Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Simiyu, Mhe.Leah Komanya amewataka Watumishi wa Idara ya ardhi kuzingatia sheria na taratibu kila wanapotwaa, kuuza, kuthamini au kupima ardhi kwa sababu kitendo cha kutofuata sheria na taratibu kwa watumishi hao kimekuwa chanzo cha migogoro mingi ya ardhi.

Wakati huo huo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka amemtaka Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Ndg.Fabian Manoza kuchunguza tuhuma zilizotolewa na wananchi dhidi ya viongozi wa Vijiji na Vitongoji juu ya kutumia maeneo ya misitu yaliyohifadhiwa yajulikanayo kama HASHI (Hifadhi Ardhi Shinyanga) kwa manufaa yao, na watakaobainika wachukuliwe hatua.
Mtaka amesema kwa kuwa wilaya hiyo inatarajia kuanzisha mradi wa ufuagaji bora wa ng’ombe wa kisasa, maeneo yote ya HASHI yatumike kupanda majani ya malisho kwa ajili ya kuwasaidia wafugaji kupata malisho hasa wakati wa kiangazi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad