Matukio : TANESCO yatoa Elimu kwa wananchi wa Kagera - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


18 Sept 2016

Matukio : TANESCO yatoa Elimu kwa wananchi wa Kagera


 Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Meja Jenerali (mstaafu), Salum Kijuu, (kushoto), akimkaribisha ofisini kwake, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania, (TANESCO), Mhandisi Felchesmi Mramba, alipomtembelea Septemba 17, 2016 ofisini kwake mkoani humo ili kumpa pole kufuatia athari za tetemeko la ardhi
 Mkuu wa Mkoa, Meja Jenerali (mstaafu), Salum Kijuu, akitoa taarifa za athari hizo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Felchesmi Mramba na ujumbe wake

NA K-VIS MEDIA/KHALFAN SAID, BUKOBA
SHIRIKA la Umeme Nchini Tanzania, TANESCO, limewahadharisha wananchi mkoani Kagera kutogusa  nyaya za umeme kwenye nyumba zilizoanguka au kupata athari kubwa kutokana na tetemeko la ardhi lililoukumba mkoa wa Kagera wakati wafanyakazi wa Shirika hilo wakiendelea na zoezi la kuondoa nyaya hizo.
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo, Mhandisi Felchesmi Mramba, (anayezungumza juu), wakati alipomtembelea Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Meja Jenerali (mstaafu), Salum Kijuu, Septemba 17, 2016 ili kumpa pole kutokana na maafa haayo.
Sambamba na wito huo, Mkurugenzi huyo pia alimuhakikishia Mkuu huyo wa Mkoa kuwa upatikanaji wa umeme mkoani humo utakuwepo bila shaka yoyote isipokuwa tu kwenye maeneo ambayo nyumba zimeathirika vibaya ili kuepusha athari zozote zinazoweza kutokea kutokana na kuguswa kwa nyaya hizo.
“Ninachoweza kusema Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, hakuna kifo kilichotokana na madhara ya umeme wakati wa tetemeko hilo, na vijana wetu walichukua hatua mara moja za kukata umeme tatizo hilo lilipotokea,” alisema Mhandisi Mramba.
Mkurugenzi huyo Mtendaji pia alisema, kutokana na ukubwa wa janga hilo, uongozi wa TANESCO ulichukua uamuzi wa kuwapeleka wafanyakazi wengine wa Shirika hilo kutoka mkoani Mwanza ili kuwaongezea nguvu wenzao wa Kagera katika jitihadav za kuhakikisha wananchi wanakuwa salama kutokana na kuharibika kwa miundombinu ya umeme kwenye majengo mbalimbali yaliyopata athari za tetemeko hilo.
Sambamba na wito huo, Mhandisi Mramba pia alimwambia Mkuu wa mkoa kuwa, Wafanyakazi wa TANESCO nchi nzima, wameanza zoezi la kuchanga fedha ili kuwasaidia wananchi wa Bukoba. “Sisi kwa upande wetu kama Shirika, tumekwisha kabidhi mchango wetu kupitia Msajili wa Hazina,” Aliongeza Mhandisi Mramba.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa Meja Jenerali (mstaafu), Salum Kijuu, alisema, tetemeko hilo lililokuwa na ukubwa wa kipimo cha richa 5.7, lilipelekea vifo vya watu 17, na kusababisha majeruhi zaidi ya 200, na kuacha nyumba zaidi ya 2,000 zikiharibika na nyingine kubomoka kabisa.
Alsiema mkoa unaendelea na kuratibu zoezi la kukuanya rasilimali fedha na vifaa ili kuwasaidia walioathirika.
Baada ya mkutano huo na Mkuu wa mkoa, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, alitembelea baadhi ya maeneo yaliyoathirika sana na tetemeko hilo huko Hamugembe, ili kukagua zoezi la utoaji elimu kwa wananchi kuhusu athari za nyaya zilizokaa vibaya kwenye makazi yao na kuwatia moyo wafanyakazi wa Shirika hilo ambao walikuwa wanaendelea na kazi hiyo.
Mhandisi Mramba, alipata fursa ya kuzungumza na Afisa Mtendaji wa Kata ya Hamugembe, Sudi Ahmada, na kumueleza kuwa, wakati wafanyakazi wa TANESCO wakiendelea na zoezi hilo, uongozi wa Kata nao ushirikiane na wafanyakazi wa Shirika hilo katika kuwaelimisha wananchi juu ya hatua zinazochukuliwa na TANESCO kwa sasa.
“Ningeomba muwaelimishe wananchi kuwa ni bora kutokuwa na umeme kwa kipindi hiki kifupi ambacho Shirika linachukua hatua za kuhakikisha usalama wao, na waonapo au kuwa na shaka yoyote juu ya nyaya au jambo linalowatia hofu kuhusu umeme, watoe taarifa haraka TANESCO na tutachukua hatua haraka,” alimuhakikishia Afisa huyo Mtendaji.
Naye Afisa huyo Mtendaji wa Kata ya Hamugembe, aliishikuru TANESCO kwa kuchukua hatua za haraka siku ya tukio hilo na kueleza furaha yake kwa jinsi anavyoona jitihada mbalimbali za wafanyakazi wa TANESCO katika kuhakikisha wananchi wanakuwa salama.

 Meneja wa TANESCO Mkoa wa Kagera, Mhandisi Francis Maze, akitoa elimu ya namna ya kuchukua hatua endapo patatokea athari zozote za umeme kwenye nyumba moja iiyoathirika na tetemeko huko Hamugembe
 Fundi akiwa kazini, Hamugembe


 Fundi wa TANESCO mkoani Kagera, akiondoa nyaya za umeme baada ya kukata umeme kwenye nyumba moja eneo la Hamugembe, ikiwa ni hatua ya kuchukua tahadhari
 Mhandisi Mramba, akitembelea maeneo yaliyoathirika na tetemeko hilo huko Hamugembe
 Bi Slivia Philip, akiwa ameketi nje ya nyumba yake iliyoharibiwa vibaya na tetemeko eneo la Hamugembe-Mkishenyi mkoani Kagera, Septemba 17, 2016
 Violet Anaclet, mkazi wa Hamugembe-Mkishenyi, akiwa na mawazo wakati akijipumzika kwenye eneo la wazi baada ya nyumba aliyokuwa akiishi kuharibiwa na tetemeko, Septemba 17, 2016
 Mhandisi Mramba, akisalimiana na Afisa Mtendaji wa Kata ya Hamugembe, Sudi Ahmada, Septemba 17, 2016
 Kaimu Meneja wa TANESCO Kanda ya Ziwa, Mhandisi Kalisa, (kulia), akizungumza na fomeni wa genge la TANESCO Kanda ya Ziwa, Freddy Lusama, wakati Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO Mhandisi Mramba alipowatembelea wafanyakazi wa Shirika hilo waliokuwa wakiendelea na kazi kwenye eneo la Hamugembe mkoani Kagera, Septemba 17, 2016
 Meneja wa TANESCO mkoani Kagera, Mhandisi Francis Maze, (katikati), akiwa amezungukwa na wafanyakazi wa shirika hilo akiwapa maelekezo, Septemba 17, 2016

 Mhandisi Mramba, alipofika eneo la Hamugembe, kuona jinsi wafanyakazi wa Shirika hilo wakiendelea na kazi
 Kwa bahati nzuri hakuna nguzo za umeme zilizoathirika na tetemeko hilo, hata hivyo TANESCO imeamua kuchukua tahadhari kwa kukagua ili kuona kama kuna nguzo yoyote iliyoathirika na kuchukua hatua za kubadilisha, kama ambavyo lori hili lililoonekana maeneo ya Hamugembe likiwa na nguzo hizo
 Mhandisi Mramba, akiongea na waanishi wa habari kwenye eneo moja lililoathirika vibaya na tetemeko la ardhi huko Hamugembe
 Kaimu Meneja Uhusiano wa Shirika la Umeme Tanzania, 9TANESCO), Leila Muhaji, akitoa ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali ya kiusalama ambayo wananchi wanapaswa kuzingatia pindi waonapo nyaya zilizoanguka au kutilia shaka yoyote kuhusiana na miundombinu ya Shirika
 Genizora Magili, anayehusika na masuala ya nyaya za umeme, akiwa amebeba vifaa vya kazi

Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Meja Jenerali (mstaafu), Salum Kijuu, akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Felchesmi Mramba na ujumbe wake, mara baada ya mazungumzo yao, Septemba 17, 2016
Meja Jenerali Kijuu, akiagana na Mhandisi Mramba na ujumbe wake

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad