Matukio /Afya : “Mwanamke wa Afrika bado anakabiliwa na changamoto” - Waziri Ummy Mwalimu - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


16 Mar 2016

Matukio /Afya : “Mwanamke wa Afrika bado anakabiliwa na changamoto” - Waziri Ummy Mwalimu


Ummy Mwalimu
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Ally Mwalimu ( Mb) ametoa hutuba kwa niaba ya Kundi la Nchi za Afrika wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 60 wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa kuhusu Hali ya Wanawake ( CSW). Mkutano huu wa wiki mbili unawakusanya wawakilishi kutoka serikali mbalimbali duniani na Asasi za Kiraia ambapo hujadiliana na kubalishana uzoefu na kuelimishana kuhusu hatua mbalimbali ambazo serikali zao zinachukua katika kuboresha maisha ya mwanamke na mtoto wa kike.
Wakati mamia ya wanawake kutoka serikalini na Asasi za Kiraia wakiwa wanakutana hapa Umoja wa Mataifa kwa mkutano wao unaojadili hali yao katika maeneo mbalimbali. Mamia mengine ya wanawake hususani wale wa Afrika wanaendelea kukumbana na changamoto lukuki zinazowarudisha nyuma kimaendeleo.
Ni wanawake hao wanaoishi katika nchi zenye migogoro, vita visivyokwisha, wenye kukabiliwa na uhaba na ukosefu mkubwa wa chakula, maji safi na salama, matatizo yatokanayo na mabadiliko ya tabia nchi, ndio ambao Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto, Mhe. Ummy Ally Mwalimu(Mb) ameitaka jumuiya ya kimataifa kuongeza kasi ya ushirikiano ili malengo mapya ya maendeleo endelevu (Agenda 2030) yaweze kuwafikia.
Waziri Mwalimu ametoa wito huo jana jumatatu, wakati alipotoa hutuba kwa niaba ya nchi za Afrika katika siku ya kwanza ya Mkutano wa 60 wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa kuhusu Hali ya wanawake (CSW) ambao umeanza hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.
08b03dc1-8077-433f-a8db-425449efcc49Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Ally Mwalimu akitoa hotuba katika Mkutano wa 60 wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa kuhusu Hali ya Wanawake ( CSW).
Changamoto hizo pamoja na nyinginezo nyingi zikiwamo kutopata fursa ya huduma za afya ya uzazi salama, elimu na usawa wa kijinsia zinamfanya mwanamke wa Afrika ashindwe kushindana na wanawake wenzie hususani wale walioko katika mataifa yaliyoendelea.
Waziri Mwalimu ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huu wa wiki mbili, alitoa hotuba hiyo kwa niaba ya nchi za Afrika kutokana na kwamba Tanzania kupitia Uwakilishi wake wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa ni Mwenyekiti wa Kundi la Nchi za Afrika kwa mwezi huu wa March.
Amewaeleza washiriki wa mkutano huo waliofurika katika Ukumbi Mkuu wa Mikutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, kwamba ingawa pamekuwapo na makubaliano na mapendekezo mengi kuanzia yale yaliyofikiwa huko Beijing, bado mwanamke anayeishi katika nchi zenye migogoro na vita barani Afrika ataendelea kuachwa nyuma na hivyo kukosa fursa ya kushinda na wenzie.
“ Ingawa vita, ukame wa kutisha, ukosefu wa chakula, ukosefu wa maji safi, ukichanganya na ukosefu wa fursa za kiuchumi, kijamii na kisiasa ni matatizo yanayowakabili watu maskini lakini mwanamke ndiye anayeathirika zaidi,” alieleza Waziri Mwalimu.
Na kuongeza kwamba Afrika inaendelea kutilia mkazo hoja ya kuwashirikisha wanawake katika majadiliano na utoaji wa maamuzi katika masuala yanayowagusa yakiwamo masuala yanayohusu mabadiliano ya tabia nchi na usuluhishi wa migogoro.
Alieleza kwamba, nchi zinazoendelea na zilizoendelea zinapashwa kuongeza kasi ya ushirikiano na ubia baina yao ili kufanikisha utekelezaji wa Agenda 2030), Makubaliano juu Mabadiliko ya Tabia nchi yaliyofikiwa huko Paris Ufaransa mwaka jana na makubaliano yaliyofikiwa na waafrika wenye kupitia Ajenda 2063 , ili katika umoja wake dunia basi iweze kumwondoa mwanamke na jamii nzima kutoka hapa ilipo na kufikia hali bora zaidi ya maisha.
Kama hiyo haitoshi Waziri alisema, Afrika inaamini pia katika uwezeshwaji wa Sekta binafsi, kupanua wigo wa ujasiliamali kama njia mojawapo ya kukuza uchumi endelevu , usawa wa kijamii, usawa wa jinsia, ulinzi wa mazingira na uwezeshaji wa mwanamke.
Mada kuu ya Mkutano wa 60 wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa kuhusu Hali ya Wanawake, ni “Uwezeshaji wa Wanawake na uhusiano wake na Ajenda 2030.
Awali akizungumza mwanzoni mwa mkutano huu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon amasema tangu alipoingia madarakani mwaka 2006 amejjitadi kuongeza nafasi za viongozi wanawake katika Idara za Sekretarieti ya Umoja wa Mataifa.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Ally Mwalimu akiwa katika Mkutano wa 60 wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa kuhusu Hali ya Wanawake ( CSW). Kushoto kwake ni Mwakilishi wa Tanzania wa Kudumu Katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manong.
Akitilia msisitizo hoja na haja ya kupanua wigo wa wanawake kushika nafasi katika ngazi za juu za maamumizi, Ban Ki Moon amesema, ingawa nchi nyingi zimejitahidi sana kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za juu za uongozi bado kuna Nchi Tano ambazo hazina wanawake katika Mabunge yao ili hali Nchi nyingine 7 hazina mawaziri wanawake katika serikali zao.
Naye Rais wa Baraza Kuu la 70 la Umoja wa Mataifa Bw Monges Lykketoft, akizungumza wakati wa mkutano huo, pamoja na kusisitiza umuhimu wa utekelezaji wa Agenda 2030 ambayo ameitaja kuwa ni jumuishi ameendelea kupigia chapuo la kutaka Katibu Mkuu ajaye wa Umoja wa Mataifa awe Mwanamke.
Na Mwandishi Maalum, New York

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad