Elimu : AfDB Yasisitiza weledi kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Nelson Mandela wanaofadhiliwa na Benki hiyo - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


6 Aug 2017

Elimu : AfDB Yasisitiza weledi kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Nelson Mandela wanaofadhiliwa na Benki hiyo





--

Benny Mwaipaja-WFM, Arusha


MKURUGENZI Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Kanda ya Afrika Mashariki, Dkt. Nyamajeje Weggoro, amewataka wanafunzi 45 kutoka Tanzania, Kenya, Uganda na Ethiopia, wanaosoma katika Chuo Kikuu cha Nelson Mandela cha Sayansi na Teknolojia kilichoko mkoani Arusha, kusoma kwa bidii na maarifa ili waweze kuzisaidia nchi zao kuinua sekta ya viwanda kwa njia ya utafiti na ubunifu wa teknolojia mbalimbali


Dkt. Weggoro ametoa rai hiyo alipotembelea Chuoni hapo ili kuangalia utekelezaji wa programu ya miaka mitano ya kuboresha masuala ya rasilimali watu inayofadhiliwa na Benki yake kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 8.2


Alisema kuwa Benki yake imeamua kuwekeza fedha nyingi katika eneo la Sekta ya elimu ya juu katika nyanja ya ufundi ili kuwapata vijana wa kutosha watakaoziba pengo lililopo na kuweka misingi mizuri ya maendeleo ya baadae hasa katika matumizi ya teknolojia na sayansi.


“Nimefurahi sana kuona wanafunzi wanasoma na wana ari kubwa na kwamba fedha tulizozitoa zinatumika vizuri, tunadhani hata baada ya mradi huu wa miaka 5 kukamilika, Benki itaweza kusaidia zaidi ufadhili wa fedha na vifaa” Alisema Dkt. Weggoro.


Kaimu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela, Prof. Joram Buza, ameishukuru Benki ya Maendeleo ya Afrika-AfDB kwa ufadhili huo, hatua iliyoongeza udahili wa wanafunzi katika chuo hicho.


“Mwaka wa masomo wa 2014/2015, Chuo kilidahili wanafunzi 7 pekee kutokana na changamoto wafadhili lakini baada ya ufadhili wa AfDB na Benki ya Dunia, wanafunzi wameongezeka hadi kufikia 135 jambo linalotia matumaini” alisema Pro. Buza.


Bi. Mwanaisha Mkangara na Bw. Alexander Mzura, wanaosomea shahada ya uzamivu katika masuala ya uhandisi na mifugo, kupitia ufadhili wa AfDB, wamesema kuwa masomo yao yatawaongezea ujuzi wa namna ya kufanya utafiti wa kihandisi na kuvumbua chanjo mbalimbali za mifugo.


AfDB inafadhili wanafunzi 45 ambapo 42 kati yao wanatoka Tanzania, huku Uganda, Kenya na Ethipia zikitoa mwanafunzi mmoja mmoja.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) Kanda ya Afrika Mashariki Dkt. Nyamajeje Weggoro akizungumza kuhusu umuhimu wa vijana wenye weledi wa kitaaluma katika kukuza uchumi, alipokutana na wanafunzi wa Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha (hawapo pichani) wanaofadhiliwa na Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB)


Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB), Kanda ya Afrika Mashariki, Dkt. Nyamajeje Weggoro (kulia) akiwa na Mkutano na Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha Prof. Joram Buza, alipotembelea chuo hicho kuangalia mradi wa kuwafadhili wanafunzi unaotekelezwa na Benki yake.



Baadhi ya wanafunzi wa Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha wanaofadhiliwa na Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) Kanda ya Afrika Mashariki Dkt. Nyamajeje Weggoro (hayupo pichani) alipotembelea Chuo hicho, ambapo aliwasisitiza kusoma kwa bidii ili kuhimili ushindani katika soko la ajira.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) Kanda ya Afrika Mashariki, Dkt. Nyamajeje Weggoro (kulia), na Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha Prof. Joram Buza wakizungumza jambo baada ya kumalizika kwa mkutano na wanafunzi wa chuo hicho wanaofadhiliwa na AfDB.

Afisa wa Idara ya Fedha za Nje anayeshughulikia Dawati la AfDB kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Said Nyenge (kulia) na Meneja wa Mradi wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) wa ufadhili wa wanafunzi katika Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela, Arusha, Bw. Julius Lenguyana (kushoto), wakibadilishana mawazo baada ya kumalizika kwa mkutano kati yao kuhusu ufadhili wa AfDB katika mradi wa miaka 5 kwa baadhi ya wanafunzi wa chuo hicho.

Meneja wa Mradi wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) katika Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha, Julius Lenguyana (kulia) akimuongoza Mkurugenzi Mtendaji wa AfDB Kanda ya Afrika Mashariki Dkt. Nyamajeje Weggoro (kushoto) alipowasili chuoni hapo kuangalia utekelezaji wa mradi wa ufadhili wa wanafunzi unaotekelezwa na Benki yake kwa miaka mitano katika Chuo hicho.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) Kanda ya Afrika Mashariki Dkt. Nyamajeje Weggoro (mbele wa pili kushoto), Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha Prof. Joram Buza (kulia kwake), Mshauri wa Mkurugenzi huyo Bw. Amos Kipronoh Cheptoo (kushoto kwake) na Afisa Mwandamizi wa Idara ya Fedha za Nje anayeshughulikia Dawati la AfDB kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Said Nyenge (kulia), wakiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wa Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha wanaofadhiliwa na Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) kwa ngazi ya shahada ya uzamili na uzamivu.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad