AFYA YETU :SERIKALI YAWATAKA WASIMAMIZI NA WADADISI WA UTAFITI WA TATHMINI YA HUDUMA ZA AFYA NCHINI KUZINGATIA WELEDI - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


25 Sept 2014

AFYA YETU :SERIKALI YAWATAKA WASIMAMIZI NA WADADISI WA UTAFITI WA TATHMINI YA HUDUMA ZA AFYA NCHINI KUZINGATIA WELEDI

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Seif Rashid akifungua mafunzo ya siku 27 kwa wakufunzi na wadadisi kutoka Tanzania Bara na Zanzibar watakaoendesha Utafiti wa Tathmini ya utoaji wa Huduma za Afya nchini 2014/15 mkoani Kilimanjaro.
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dkt. Albina Chuwa akizungumza na washiriki wa mafunzo ya Utafiti wa Tathmini ya utoaji wa Huduma za Afya nchini, mkoani Kilimanjaro.
Mkufunzi wa mafunzo ya wasimamizi na wadadisi wa Utafiti wa Tathmini ya Utoaji wa Huduma za Afya nchini Bi. Saumu Said akiendelea kutoa mafunzo kwa washiriki wa utafiti huo mkoani Kilimanjaro.
Washiriki wa mafunzo ya Wasimamizi na wadadisi wa Utafiti wa Tathmini ya Utoaji wa Huduma za Afya nchini wakiendelea na mafunzo yatakayowawezesha kufanya utafiti huo mkoani Kilimanjaro.
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Seif Rashid akisalimiana na wakufunzi na wadadisi kutoka Tanzania Bara na Zanzibar watakaoendesha Utafiti wa Tathmini ya utoaji wa Huduma za Afya nchini 2014/15 walio kwenye mafunzo ,mkoani Kilimanjaro.
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Seif Rashid akiwa katika picha ya pamoja na wakufunzi na wadadisi kutoka Tanzania Bara na Zanzibar watakaoendesha Utafiti wa Tathmini ya utoaji wa Huduma za Afya nchini 2014/15 mkoani Kilimanjaro.

SERIKALI imewataka wasimamizi na wadadisi wa Utafiti wa Tathmini ya Utoaji wa huduma za Afya nchini mwaka 2014/15 kuzingatia weledi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuepuka  kukusanya takwimu zisizo wakati wa utafiti huo utakaofanyika nchi nzima kuanzia Oktoba 13 mwaka huu. 

Aidha, imewaagiza Waganga Wakuu wa Mikoa, Wilaya, madakatari na wafanyakazi wa vituo vyote vya kutolea huduma za afya nchini  kutoa ushirikiano kwa wadadisi watakaoendesha utafiti huo ili waweze kufika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya vilivyopo katika maeneo yao kwa lengo la kupata taarifa sahihi  zitakazofanikisha utafiti huo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Seif Rashid akizungumza wakati akifungua mafunzo ya siku 27 kwa wakufunzi na wadadisi  kutoka  Tanzania Bara na Zanzibar  watakaoendesha  utafiti huo  amesema kuwa wakufunzi, wadadisi na wataalam  hao wanayo nafasi kubwa ya kufanikisha upatikanaji wa takwimu sahihi zitakazotoa taswira halisi ya utoaji wa huduma ya afya nchini kwa mwaka 2014/2015.

Amesema utafiti huo utaiwezesha serikali kutathmini utekelezaji wa mipango mbalimbali na kufikia malengo iliyojiwekea kitaifa na kimataifa kwa kuboresha na kuendelea  kutoa huduma bora za afya kwa wananchi wake.

Amesema Serikali imekuwa ikitekeleza programu mbalimbali za kuboresha huduma za afya na maisha ya Watanzania kwa kupitia Mikakati ya Kimataifa na Kitaifa ikiwemo ile ya Malengo ya Milenia ya Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011 -2016).

Amezitaja programu nyingine kuwa ni pamoja ile ya Dira ya Maendeleo ya Mwaka 2025, Matokeo Makubwa Sasa (BRN), Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania Bara (MKUKUTA) na Mkakati wa Kupunguza Umaskini Zanzibar (MKUZA) kwa upande wa Zanzibar. 

Dkt. Seif amesema katika juhudi hizo Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imekuwa na jukumu la kusimamia programu mbalimbali za afya na kufuatilia utekelezaji na utoaji wa huduma za afya nchini.

Ameeleza kuwa wakati wa utafiti wa kwanza wa Kutathmini Utoaji wa Huduma za Afya  nchini unafanyika na Ofisi ya Taifa ya Takwimu mwaka 2006,Tanzania ilikuwa na  jumla ya vituo vya kutolea huduma za afya 5669, kati ya hivyo 224  zilikuwa ni hospitali, 541 vikiwa  ni vituo vya afya na zahanati 4904. 

Amesema kumekuwa na maboresho makubwa katika sekta ya afya hadi kufikia mwaka 2013 ambapo takwimu zinaonyesha kuwepo kwa  vituo  6767 vya kutolea huduma ya afya nchini , hospitali 256, vituo vya afya 701 na zahanati 5810.

“Nyote ni mashahidi kuwa toka kipindi hicho mpaka sasa serikali imeendelea kusogeza huduma za afya karibu na wananchi wake,sasa tuna huduma ya kuzuia maambukizi ya UKIMWI kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto ambayo inapatikana  katika vituo vyote vinavyotoa huduma za mama mjamzito” Amesisitiza.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dkt. Albina Chuwa akizungumzia mafunzo hayo amesema kuwa washiriki watakaofaulu na kukidhi vigezo vilivyowekwa  watashiriki katika zoezi la kukusanya takwimu za utafiti huo  kwa kipindi cha miezi minne kuanzia  tarehe 13 Oktoba 2014 .

Amesema utekelezaji wa utafiti huo na mafunzo hayo unafanywa kwa pamoja na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii - Tanzania Bara, Wizara Afya - Zanzibar, Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, na Shirika la ICF International la Marekani ambao pia wanatoa ushauri wa kitaalamu katika kufanikisha utafiti huo.

Dkt. Chuwa amefafanua kuwa utafiti huo utahusisha ukusanyaji wa takwimu katika sehemu za kutolea huduma za afya kwa lengo la  kufahamu utayari wa vituo vinavyotoa huduma za afya na huduma bora za afya kwa wananchi.

Aidha amezitaja huduma zitakazoguswa na utafiti huo kuwa ni pamoja pamoja na Huduma za Afya ya Uzazi, Afya ya Watoto, Maradhi ya Kuambukiza kama vile Kifua Kikuu, UKIMWI, Malaria pamoja na Maradhi yasiyo ya kuambukiza kama vile magonjwa ya Kisukari na Moyo.

 Amefafanua kuwa lengo la kufanyika kwa utafiti huo ni kuiwezesha serikali kujua ni kwa namna gani vituo vinavyotoa huduma ya afya vimejipanga kutoa huduma bora ya afya kwa kuangalia upatikanaji wa huduma mbalimbali, vifaa, dawa, miundombinu na rasilimali watu kwa kada mbalimbali.

Kuhusu utafiti huo Dkt. Chuwa amesema ni wa pili kwa ngazi ya kitaifa ukifuatiwa na ule wa kwanza uliofanyika mwaka 2006  na kuongeza kuwa utahusisha sampuli wakilishi ya vituo vya kutolea huduma vya serikali ,binafsi, mashirika ya umma na vinavyomilikiwa na madhehebu ya dini ambavyo vimetayarishwa,  hospitali maalum zote, hospitali zote za mikoa , wilaya na baadhi ya vituo vya afya na zahanati. 

Naye mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Dkt. Ibrahimu Msengi akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo amesema kuwa mkoa huo unaendelea na juhudi za kuboresha huduma  za afya zinazotolewa katika vituo vya  afya pamoja  kwa lengo la kuboresha hali ya maisha ya wakazi wa Kilimanjaro na kukuza pato la mkoa huo.

Amesema mkoa umeweka kipaumbele katika kuboresha miundombinu ya afya iliyopo ili iweze kuakisi ukuaji wa Pato la Mkoa na mahitaji ya wananchi katika kupata huduma za afya zilizo bora kulingana na ongezeko la idadi ya Watu.

Amefafanua kuwa utafiti huo umekuja wakati muafaka ambapo mkoa huo na mikoa mingine nchini inahitaji kuboresha huduma za afya katika vituo vyote vya kutolea huduma.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad