Maisha : NSSF Imekuwa Mfano wa Kuigwa katika Nyanja za Kiuchumi na Kijamii - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


19 Oct 2017

Maisha : NSSF Imekuwa Mfano wa Kuigwa katika Nyanja za Kiuchumi na Kijamii






Waziri wa kazi, ajira, sera, bunge, vijana na wenye ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amelipongeza Shirika la NSSF kwa kuwa mfano wa kuigwa katika nyanja za kiuchumi na kijamii. Waziri mkuu aliyasema hayo katika mkutano wa wadau wa NSSF unaoendelea katika Kituo cha kimataifa cha mikutano AICC, Arusha


Waziri wa kazi pia alipongeza NSSF kwa kuandaa mkutano wa wadau unaofanyika hapa jijini Arusha, alisema mkutano huo siyo muhimu kwa NSSF na wadau tu bali pia kwa maendeleo na ustawi wa Taifa letu. Pia alifurahi kupata nafasi ya kufuatilia utendaji wa NSSF pamoja na kuona moja kwa moja kutoka kwa wadau wa NSSF.

Pia aliwapongeza wadau wa NSSF kwa kuitikia wito wake wa kuja kushiriki ili kupata taarifa za utekelezaji wa maazimio waliyokubaliana mwaka jana, taarifa za utendaji na kuchangia mawazo yatakayoleta tija ya kulijenga Shirika. Aidha, aliwapongeza Wageni mbalimbali katika mkutano huo ambao ni pamoja na Mhe. Anthony Mavunde, Katibu Mkuu Ndg. Eric Shitindi, Mkurugenzi Mkuu wa SSRA na Wakurugenzi wa Mifuko mingine ya Pensheni.


Vile vile Waziri wa kazi alitoa pongezi kubwa kwa namna ambavyo NSSF ilivyojitolea katika kutekeleza jukumu la kukuza Uchumi wa Viwanda kwani alisema Ujenzi wa Taifa si jukumu la Serikali Kuu peke yake bali ni la kila Mtanzania mmoja mmoja, taasisi na makampuni, na ndio maana NSSF pamoja na kuwa na jukumu la hifadhi ya jamii kwa mujibu ya sheria yake husika, imeona haja ya kupanua wigo wa uwekezaji wake na kuelekea katika viwanda jambo ambalo litaongeza ajira, kuongeza uzalishaji, na kukuza uchumi wa nchi kwa ujumla.

Waziri Mhagama alitoa mfano katika uwekezaji wa NSSF katika kukuza viwanda tumeshuhudia uwezekano wa kuzalisha ajira za moja kwa moja kwa Watanzania kutoka na uwekezaji ilioufanya katika viwanda mbali mbali. Nichukue fursa hii kuipongeza NSSF kwa kutoa mkopo wa shilingi bilioni 3.1 kwa lengo la kuongeza uzalishaji katika kiwanda cha madawa kilichopo Kibaha chini ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC). Katika kiwanda hiki ambapo ajira 100 zimezalishwa. Uzalishaji wa viuadudu ulianza Mwezi Desemba 2016 na mpaka sasa kiwanda kimezalisha jumla ya lita 327,400 ambazo ziliuzwa katika masoko ya ndani na nje.


Shirika lilitoa Mkopo kwa ajili ya upanuzi wa Kiwanda cha Chaki kilicho chini ya Usimamizi wa Halmashauri ya Maswa, Mkoani Simiyu mnamo mwezi June, 2017. Mkopo huu kwa ujumla utaongeza uzalishaji wa chaki kutokea vipande 432,000 vya chaki nyeupe (sawa na Katoni 180) kwa siku hadi vipande milioni 4.8 vya chaki nyeupe na za rangi (sawa na Katoni 2,000) kwa siku. Ongezeko la uzalishaji huu wa chaki utasaidia kuendeleza Sera ya Serikali ya “Elimu Bila Malipo” kwani itasaidia kupunguza mahitaji makubwa ya chaki katika shule za awali na msingi. Jumla ya Ajira 100 za moja kwa moja zinatarajiwa kutokana na uwekezaji huu.

Pia aliwapongeza NSSF kwa kushirikiana na PPF, na Jeshi la Magereza kupitia Kampuni ya Mkulazi, wamewekeza katika Mradi mkubwa wa shamba la miwa na Kiwanda cha Sukari kilichopo Mbigiri ambapo tayari hatua za upandaji miwa zimeanza nami nikiwa miongoni mwa watu waliopata fursa ya kupanda miwa ya


mwanzo kabisa. Kiwanda hiki Cha Mbigiri kitakapokamilika kinatarajiwa kuzalisha tani 50,000 za sukari kwa mwaka. Mpaka sasa mradi huu umezalisha ajira 300 za moja kwa moja na pia kupitia mpango wake wa wakulima wa nje katika eneo la Dakawa, imeweza kuandikisha jumla ya wakulima 1,500 wanaotegemewa kuanza kilimo cha miwa kuanzia mwezi Novemba, 2017 ambao watalima heka 15,297.


Hapo nyuma maeneo haya yatakayolima miwa na wakulima wa nje ama hayakuwa yakilimwa kitu chochote kama mashamba pori au yalikuwa yakilima mazao yasiyo na tija kama itakavyokuwa kwa zao la miwa. Hii ni hatua kubwa na ya kupongezwa sana Pia NSSF na PPF kupitia Mkulazi, watajenga Kiwanda cha Sukari kitakachokuwa na uwezo wa kuzalisha tani 200,000 kwa mwaka, kiwanda hicho kitajengwa katika eneo la Mkulazi lililopo Ngerengere, Mkoani Morogoro, ambapo kinamtazamo wa kutoa ajira zaidi 100,000 kwa watanzania.

Alisema Mbali na kuzalisha ajira hizo, NSSF kupitia miradi inayoifadhili ya kufufua viwanda vya iliyokuwa National Milling Corporation (NMC) ambavyo kwa sasa vipo chini ya Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB) inategemewa kuwa itakapokamilika itazalisha jumla ya ajira 30,000. Kiwanda kilichopo Kizota, Dodoma kina uwezo wa kuzalisha tani 60 za unga na tani 20 za mafuta ya alizeti. Kiwanda hiki kitatoa ajira 6000 za moja kwa moja, na kiwanda cha NMC Mwanza chenye uwezo wa kuzalisha tani 250 za unga na tani 60 za mchele kinatarajiwa kutoa ajira za moja kwa moja 24,000.


Na alihitimisha kwa kusema Kwa uwekezaji huu, maana yake ni kwamba mifuko hii itaondoa tatizo la ajira katika nchi, itasaidia kuweka ushindani katika soko na hivyo kushusha makali ya bei katika bidhaa zitakazokuwa zikizalishwa na pia itasaidia serikali kukusanya kodi na hivyo kuisaidia kuwekeza katika miradi mingine ya kimaendeleo na kijamii. Mbali na haya, Mifuko hii itapata wanachama wapya na kukusanya michango zaidi na kuwekeza zaidi ili kuweza kutimiza malengo yake ya msingi ya Hifadhi ya Jamii. Hivyo, hatuna budi kwa pamoja kutoa pongezi za dhati kwa ubunifu mkubwa unaonyeshwa na mifuko hii

Nae Mkurugenzi mkuu wa NSSF Prof Godius Kahyarara alisema Kwa muda mfupi, Mfuko wa NSSF umeonyesha ufanisi mkubwa na mafanikio ya kuridhisha kwa kutunisha mapato yake kwa kuongeza ukusanyaji wa michango, kupunguza matumizi ya uendeshaji wa shughuli zake na pia kuongeza wigo wa uwekezaji kwa kipindi kifupi cha uwekezaji kutoka Shilingo Bilioni 12 mwezi Aprili mwaka 2016 hadi Shilingi Bilioni 418.82 mwezi Juni mwaka huu, 2017. Mfuko pia umeweza kupunguza malipo hewa ya kujitoa kwa asilimia 127 na hivyo kuokoa kiasi cha Shilingi Bilioni 160 kwa kipindi cha mwaka mmoja. Taarifa za uwezo wa fedha zinaonyesha kuwa tumeweza kuwekeza takribani Shilingi bilioni 50 za Tanzania kupitia hisa za Vodacom zilizowekwa sokoni mwaka huu. Zaidi ya hapo, tumeweza pia kulipa malimbikizo yote ya kodi kwa zaidi ya Shilingi bilioni 94 za Tanzania na pia kumaliza malipo yote ya mikatabayenye thamani ya Shilingi 169.5 bilioni za Tanzania.


Mkutano huu wa Wadau wa Mfuko wa NSSF unafanyika katika kipindi ambacho Serikali ya Awamu ya Tano imeweka mikakati na malengo muhimu ya mabadiliko ya kukuza uchumi wa viwanda. NSSF imawahakikishia ushiriki wake katika kutekeleza Sera ya Serikali ya kukuza na kujenga uchumi wa viwanda. Mfuko wa NSSF umejikita katika kukuza uchumi kupitia Sekta ya Viwanda kabla ya miaka ya 1990 wakati ambao Tanzania ilijikita katika mapinduzi ya uchumi wa viwanda. Mifano michache ni ushiriki wa Mfuko wa NSSF katika uwekezaji wa ubia na viwanda vya Aluminum Africa, Kwanza Bottles, Phantom Limited, Mbeya Cement, Meditech, General Tyre, Katani Limited, Kagera Sugar, Tanzania Pharmaceuticals Limited, 21st Century na Dar Cement Company.


Kupitia uzoefu mpana tuliopata katika ushiriki wa maendeleo ya viwanda, Mfuko wa NSSF upo tayari kuongeza juhudi za kusaidia malengo ya Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli ya kujenga “Tanzania ya Viwanda”.Alisema, Wakati huu tunapotekeleza azma yetu ya kusaidia juhudi za Serikali kujenga uchumi wa viwanda, Mfuko wa NSSF unaendelea kutekeleza mikakati yake ya shirika kuwa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Unoongoza miongoni mwa Mifuko yote Barani Afrika ifikapo mwaka 2020. Ili kufikia lengo hilo, Mfuko unahitaji wanachama 1,823,927 na makusanyo ya michango kiasi cha Shilingi Trilioni 1.76 za Tanzania kila mwaka.


Alisema Mfuko wa NSSF umetumia kiasi cha Shilingi za Tanzania17,384,771,999 kwa kutoa huduma za Bima ya Mafao ya Afya. Mafao kwa Bima ya Afya ni muhimu ambao wanachama 443,293 walipewa huduma hizo. Mfuko pia umewafikia wanachama 121,460 kutoka Sekta isiyo Rasmi kwa kuandikisha wanachama kutoka makundi ya wajasiriamali wadogo wakiwemo Wachimbaji wadogo wadogo wa Madini, Wavuvi, Waendesha Pikipiki (Boda Boda), Wachuuzi wadogo wadogo wa bidhaa (Machinga), Mama Lishe pamoja na Wanafunzi wa Vyuo Vikuu nchini


Vile vile Prof Kahyarara alisema Kuhusu ushiriki wa Mfuko wa NSSF katika kusaidia na kuwajibika kwa Jamii ya Wanzania, Mfuko wa NSSF umesaidia makundi kadhaa ya wanachi kwa kutoa na kuboresha huduma za Afya kwa kujenga Vituo vya Afya, Zahanati, kusaidia utoaji wa huduma za afya na pia kampeni ya kupambana na magonjwa yasiyoambukiza. Michango mingine ya Mfuko pia imelenga kusaidia kampeni za kupambana na Maambukizi ya Virusi vinavyoeneza Ukimwi kupitia TACAIDS katika Mpango wa Miaka Mitano wa kupambana na kuenea kwa Virusi vya VVU.


Mfuko wa NSSF pia umesaidia ununuzi wa Madawati katika Shule kadhaa za Tanzania ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Mh. Rais John Magufuli ya kupanua elimu nchini Tanzania. Mfuko pia umesaidia kukarabati madarasa na maabara kadhaa ya shule nchini. Mfuko wa NSSF pia umesaidia maeneo ya usalama kwa njia ya michango kwa kujenga Kituo cha Polisi cha Kiluvya pamoja na Nyumba za Askari Polisi, pia Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani. Pamoja na misaada mingine, Mfuko wa NSSF umesaidia kuchangia katika maafa yaliyoikumba Tanzania ikiwemo Majanga ya Asili na Moto. Mfuko umechangia kujenga upya miundombinu iliyoharibiwa na mafuriko huko Lindi, Nasibugani, Mtwara na Shule ya Sekondari ya Moreto.


Shule kadhaa zilizoharibiwa pamoja na mabweni na madarasa yake kubomolewa kutokana na Tetemeko la Ardhi Mkoani Kagera pamoja na wahanga wa Tetemeko hilo walipatiwa misaada mbalimbali. Mfuko wa NSSF pia umetoa msaada kwa wakazi wa Kagera kununua mbegu za viazi vitamu vinavyoota na kukomaa haraka wakati wa uhaba wa mvua kutokana na mashamba mengi ya nafaka kuharibiwa na Tetemeko hilo mwaka jana.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad