Afya Zetu : Ololosokwan yazindua utabibu kwa njia ya Tehama , Arusha - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


31 Oct 2016

Afya Zetu : Ololosokwan yazindua utabibu kwa njia ya Tehama , Arusha

Mradi mkubwa wa kijiji cha digitali cha Ololosokwan, Loliondo umezinduliwa rasmi mwishoni mwa wiki, miaka miwili tangu kutiwa saini kwa uanzishwaji wake kati ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (Unesco) na kampuni ya Samsung.

Hiki kitakuwa ni kijiji cha nne cha digitali barani Afrika cha kwanza kikiwa nchini Afrika Kusini huku kingine kikiwa Gabon na Ethiopia.

Kijiji hicho cha digitali ni nadharia ya Samsung katika kurejesha faida kwa umma na kina huduma mbalimbali ambazo zikiunganishwa na haja ya wananchi zitasaidia kubadili maisha ya wamasai na kuondokana na utegemezi wa mifugo pekee.

Uzinduzi rasmi wa kijiji hicho umefanywa na Mkuu wa mkoa Arusha Mrisho Gambo kwa niaba yaWaziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na watoto Ummy Mwalimu.

Kijiji hicho cha digitali kina shule yenye tehama ikiwa na maunganisho ya intaneti, kiliniki ya kisasa ikiwa na kituo cha teknolojia ya mawasiliano yenye kuwezesha utabibu (telemedicine) na jenereta linalotumia nguvu za jua.

Mradi huo ambao ulishuhudiwa utiaji saini na Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Bi. Leah Kihimbi kutoka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo na Dkt. N. Iriya kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) Dar es Salaam na wafanyakazi wa UNESCO mwaka 2014, kukamilika kwake kunawezesha UNESCO na serikali ya Tanzania kuwapatia wakazi wa eneo hilo huduma bora za afya na vijana wa Kimasai nafasi ya kupata elimu kutokana na ukweli kuwa kwa utamaduni na kazi zao za ufugaji wamekuwa wakipata shida ya kupata elimu.

Utiaji saini wake katika mwaka huo ulifanywa na Mkuu wa ofisi na Mwakilishi Shirika la UNESCO nchini Bi. Zulmira Rodrigues na Mkurugenzi wa Samsung Electronics nchini Tanzania, Bw. Mike Seo .

Kupitia kijiji hicho vijana wataendelea na masomo hata kama wanachunga mifugo yao kutokana na kupatiwa tablet ambazo zitawawezesha kujifunza hata wakiwa nje wakichunga mifugo yao.

Aidha miongoni mwa manufaa makubwa yatakayopatikana katika mradi huo wa kijiji cha digitali ni kuweza kupata nishati rahisi na iliyo rafiki kwa mazingira kwa kuwepo na jenereta linalotumia nishati ya jua.

Kuwepo kwa kijiji hicho kunataka kudhihirisha ni kwa namna gani teknolojia inaweza kutumika kuleta mabadiliko chanya yanayotakiwa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi waliopo vijijini.

Kijiji hicho cha Loliondo ambacho kitakuwa cha nne katika vijiji vya kidigitali barani Afrika kimeelezwa naMkuu wa mkoa wa Arusha Mheshimiwa Mrisho Gambo kama utekelezaji wa Sera ya Tiba Mtandao kutokana na kuzinduliwa kwa Kliniki Mtandao iliyopo katika Kijiji hicho.

Katika uzinduzi wa mradi huo kwa ujumla wake, kliniki ndicho kitu ambacho kinaonekana kwenda karibu zaidi na wananchi wa Ololosokwan kwani itakuwa inatoa huduma za afya, bora za kisiasa na za haraka kwa wakazi wa kata za Soitsambu naa Oloipiri, Wilayani Ngorongoro.

Katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa mkoa wa Arusha ,Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na watoto Mhe Ummi Mwalimu wakati wa uzinduzi wa kliniki hiyo,alisema kuwa Tiba Mtandao imekua ni miongoni mwa Vipaumbele vya Wizara yake ili wananchi wote Tanzania waweze kupata huduma stahiki za matibabu pasipo kujali changamoto za Kijiografia zinazotukabili,

Pamoja na kufanya uzinduzi huo katika hotuba yake Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo aliwashukuru wote walioshiriki kuleta Mradi huo wa maana kwa mkoa wa Arusha kwani wangeweza kupeleka sehemu nyingine yeyote na kuongeza kuwa ni deni kubwa sana lazima tuhakikishe huduma hiyo imefanikiwa.

Akizungumzia masuala ya afya kama kipaumbele katika mradi huo wenye lengo la kuhifadhi utamaduni wa kimasai huku wakitumia teknolojia ya kisasa kuleta maendeleo katika elimu na kuhifadhi mazingira, Mkuu huyo wa mkoa akizungumza kwa niaba ya Waziri alisema kuwa kutokana na umuhimu wa sekta ya afya kwa kila Mtanzania ,serikali itaelekeza nguvu katika Kliniki hiyo ili kuiwezesha kutoa huduma stahiki na Kwa muda mrefu kwa wananchi wa maeneo haya.

"Kliniki hii ni ya kwanza Tanzania na itaweza kutoa huduma bora na za kisasa kwa njia ya mtandao kwa wananchi zaidi ya elfu kumi kutoka katika maeneo ambayo hapo awali wananchi walikuwa wanatembea umbali mrefu zaidi ya Kilomita 50 kufuata huduma za afya".

" Hii inadhihirisha kwamba mwananchi wa Ololosokwan na maeneo ya jirani anaweza kuhudumiwa na daktari bingwa aliyeko Muhimbili au kokote Duniani kupitia Klinik hii;na mfumo wa Mtandao uliopo unaruhusu upatikanaji wa huduma hizi kwa kipindi chote cha mwaka mzima".

Aidha aliitaka Halmashauri kutenga Bajeti kwa ajili ya kuongeza hadhi ya zahanati hiyo kuwa Kituo cha Afya ambapo itaenda sambamba na kuongeza majengo Pamoja na wataalam watakaoweza kutoa huduma stahiki Kwa wananchi.

Upatikanaji wa kituo cha Afya katika eneo hilo huku kukiwepo na kliniki mtandao kutasaidia kuokoa maisha ya wananchi ambao wengi wao waliamini kupona magonjwa makubwa ni mpaka uende KCMC au Muhimbili tu.

Awali akizungumza katika uzinduzi huo Mkuu Shirika la Umoja wa mataifa linaloshigulikia Elimu na Sayansi (UNESCO) nchini Tanzania Bi. Zulmira Rodrigues alisema kijiji hicho ni ushuhuda tosha wa ukuaji wa teknolojia unaenda sambamba na maono ya shirika la Unesco la kutoa kipaumbele katika miradi ya sayansi inayosaidia wananchi wenye mahitaji moja kwa moja.

Alisema kwa kutambua adha waliyokuwa wanaipata wananchi wa Ololosokwan walitengeneza mradi ambao sehemu mojawapo ni kliniki Mtandao ili kuleta mabadiliko ya afya za watu kwa njia ya kisayansi.

Naye mkurugenzi wa Tiba Kutoka Wizara ya Afya Dr. Margareth Evelyne Mhando alishukuru Unesco kusaidia kutekeleza malengo ya Wizara kupitia Mradi huu wa kijiji cha digitali na kuongeza kuwa ni hatua nzuri katika sekta ya afya Kwa sababu hivi sasa wananchi waliombali na vituo vya Afya kupitia Mradi huu watapata huduma bora kutoka Kwa matabibu wabobezi.

Uzinduzi wa Mradi huu ulihudhuriwa pia na Balozi wa Switzerland Nchini Tanzania Bi. Florence Mattli, Wawakilishi wa Samsung ambao ndio waliotoa fedha na Teknolojia pamoja na wawakilishi kutoka Umoja wa Ulaya (EU).

Bi. Mattli alisema kwamba wataendelea kusaka wadau wengine kuhakikisha kwamba mradi huo unaendelea kutanuka na kufanikiwa kwa kujazia maeneo ambapo panahitaji nguvu nyingine.
Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Rashid Taka akizungumza machache kabla ya kumkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo (kushoto aliyeketi) kuhutubia wageni waalikwa na wanakijiji wa Ololosokwan wilayani Ngorongoro kwenye hafla fupi ya uzinduzi wa kijiji cha kidigitali chenye kituo cha huduma maalum za afya pamoja na kituo cha elimu kwa njia ya mtandao uliofanyika mwishoni mwa wiki mkoani Arusha.
Pichani juu na chini ni Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo akisoma hotuba katika hafla ya uzinduzi wa kijiji cha kidigitali chenye kituo cha huduma maalum za afya pamoja na kituo cha elimu kwa njia ya mtandao kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu uliofanyika kwenye kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Pichani juu na chini ni baadhi ya wanakijiji wa Ololosokwan na wageni waalikwa wakimsikiliza mgeni rasmi RC Gambo kwenye hafla ya uzinduzi wa kijiji cha kidigitali chenye kituo cha huduma maalum za afya pamoja na kituo cha elimu kwa njia ya mtandao uliofanyika mwishoni mwa wiki, wilayani Simanjro, mkoani Arusha.

Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues akizungumzia ukuaji wa teknolojia ambayo inaenda sambamba na maono ya shirika lake kwenye hafla uzinduzi wa kijiji cha kidigitali chenye kituo cha huduma maalum za afya pamoja na kituo cha elimu kwa njia ya mtandao uliofanyika mwishoni mwa wiki, wilayani Simanjro, mkoani Arusha.

Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori akizungumza kwenye hafla uzinduzi wa kijiji cha kidigitali cha Samsung (Samsung Digital Village) kinachotumia umeme wa jua chenye kituo cha huduma maalum za afya pamoja na kituo cha elimu kwa njia ya mtandao uliofanyika mwishoni mwa wiki, wilayani Simanjro, mkoani Arusha.
Balozi wa Uswisi nchini, Mh. Florence Tinguely Mattli akizungumza kwenye uzinduzi wa kijiji cha kidigitali cha Samsung (Samsung Digital Village) kinachotumia umeme wa jua ambacho kina kituo cha huduma maalum za afya pamoja na kituo cha elimu kwa njia ya mtandao kilichopo katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Simanjro mkoani Arusha.

Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Dr. Margaret Mhando akitoa neno ambapo aliwashukuru Unesco kusaidia kutekeleza malengo ya wizara kupitia mradi huu wa kijiji cha kidigitali cha (Samsung Digital Village) unaoratibiwa na Shirika la UNESCO kwenye kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro, mkoani Arusha.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo akimsikiliza kwa makini Balozi wa Uswisi nchini, Mh. Florence Tinguely Mattli wakati wa hafla ya uzinduzi wa kijiji cha kidigital cha Samsung chenye kituo cha huduma maalum za afya pamoja na kituo cha elimu kwa njia ya mtandao (Samsung Digital Village) uliofanyika kwenye kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo akijipanga kuzindua rasmi moja ya kituo cha huduma maalum za afya huku Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori (katikati) Balozi wa Uswisi nchini, Mh. Florence Tinguely Mattli (kushoto), Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Dr. Margaret Mhando (kulia), Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues (wa pili kushoto) wakishuhudia tukio hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo akikata utepe kuzindua rasmi moja ya kituo cha huduma maalum za afya huku Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori (katikati) Balozi wa Uswisi nchini, Mh. Florence Tinguely Mattli (wa pili kushoto), aibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nuru Milao (kushoto), Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Dr. Margaret Mhando (kulia), Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues (wa pili kushoto) wakishuhudia tukio hilo.
Mganga Mkuu wa Wilaya Ngorongoro, Dk. Omari Sukari akitoa maelezo ya huduma mbalimbali za Afya zitakazokuwa zikipatikana ndani ya moja ya makontena ya kijiji cha Kidigitali cha Samsung (Samsung Digital Village) kwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mh. Mrisho Gambo (kulia) wakati wa uzinduzi wa kituo cha huduma maalum za afya uliofanyika katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mh. Mrisho Gambo akifanya kipimo cha B.M.I ndani ya kituo cha huduma maalum za afya kilichopo katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha mara baada ya kukizundua rasmi.
Mganga Mkuu wa Wilaya Ngorongoro, Dk. Omari Sukari akimsoea majibu ya BMI Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo ndani ya kituo cha huduma maalum za afya kilichopo katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha ambacho kimezinduliwa rasmi mwishoni mwa juma.
Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues (kushoto) akifurahi jambo wakati Mganga Mkuu wa Wilaya Ngorongoro, Dk. Omari Sukari (katikati) akimsoma majibu ya BMI Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo (kulia) akiwa ndani ya Kliniki hiyo ya Kidigitali ya Samsung akifanya uchunguzi wa kupima uwezo wake wa kusikia kwa kutumia kifaa maalum.
Mratibu wa Telemedicine kutoka Wizara wa Afya ,Maendeleo ya jamii, Jinsia,Wazee na Watoto, Dk. Liggy Vumilia akifafanua kwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo (hayupo pichani) jinsi kituo cha huduma maalum za afya cha kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha kinavyoweza kufanya mawasiliano na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa njia ya mtandao na kupata ufumbuzi wa tatizo la mgonjwa katika hafla fupi ya uzinduzi wa kituo hicho. Kulia ni Stella Kairuki kutoka Samsung.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo akitoa mkono wa pongezi kwa Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori kwa kusogeza huduma muhimu za afya kwa wanakijiji wa Ololosokwan mara baada ya kuzindua kituo hicho cha afya wilayani Ngorongoro mwishoni mwa juma.

Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo akimpongeza Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues kwa kuratibu mradi huo utakaowasaidia wanakijiji wa Ololosokwan katika huduma za afya na elimu kwa njia ya mtandao.

Kutoka kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nuru Milao, Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori pamoja na Afisa Utawala na Fedha wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Spencer Bokosha wakifuatilia yaliyokuwa yakijiri kwenye hafla ya uzinduzi wa kituo cha huduma maalum za afya uliofanyika katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Televisheni ya Samsung iliyopo nje ya kituo hicho cha huduma za afya ikionyesha kipindi maalum cha kuelimisha jamii ya wafugaji (Wamasai) wa kijiji cha Ololosokwan iliyotafsiriwa Kimasai kuhusiana na masuala ya afya na usafi wakati wakisubiri kupata huduma za afya.

Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues akifafanua jambo kwa wageni waalikwa nje ya kituo cha huduma ya meno na maabara ya kijiji cha kidigitali wakati wa uzinduzi wa kituo cha huduma maalum za afya pamoja na kituo cha elimu kwa njia ya mtandao (Samsung Digital Village) uliofanyika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues akibadilishana mawazo na Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori kwenye hafla ya uzinduzi wa kituo cha huduma maalum za afya uliofanyika katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Arusha kwenye picha ya pamoja na wadau waliofanikisha mradi wa Samsung Digital Village pamoja na baadhi ya wanakijiji wa Ololosokwan watakaonufaika na mradi huo.

Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues (wa pili kushoto) Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori (kushoto) Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Unesco (NATCOM), Dkt Moshi Kimizi (wa pili kulia) pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nuru Milao (kulia) wakiwasili kwenye eneo la kituo cha elimu kwa njia ya mtandao kwa ajili ya uzinduzi rasmi katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Balozi wa Uswisi nchini, Mh. Florence Tinguely Mattli (wa pili kushoto) akiwa ameambatana na Wawakilishi kutoka Umoja wa Ulaya (EU), Olivier Couplex (wa pili kulia) pamoja na Anna Costantine wakiwasili ene la tukio.

Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues na Balozi wa Uswisi nchini, Mh. Florence Tinguely Mattli wakifurahia jambo kwenye hafla ya uzinduzi huo.

Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo akikaribishwa kwa ngoma za kimasai katika eneo la tukio.

Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori akizungumza machache jengo la kituo cha elimu kwa njia ya mtandao ambalo limetengenezwa na Samsung kabla halijazinduliwa rasmi kwenye kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues akitoa neno wakati wa jengo la kituo cha elimu kwa njia ya mtandao kabla kuzinduliwa rasmi kwenye kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha. Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo (wa pili kulia) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa kituo cha elimu kwa njia ya mtandao kinachotumia umeme wa jua (Solar Power Internet School) uliofanyika katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha. Wanaoshuhudia tukio hilo ni Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Samsung Afrika Mashariki, Patricia Kingori (wa tatu kushoto) Balozi wa Uswisi nchini, Mh. Florence Tinguely Mattli (wa kwanza kushoto), Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nuru Milao (wapili kushoto), Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues (kulia).

Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Emanyata ya Loliondo, Kenneth Pascal wa kidato cha pili akitoa elimu kwa njia ya mtandao kupita programu ya Shule Direct kwa wanafunzi wenzake wa darasa la kompyuta waliojumuika na mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo wakati wa sherehe ya uzinduzi wa kituo hicho uliofanyika katika kijiji cha Ololosokwan, Wilayani Ngorongoro, mkoani Arusha.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo (katikati), Balozi wa Uswisi nchini, Mh. Florence Tinguely Mattli (kushoto) pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nuru Milao wakiwa ndani ya kituo cha elimu kwa njia ya mtandao kinachotumia umeme wa jua (Solar Power Internet School) mara baada ya kukizindua katika kijiji cha Ololosokwan, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Darasa la kompyuta kwa njia mtandao likiendelea huku wageni wakishuhudia.

Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues akifuatilia kwa makini darasa lililokuwa likiendeshwa na mwanafunzi wa kidato cha pili (hayupo pichani).

Mafunzo kwa vitendo yakiendelea.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad