Matukio /Zanzibar : Mhe. Mahmoud Kombo atembelea vituo vya Afya Mkoa wa Kaskazini - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


14 Jun 2016

Matukio /Zanzibar : Mhe. Mahmoud Kombo atembelea vituo vya Afya Mkoa wa Kaskazini

Waziri wa Afya Zanzibar Mahmoud Thabit Kombo akisalimiana na viongozi wa Chama na Serikali alipowasili Chaani Masingini kukagua kituo cha Afya cha kijiji hicho kufuatia mwaliko wa Mwakilishi wa Jimbo hilo Nadir Abdul- latif.
Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo akitoa maelekezo kwa Mkuu wa Wilaya Kaskazi ‘A’ Hassan Ali Kombo na Daktari dhamana wa Wilaya hiyo Rahma Abdalla Maisra wakati akikitembelea kituo cha Afya cha Chaani Masingini.
Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo akifuatana na viongozi wa Jimbo la Chaani wakiangalia tanuri la kuchomea taka za kituo cha Afya cha Chaani Masingini alipotembelea kituo hicho.
Mwakilishi wa Jimbo la Chaani Nadir Abdul-latif akimkaribisha Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo kuzungumza na wananchi waliofika kituo cha Afya cha Chaani Masingi ambacho kinahitaji matengenezo makubwa.
Waziri Mahmoud Thabit Kombo akizungumza na wafanyakazi wa kituo cha afya cha Donge na Kamati Kiongozi ya Jimbo hilo katika Kituo cha Afya cha Donge Wilaya Kaskazini B.
Mkuu wa kituo cha Afya Donge vijibweni Miza Ali Ussi akitoa maelezo kwa Waziri wa Afya (hayupo pichani) alipotembelea kituo hicho kujua changamoto zinazowakabili.
Mwakilishi wa Jimbo la Donge Dkt. Khalid Salum Mohammed akizungumza katika mkutano huo (kulia kwake) ni Mkuu wa kituo cha Afya Donge Miza Ali Ussi. Picha zote na Makame Mshenga/Maelezo Zanzibar.

Na RAMADHANI ALI/MAELEZO ZANZIBAR

Waziri wa Afya Zanzibar Mahmoud Thabit Kombo amezitaka Kamati Kiongozi za Majibo kusimamia kikamilifu vituo vyao vya  Afya na kuhakikisha majukumu waliyopangiwa wanayatekeleza kikamilifu  ili kuimarisha huduma katika vituo hivyo.

Alisema Serikali imebadili mfumo katika kusimamia vituo vya afya kwa kuvipeleka moja kwa moja kwa jamii kusaidia huduma ndogo ndogo huku Serikali kuu  ikibakia na jukumu lake la msingi la  kuvipatia vifaa vya matibabu, dawa na mishahara ya wafanyakazi. 

Waziri Mahmoud Thabit Kombo alieleza hayo alipofanya ziara ya kutembelea vituo vya Afya vya Mkoa wa Kaskazini Unguja kujua changamoto zinazowakabili wafanyakazi wa vituo hivyo katika kutoa huduma bora.

Alisema huduma ya matengenezo madogo madogo, kulipia umeme na maji, kuviwekea uzio na ulinzi  sasa vipo chini ya  Kamati Kiongozi za Majimbo ambazo zinaundwa na Wabunge, Wawakilishi, Madiwani, Masheha na Mkuu wa kituo cha Afya husika.

Aliongeza kuwa hivi sasa Serikali haitoa kipaumbele kujenga vituo vipya vya Afya bali inaelekeza nguvu zake kuviimarisha vituo viliopo kwa kushirikiana na mradi wa ORIO na Milele pamoja na Kamati Kiongozi za Majimbo.

Aliwahakikishia wananchi wa Jimbo la Chaani kwamba kituo chao cha Afya cha Chaani Masingini, ambacho kimesitisha kutoa huduma kwa miaka mitano kutokana na kuwa kibovu, kitaanza kufanyiwa matengenezo makubwa hivi karibuni kupitia Mradi wa ORIO.

Waziri wa Afya aliwataka viongozi na wafanyakazi wa sekta ya Afya kuwapa ushirikiano wa karibu wakunga wa jadi ambao wanatoa mchango mkubwa katika kupunguza vifo vya mama wajawazito na watoto wachanga wakati wa kujifungua.

Alisema wakunga wa jadi bado wanaendelea kuaminiwa na wanachi wengi, hasa sehemu za vijijini, kutokana na huduma nzuri wanazotoa kwa wateja wao na ameshauri wapatiwe vitambulisho maalum  ili waweze kutambulika.

Aidha alisema Zanzibar imepata sifa kubwa mbele ya Jamii ya Kimataifa katika kupambana na Malaria na maradhi mengine yaliyokuwa yakiwasumbua wananchi, lakini hali sio nzuri katika kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wachanga hivyo ametaka juhudi zaidi ifanywe kukabiliana na tatizo hilo.

Akinamama wa Jimbo la Chaani walimueleza Waziri wa Afya kuwa wanapendelea zaidi kujifungua kwa wakunga wa jadi kutokana na kauli zisizoridhisha kutoka kwa wakunga wa vituo vya Afya wanapokwenda kujifungua.

Walishauri kutolewa elimu ya ukarimu na upole kwa wakunga wa vituo vya afya ili kuwajengea imani wajawazito kwenda kujifungulia kwa wingi katika vituo hivyo.

Mwakilishi wa Jimbo la Chaani Nadir Abdul-latif alimuhakikishia Waziri wa Afya kwamba yupo tayari kutoa kila msaada unaotakiwa ili kuona huduma za Afya katika Jimbo hilo zinaimarika.

Waziri wa Afya alitembelea vituo vya Afya vya Chaani Masingini, Chaani Kikobweni na Kituo cha Afya   Donge.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad