Nishati : Waziri Prof. Muhongo Azitaka taasisi kuongeza kasi ya miradi ya umeme nchini - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


16 Feb 2016

Nishati : Waziri Prof. Muhongo Azitaka taasisi kuongeza kasi ya miradi ya umeme nchini


Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo akisisitiza jambo katika kikao hicho. 
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo ( kulia) akimweleza Mkurugenzi Mtendaji kutoka Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Kibo Mining, Louis Coetzee (kushoto) fursa za uwekezaji nchini kwenye sekta ya umeme.
Mkurugenzi Mtendaji kutoka Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Kibo Mining, Louis Coetzee ( wa pili kutoka kulia) akielezea mikakati ya kampuni hiyo katika uwekezaji wa uzalishaji wa umeme kwa kutumia makaa ya mawe mbele ya Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo na Watendaji kutoka Wizara ya Nishati na Madini na Taasisi zake.
Mkurugenzi Mtendaji kutoka Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Kibo Mining, Louis Coetzee akifafanua jambo katika kikao hicho.
Na Greyson Mwase, Dar es Salaam.
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo amezitaka taasisi  zinazosimamia miradi ya umeme nchini  kuongeza kasi  ya utendaji kazi ili  Tanzania  iweze kupata umeme wa uhakika.
Profesa Muhongo aliyasema hayo katika kikao chake  kilichokutanisha Kampuni ya Uchimbaji Madini  ya Kibo Mining na watendaji kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Maendeleo la  Taifa (NDC) Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Wizara ya Nishati na Madini.
Alisema kuwa ili nchi iweze kuwa na umeme wa uhakika unaozalishwa kwa wakati ni  lazima  taasisi  zilizopo chini ya  Wizara zikahakikisha zinaongeza kasi katika uwekezaji kwenye  uzalishaji wa umeme kwa kushirikiana na wawekezaji wa ndani na nje  ya nchi wenye  vigezo  ili uchumi wa nchi uweze kukua kwa kasi na kufikia malengo  ya   Dira ya Maendeleo ya Taifa  ya Mwaka 2025 ambayo ni kuhakikisha  kuwa nchi inatoka katika kundi la nchi masikini duniani na kuingia katika kundi la nchi zenye kipato cha kati ifikapo mwaka 2025.
Alisisitiza kuwa ili kufikia lengo hilo ni lazima taasisi zikaongeza kasi katika miradi yake ya umeme, kwa kushirikiana na wawekezaji mbalimbali na kuwataka kuondoa urasimu  kwa wawekezaji wenye nia ya kuwekeza kwenye  miradi ya uzalishaji  wa umeme nchini.
Aliongeza kuwa nishati ni roho ya uchumi wa nchi na kusisitiza kuwa hakuna nchi yoyote duniani iliyopiga hatua bila kuwa na nishati ya umeme ya uhakika.
“ Serikali ya awamu ya tano  imedhamiria kuhakikisha kuwa sekta ya  viwanda inakua kwa kasi na kutoa ajira hivyo kuchangia  ukuaji wa uchumi wa nchi, hivyo nishati ya  umeme inahitajika  sana; bila nishati ya uhakika uchumi hauwezi kukua kwa kasi inayotakiwa,’ alisisitiza Profesa Muhongo.
Waziri Muhongo aliendelea kusema kuwa nishati ya umeme ya uhakika itachangia  ukuaji wa sekta za  viwanda  vidogo  hasa maeneo ya  vijijini, kilimo kukua kwa kasi na  hivyo  kunufaisha wananchi na pato la  taifa kukua kwa kasi.
Aidha Profesa Muhongo alilitaka Shirika la Umeme Tanzania  (TANESCO) na Mamlaka  ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kushirikiana kwa pamoja katika hatua zote za uwekezaji  nchini ili kuondoa mkanganyiko unaoweza kujitokeza kati ya serikali na wawekezaji.
“TANESCO na EWURA naomba mshirikiane katika kila hatua, kwa kukaa meza moja na wawekezaji na kufikia mwafaka kabla  hawajaanza kuwekeza”, alisema Profesa Muhongo
Awali Mkurugenzi Mtendaji kutoka  Kampuni ya Uchimbaji  Madini ya Kibo Mining, Louis Coetzee akizungumza katika kikao hicho, alisema kuwa kampuni ya Kibo Mining  ina  mpango wa kuwekeza katika uzalishaji wa umeme kwa kutumia makaa ya mawe ambapo itaanza na ujenzi wa mtambo wa kuzalisha  umeme kwa kutumia makaa ya mawe wa Megawati 900 kwa awamu tofauti.
Alisema awamu ya kwanza ambayo ni ujenzi wa mtambo wa kuzalisha Megawati 300 utakaogharimu Dola za Marekani milioni 800 utakamilika ifikapo mwaka 2019.
Akielezea hatua iliyofikia ya maandalizi ya uwekezaji wa kampuni ya Kibo Mining  Coetzee alisema kuwa kampuni hiyo iliyoanza maandalizi yake mwaka 2008 inakamilisha   upembuzi  yakinifu (feasibility study) katika mradi  wake na kuongeza kuwa wana mpango wa kuanza ujenzi wa awamu ya kwanza mwaka 2017 baada ya  taratibu zote kukamilika.
Alisema  mara baada ya ujenzi wa mtambo wa kwanza kukamilika mwaka 2019, umeme utakaozalishwa mbali na kutumika  viwandani utaongezwa kwenye  gridi ya  taifa na hivyo kupunguza  changamoto ya ukosefu wa umeme nchini.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad