HATA WALEMAVU WANAWEZA : CHAMI NI MLEMAVU ALIYEHITIMU CHUO KIKUU - Wazalendo 25 Blog

Glory to Story.

Habari Mpya

PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0784 643 633


PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0676 643 633

Tuesday 4 February 2014

HATA WALEMAVU WANAWEZA : CHAMI NI MLEMAVU ALIYEHITIMU CHUO KIKUU

Deogratius Chami, mlemavu wa viungo aliyejikubali na kutafuta elimu licha ya unyanyapaa aliokutana nao hatimaye amehitimu shahada.Picha na Rehema Matowo. 
Suala la  elimu kwa  walemavu limekuwa likipuuzwa na wazazi, jamii na Serikali kwa ujumla

Zipo baadhi ya familia ambazo zinaamini ulemavu ni laana ama mkosi, jambo linalosababisha mtoto anayezaliwa na ulemavu kuishi maisha ya kificho na wakati mwingine huuawa, wakiamini kuwa kuzaa mlemavu ni laana kwenye familia.

Hata hivyo, kuna familia zinazojenga uthubutu na kuionyesha jamii kuwa ulemavu sio laana wala mkosi; kwamba watoto wao walio na ulemavu huwasaidia kupata elimu na mahitaji mengine muhimu.

Nimekutana na mlemavu wa viungo ambaye anatembea na kiti cha magurudumu, miguu yake yote miwili haina uwezo wa kutembea.

Mlemavu huyu ni mhitimu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Ushirika na Biashara Moshi; amepata Shahada ya Maendeleo ya Jamii na anaamini  ulemavu alionao  siyo kasoro bali ni uwezo wa Mungu kuonyesha karama zake.

Deogratius Chami (29), ni mlemavu ambaye katika ulemavu huo ameyaona mengi ikiwa ni pamoja na kunyanyapaliwa kila anapofika katika baadhi ya ofisi za Serikali au kuzungumza na mtu kwa lengo la kutaka kusaidiwa kielimu .

Chami anasema hakuzaliwa akiwa mlemavu, bali alipata ulemavu akiwa darasa la tano mwaka 1997;ulemavu wake ulisababishwa na kuporomoka kwenye udongo maeneo ya Kibosho wilaya ya Moshi Mkoani Kilimanjaro.

Anasema ajali hiyo ilimfanya alazwe hospitali ya rufaa ya KCMC kwa miaka miwili  na baadaye alipata msamaria aliyempeleka kwenye Kituo cha Moshi Chaple,  akaishi hapo ili aweze kupata elimu kwa kuwa ndio kitu pekee alichokuwa akitamani kwa wakati huo.

Anasema akiwa mtoto wa sita kati ya watoto 11 wa familia yao ,asingeweza kuendelea na masomo kutokana na hali ya ulemavu aliyokuwa nayo huku familia yao ikiwa ni ya kipato cha chini ikitegemea kilimo cha kawaida kilichokuwa kikiwasaidia kupata mlo tu.

Anasema ufadhili alioupata wa kuishi Moshi Chaple ulimsaidia kurudi darasani ambako mwaka 1999 ilimlazimu kurudia darasa la tano katika Shule ya Msingi Kilimanjaro  na kwa uweza wa Mungu alifaulu na kujiunga na Shule ya Sekondari Old Moshi hadi mwaka 2005. Anasema kutokana na ulemavu aliokuwa nao alikuwa akikaa kwenye kiti cha magurudumu muda wote hali iliyomsababishia vidonda vilivyosababishwa na kukaa kwa muda mrefu hivyo kumfanya ashindwe kuingia darasani.

Hali hiyo ilimfanya afanye vibaya darasani, walimu wake walijaribu kumshauri kurudia darasa lakini yeye alipinga na kuamua kufanya mtihani wa kidato cha nne na kwa bahati mbaya matokeo hayakuwa mazuri hivyo akashindwa kuendelea na kidato cha tano.

Siku zote wahenga wanasema penye nia pana njia na ndio msemo aliousema Chami. Anasema baada ya kutafakari sana aliamua kurudi darasani na kurudia mtihani mwaka 2006 akiwa kama mwanafunzi wa kujitegemea na kufanikiwa kufaulu na kujiunga na kidato cha tano mwaka 2007 katika Shule ya Sekondari Majengo.
Matokeo ya kidato cha sita yalikuwa mazuri ambayo yangemuwezesha kuendelea na elimu ya juu lakini kutokana na umaskini wa kipato na familia kutokuwa na uwezo alishindwa kuingia darasani kama wanafunzi wengine jambo ambalo lilimuumiza sana.

Anasema alihangaika kuingia kwenye mashirika binafsi  na kwenye ofisi za Serikali lakini hakufanikiwa hata kujieleza kwa kuwa kila anapofika kabla hata ya salamu hujibiwa ‘leo hatuna njoo kesho ‘wakimuona yeye ni ombaomba.

Anasema jambo hilo lilikua likimuumiza sana kutokana na ukweli kwamba hakuwa ombaomba kama walivyofikiri.

Anasema nenda rudi kwenye ofisi hizo ndio ulikuwa mlango wake wa mafanikio kwani kutokana na yeye kutokata tamaa ya kwenda na kurudi kesho yake ndio ilimgusa mfanyakazi mmoja wa ofisi ya mkuu wa wilaya aliyemtaja kwa jina moja la Koshuma aliyetaka kujua tatizo la yeye kufika katika ofisi hizo kila siku.

Anasema Koshuma alimsikiliza kama mtoto anavyozungumza na baba  yake na kuahidi kumsaidia na ndipo mlango wa mafanikio ya kusonga mbele ulipofunguka.

Anasema Koshuma alimkutanisha na Peter Kisumo mzee ambaye kwake amekuwa kama daraja la kusonga mbele kwa kuwa alimkubali kama mtoto na kumwahidi kumsaidia kwa kadri ya uwezo wake.

Ndipo alipomtafutia mfadhili aliyemtaja kwa jina la Atul ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Mount Meru ambaye alikubali kumsomesha kwa kipindi cha miaka mitatu akiwa Chuo Kikuu Ushirika.

 “Kwa kweli nawashukuru sana wote walionisaidia, hasa Atul na Kisumo, Mungu awabariki sana,” anasema.

Anaushukuru pia uongozi wa chuo kwa kumsaidia kusoma vizuri kwani walihakikisha hakuna mwanafunzi anayemnyanyapaa. Chanzo MWANANCHI

No comments:

Post a Comment