Matukio : Mama Salma- Autaka Mkoa wa Pwani Kupambana na Mafataki Kuondoa Tatizo la Mimba za Utotoni - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


12 Oct 2017

Matukio : Mama Salma- Autaka Mkoa wa Pwani Kupambana na Mafataki Kuondoa Tatizo la Mimba za Utotoni



MKE wa rais mstaafu ,mama Salma Kikwete ,akiwa katika maadhimisho ya siku ya mtoto wa kike kimkoa Mkoani Pwani yaliyofanyika Kibaha na kufadhiliwa na shirika lisilo la kiserikali la Room To Read linalotekeleza mradi wa kumwendeleza mtoto wa kike.Picha na Mwamvua Mwinyi




Na Mwamvua Mwinyi,Kibaha


MKE wa rais mstaafu ,mama Salma Kikwete,amesema mkoa wa Pwani upambane na mafataki wanaoteka fikra za watoto wao wa kike ili kuondokana na mimba za utotoni ambapo mkoa huo ni kati ya mikoa kumi inayoongoza kwa mimba hizo kitaifa.


Aidha amekemea tabia inayofanywa na mashuga dadi wanaojiona mahodari wa kutongoza na kunyemelea watoto wa kike wanafunzi na wengine kuwakatisha masomo kwa kuwatia mimba na kudai anaejiona hodari wa kutongoza dunia aende kwa wanawake wakubwa huko mitaani.


Pamoja na hilo,Mama Salma ,ameitaka jamii kuachana na mila na desturi zinazochochea mimba ,na kusema lazima zitazamwe ili kuwawezesha watoto hao waendelee na masomo yao.


Aliyasema hayo,wakati wa maadhimisho ya siku ya mtoto wa kike kimkoa,yaliyofanyika wilayani Kibaha mkoani Pwani,ambayo yamefadhiliwa na shirika lisilo la kiserikali la Room To Read.


Alisema mkoa unaoongoza kwa mimba za utotoni ni mkoa wa Katavi wenye asilimia 45 ambapo mkoa wa Pwani upo ndani ya mikoa kumi inayoongoza kwa mimba hizo ukiwa na asilimia 30.


Mama Salma alisema,mimba za utotoni hazikubaliki ,watoto wa kike wajitambue , na wajijue wao ni lulu ,na thamani ya mtoto wa kike ni kufunga mapaja,wafunge mapaja yao na wakifunga mapaja hakuna mdudu atakaeingia.“Situmii kitu kinachoitwa tafsida hapa,naongea kama ilivyo ili mzidi kunielewa na walengwa yawaingie kikamilifu kichwani mwao”,alisema mama Salma.


Alisema ni wakati wa mkoa huo kuongoza kielimu na kuwa kumi bora kitaaluma badala ya kuongoza kwenye mimba za utotoni.Hata hivyo Mama Salma alieleza kwamba,tabia inayofanywa na baadhi ya wazazi wanaodiriki kufanya mapenzi na watoto wao wa kike ni lazima ilaaniwe duniani kote,ili kukomesha vitendo hivyo vya aibu.


Alisema dunia ya leo imeharibika kwani wapo wazazi ambao wanawabaka ama kuwafanya mapenzi watoto waliowazaa wenyewe bila ya kuona aya.Alieleza pia,vijana na wazee(mashuga dadi) wanaokimbilia watoto wadogo waliopo mashuleni waache tamaa za kimwili na atakaebainika atafungwa miaka 30 jela .


Mama Salma aliitaka jamii kuheshimu na kujali watoto wa kike maana ni nguzo ya maendeleo ya taifa ,dhana potofu zikomeshwe zinazowanyanyapaa na kuwadhalilisha watoto wa kike na ikumbukwe malezi na makuzi ya watoto wa kike ni wajibu kwa kila mmoja kwenye jamii .“Unavyoona huwezi kufanya mapenzi na mtoto wako basi usijaribu kufanya mapenzi na mtoto wa jirani yako,kwani mtoto wa mwenzio ni wako,”


Mama Salma aliwaambia wazazi na walezi, watenge muda wa kuwafundisha kujikinga na majaribu wanayokutana nayo kwenye mzunguko wa maisha yao,wawape haki za msingi zinazostahili ikiwa ni sanjali na elimu sawa na watoto wa kiume.Aliwaasa na wanafunzi wa kike wakubaliane na hali ya maisha waliyonayo wazazi wao wasiwe na tamaa hali inayosababisha kupata vishawishi.


Mama Salma,aliwahusia watoto hao watumie stadi walizopatiwa kama silaha ya kujikinga na maadui hivyo wasikubali kuzima ndoto zao na elimu .
“Someni msikimbilie kuolewa ,mtapata mnachokitaka hadi mtachoka,wanaume wapo tuu,serikali inahimiza msome na kuwawekea misingi mizuri ya kielemu ikiwemo kusomeshwa bure, acheni mchezo,jilindeni”


“Ni haki ya mtoto wa kike nae kujilinda,ajitunze ili siku moja afikie ndoto zake kuwa mwalimu,mainjinia ama madaktari bingwa.mawaziri, makamu wa rais”.Mama Salma alielezea,kwasasa nchi inajivunia kuwa na naibu katibu mkuu wa kwanza mwanamke wa umoja wa mataifa kutoka Tanzania,Asharose Migiro ,makamu wa rais mwanamke wa kwanza Samia Suluhu Hassan na waziri wa fedha wa kwanza Tanzania Zakia Meghji.


“Wapo wengi nikiwataja hapa hawatoshi ,hawa wametupa heshima na wamefika hapo kutoka na elimu,jaribuni kufanya bidii mfikie malengo yenu,“Ninawausia ni lazima kuienzi elimu kwanza,tunahitaji walimu kutoka nchini sio nje ya nchi,na kuacha kubeza ualimu kuwa kwenda ualimu ni hadi ukose kazi nzuri nyingine ,alifafanua Mama Salma.


Katika hatua nyingine alisema anaimani kutatiliwa mkazo kwa kuingiza somo la stadi za maisha katika mtaala wa shule nchini ili kujenga wasichana waweze kujisimamia na kujitambua wenyewe .Mama Salma alisema,tumekuwa tukijifunza mengi kupitia miradi mbalimbali ya kufundisha stadi za maisha ikiwemo kupambana na mimba za utotoni.


Alitoa wito kwa wadau wa elimu ,halmashauri kuchangia changamoto hizo kwa kutenga bajeti za ujenzi wa mabweni ya wanafunzi wa kike katika shule za sekondari”,Sanjali na madarasa na maabara kwani itakuwa rahisi kuzungumza na mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali yaweze kusaidia kirahisi.


Nae mkuu wa wilaya ya Kibaha,Assumpter Mshama ambae alimwakilisha mkuu wa mkoa huo,alisema zipo baadhi ya mila na desturi zipo mkoani hapo ambazo zinachangiua kukatisha masomo ya watoto kwa kuwaoza kabla ya kumaliza masomo yao.


Alisema utoro na mimba mkoani Pwani ni sababu kubwa inayoshusha taaluma kwa watoto kijumla kwani kwa mwaka huu watoto wa kike 61 wa darasa la saba mkoani hapo wamepata mimba na kushindwa kufanya mitihani yao ya mwisho.Assumpter alieleza ,utoro ni 58 ,vifo sita na magonjwa ni 12 hivyo watoto watambue umuhi wa kujiendelea kielimu kama ufunguo wao wa maisha.


Kwa upande wake,afisa elimu mkoa wa Pwani ,Germana Sondoka alisema wataendelea kusimamia maelekezo ya serikali na kimataifa ambayo yanahusika kumlinda mtoto wa kike ili aweze kutimzia ndoto zake.


Alisema watahakikisha wanafunzi mkoani humo hasa wa kike wanafikia malengo yao na kutokomeza vitendo vinavyochangia kumkatisha mtoto huyo masomo yake.


Germana alieleza kufuatia kaulimbiu ya kutokomeza mimba za utotoni kufikia uchumi wa viwanda ,watashirikiana baina ya serikali mkoa,maafisa elimu,walimu na wanafunzi kwa kuendelea kuitafsiri kauli hiyo kwa vitendo.


Mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali la Room To Read,wanatekeleza mradi wa kumwendeleza mtoto wa kike ,Peter Mwamanga,alisema shirika hilo lilianza mwaka 2012 ambapo wanafundisha pia stadi za maisha kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.


Alisema mtoto wa kike amekuwa akipambana na changamoto nyingi hadi kufanikiwa na kujikuta zipo anazokutana nazo na kusababisha ndoto zake zikififia siku hadi siku.Mwamanga alitoa wito kwa wadau mbalimbali kushirikiana kutokomeza vitendo vya mimba za utotoni na kupambana na wale wanaokatisha masomo ya watoto hao.


Room To Read walichukua fursa hiyo kumpatia tuzo mama Salma ya kutambua na kuthamini mchango wake wa kuwakomboa na kupambana kutetea haki za mtoto wa kike na mimba za utotoni,kupitia WAMA.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad