SERIKALI ya Tanzania, imeshukuru Mfuko wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNCDF) kwa kuwezesha watanzania kupambana na umaskini kupitia miradi wanayoidhamini au kuitafutia fedha. Kwa miongo miwili UNCDF imekuwa ikifanya kazi kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania kupitia ofisi ya rais Tawala za Mikoa na serikali za mitaa (TAMISEMI) katika mpango wa kupeleka madaraka kwa umma na shughuli za maendeleo ya kiuchumi .
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhandisi Mussa Iyombe katika hotuba yake iliyosomwa na Katibu Tawala wa mkoa wa Kilimanjaro Aisha Amour kwenye ufunguzi wa kongamano la siku 2 la Wadau wa Ufugaji Samaki Kibiashara Bwawa la Kalemawe lililoko wilaya ya Same mwishoni mwa wiki.
“Tunafurahishwa kwa namna ya pekee na UNCDF kwa jitihada zake zinazoendeshwa kupitia katika Mpango wa Ufadhili Miradi ya kiuchumi (LFI),” alisema Iyombe na kuongeza: “Tunapokutana hapa tunapewa fursa na kufunuliwa uzoefu wa ushiriki wa UNCDF katika miradi mbalimbali, safari hii tukishuhudia hatua yake ya kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Same katika Mkoa wa Kilimanjaro.”
Pamoja na kushukuru kwa hatua mbalimbali zilizofikiwa na taasisi hiyo katika kusaidia watanzania, aliwataka wakazi wa Same kuhakikisha kwamba mradi huo ulioundiwa kampuni ili kwenda kibiashara unafanikiwa na kuwa mfano kwa wengine. Halmashauri ya wilaya ya Same, na jamii inayozunguka bwawa la Kalemawe wanashirikiana na UNCDF kuboresha miundo mbinu ya bwawa hilo na kuwezesha uwapo wa uwekezaji kwa kuanzisha kampuni.
Kampuni hiyo iliyosajiliwa ya Kalemawe Dam Investment Limited katika mpango maalum (SPV) inamilikiwa na wadau mbalimbali ikiwemo Halmashauri ya wilaya ya Same, halmashauri ya vijiji sita, wakala wa serikali, watu binafsi pamoja na makundi ya kijamii. Kuwapo kwa kampuni hiyo ni juhudi zinazofanywa za kuwezesha uhusiano mahsusi wa kibiashara unaohusisha ubia wa Serikali, Binafsi na jamii (PPCP) kwa kutoa umiliki linganifu mpaka katika ngazi za chini za mamlaka za kijiji, ambazo kimsingi ndizo wamiliki wa maliasili muhimu ya ardhi kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi ya Vijiji ya Mwaka 1999.
Mradi huo wa Ufugaji wa Samaki Kibiashara wa Bwawa la Kalemawe ni zao la ushirikiano kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Same, Kata za Ndungu na Kalemawe, asasi zisizo za kiserikali na wadau wa maendeleo walioazimia kukarabati na kufufua bwawa hilo na mfumo wake wa kilimo cha umwagiliaji. UNCDF kwa kushirikiana na wabia wake waitwao Mikono Tayari (ambao ni kundi linaloundwa na washirika kutoka Tanzania na Norway) ni wataalamu katika mradi hu wa ufugaji samaki kwa pamoja na SPV ya Same na washirika wake.
Katika kongamano hilo Mkuu wa wilaya ya Same Rosemary Staki amesema wilaya yake ipo tayari kutekeleza mradi huo ambao una manufaa makubwa si tu kwa watu wa Kalemawe na vijiji vinavyozunguka bali pia na halmashauri ya wilaya ya Same.
Akishiriki katika mjadala aliwataka wanakalemawe kutambua umuhimu wa mradi huo na kwamba hicho ni kichocheo cha ukuaji wa uchumi wa watu binafsi na jamii kwa ujumla. Mradi huo ambao ni sehemu ya programu kubwa ya kubadili watu wenye makazi kuzunguka bwawa hilo umelenga katika siku za usoni kuzalisha samaki na vifaranga vyake.
Ili kuwa na uelewa mkubwa wa kufanya biashara hiyo ya samaki, madiwani na wenyeviti wa serikali za mitaa za vijiji vinavyotengeneza kampuni hiyo ya Kalemawe walitembelea shamba la samaki Ruvu ambapo waliona shughuli mbalimbali zinazoendelea katika shamba hilo ili iwe mfano kwao Pamoja na kuuza samaki shamba hilo ambalo lipo kilomita 20 kutoka Bagamoyo na kilomita 13 hivi kutoka Mlandizi linafuga samaki aina ya sato na hutotolesha vifaranga laki moja kila wiki kwa kulingana na oda zilizopo.
Mmoja wa viongozi katika mradi huo Khumbo Kanthenga alisema kwamba mradi huo ambao bado unapanuliwa kufikia mabwawa sitini kwa sasa umelenga kutoa vifaranga kwa mujibu wa oda na pia kuuza samaki ambao wapo tayari kuingia sokoni samaki hao wanafikia gramu 350 na kuendelea. Naye Mbunge wa Same Mashariki, Naghenjwa Kaboyoka ambaye alikuwapo katika kongamano hilo alielezea haja ya wananchi wengi kutambua mipaka yao na kuhakikisha kwamba dhamira safi iliyopo ya kufufua bwawa hilo na kubadilisha maisha ya wananchi inafikiwa.
Wakifunga Kongamano hilo UNCDF ili shukuru ushirikiano mkubwa wa karibu ambao umeonyeshwa na washiriki wa warsha hii ya wadau kuanzia serikali kuu, mkoa, willaya na viongozi wa vijiji sita vinavyohusika na utekelezaji wa mradi na pia iliahidi kua mashirika mengine ya umoja wa mataifa watashirikishwa kuwa sehemu ya utekelezaji wa mradi huu na miradi mingine mbalimbali katika eneo hili la bwawa la samaki.
No comments:
Post a Comment