Matukio : Umoja wa Wazazi CCM Zanzibar Wawaasa Viongozi Kuongeza kasi ya Utekelezaji wa Ahadi zao Walizotoa - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


14 Jun 2017

Matukio : Umoja wa Wazazi CCM Zanzibar Wawaasa Viongozi Kuongeza kasi ya Utekelezaji wa Ahadi zao Walizotoa


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.


MAKATIBU wa Wilaya za Umoja wa Wazazi CCM Zanzibar wamewashauri viongozi mbali mbali wa Chama cha Mapinduzi kuongeza kasi ya utekelezaji wa ahadi walizotoa ndani ya taasisi hiyo ili kupunguza changamoto za kiutendaji.


Rai hiyo imetolewa na baadhi ya Makatibu wa Wilaya Sita za Umoja huo Zanzibar mara baada ya kukabidhiwa Komputa zilizotolelewa na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja huo, Bi. Najma Giga ikiwa ni miongoni mwa utekelezaji wa ahadi alizowahi kutoa wakati wa ziara zake Visiwani humo.


Katibu wa Wazazi Wilaya ya Amani , Bi.Mwanaisha Ame Mohamed amesema upatikanaji wa vifaa hivyo utaongeza ufanisi wa kiutendaji ndani ya umoja huo kwani watakuwa na vitendendea kazi vya kisasa vitakavyorahisisha utendaji wa kazi zao.


Aidha Katibu huyo amewataka baadhi ya Wabunge, Wawakilishi na Madiwani ambao bado hawajahamasika kuanza kutekeleza ahadi zao kwa umoja huo na chama kwa ujumla kufuata nyayo za viongozi wenzao walioanza kutatua kero za taasisi hiyo hatua kwa hatua.


“Huu ni wakati wa viongozi mbali mbali wa Chama chetu pamoja na jumuiya zetu kujitokeza kusaidia baadhi ya Mikoa na Wilaya zenye upungufu wa vitendea kazi ili waweze kukamilisha shughuli za uchaguzi kwa ufanisi.”, alisema Katibu Mwanaisha.


Naye Katibu wa Wazazi Wilaya ya Wete Pemba, Bi. Mariam Ali Said amemshukru Naibu Katibu Mkuu wa Wazazi Zanzibar kwa kutekeleza ahadi zake kwa vitendo na kuongeza kuwa vifaa hivyo ni chachu ya kumaliza changamoto za kufuata huduma za uchapaji wa nyaraka za kiofisi masafa ya mbali.


Akizungumza Kaimu Naibu Katibu Mkuu Wazazi Zanzibar, Nd. Mustafa Rashid Kumwalu kwa niaba ya Naibu Katibu Mkuu wa umoja huo Bi. Najma Gina mara baada ya kukabidhi Komputa hizo ametoa wito kwa watendaji wa umoja huo kutumia komputa hizo kwa matumizi yaliyokusudiwa ili shughuli za kiutendaji zifanyike kwa wakati mwafaka.


Nd. Rashid alieleza kuwa lengo la umoja huo ni kuhakikisha watendaji wake wanapata vitendea kazi vya kisasa vitakavyosaidia kutekeleza kwa wakati shughuli za kiutendaji kwa lengo la kwenda sambamba na matakwa ya Katiba ya CCM iliyofanyiwa mabadiliko miezi kadhaa iliyopita.


Aidha alisema Komputa zilizokabidhiwa mpaka sasa ni tisa bado kumi kwa mujibu wa idadi ya komputa zilizoahidiwa kutolewa na Naibu katibu Mkuu wa Umoja huo, ambaye pia ni Mbunge wa kuteuliwa kutoka ndani ya Umoja wa Wazazi Tanzania.


Komputa hizo zina thamani zaidi ya shilingi milioni Saba zimekabidhiwa kwa Wilaya 6 za Umoja wa Wazazi CCM Wilaya ya Amani, Wilaya ya Mfenesini, Wilaya ya Kati, Wilaya ya Kaskazini “B”, Wilaya ya Wete na Wilaya ya Chake Chake Pemba.



Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wazazi Zanzibar , Mustafa Rashid Kumwalu akimkabidhi Katibu wa Wazazi Wilaya ya Kaskazini “B” Unguja , Bi. Salma Shaibu, kwa niaba ya Naibu Katibu Mkuu wa Umoja huo Bi.Najma Giga.

Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wazazi Zanzibar Nd. Mustafa Rashid Kumwala akitoa nasaha kwa Makatibu wa Wilaya Sita za Umoja huo kabla ya kuwakabidhi komputa hizo.

Baadhi ya Komputa zilizotolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wazazi Zanzibar, Bi.Najma Giga kwa Wilaya Sita za umoja huo Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad