Matukio : Zanzibar Haibaguliwi katika EAC - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


18 May 2017

Matukio : Zanzibar Haibaguliwi katika EAC



Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, akimkaribisha Mkurugenzi wa Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii, Bw. Eliabi Chodota kutoa mada kwenye semina ya mtangamano inayoendelea Kisiwani Pemba. Ushiriki na mwitikio katika semina hiyo umekuwa mkubwa kwa washiriki ambapo wameonekana kuvutiwa sana na semina hii pia wamekuwa wadadisi wazuri wa kutaka kujua zaidi fursa zinazo patikana kwenye mtangamano huo.

Bw. Chodota akitoa mada kwenye semina ya mtangamano inayoendelea Pemba.

Sehemu ya washiriki wakisikiliza kwa makini mada iliyokuwa ikitolewa na Bw. Chodota (hayupo pichani).

Bw. Chodota akiendelea kutoa mada yake.

Mmoja wa washiriki Bi. Kauthari akiuliza swali mara baada ya mada kumalizika kutolewa na Bw. Chodota hayupo pichani.

Sehemu nyingine ya washiriki wakimsikiliza kwa makini.

Bw. Chodota akijibu swali lililokuwa limeulizwa na Bi Kauthari (hayupo pichani).

Bw. Suleimani Haji kutoka ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar naye akitoa mada kuhusu nafasi ya Zanzibar kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Sehemu ya washiriki wakimsikiliza kwa makini Bw. Suleimani (hayupo pichani).

Washiriki wakisikiliza kwa makini mada na maswali yaliyo kuwa yakiulizwa na washiriki wengine.

Mhe. Mbarouk Salim Ali Mbunge wa Jimbo la Wete akiuliza swali kwenye semina. Pembeni yake ni Mbunge wa Jimbo la Konga, Mhe. Mbarouk Ali akisikiliza kwa makini.

Meneja wa TRA kwa upande wa Kisiwani Pemba Bw. Habibu Saleh naye akiuliza swali kwa mtoa mada, Bw. Suleimani (hayupo pichani).

Bw. Salehe akijibu maswali hayo na kutolea ufafanuzi kwa baadhi ya mambo.









Serikali ya Zanzibar inashiriki moja kwa moja bila ukomo katika masuala yote ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), hivyo Wazanzibari wamehimizwa kuchangamkia fursa zilizopo kwenye Jumuiya hiyo na kuondokana na dhana kuwa eti, Serikali yao inabaguliwa.


Akiwasilisha mada leo kuhusu ushiriki wa Zanzibar katika Jumuiya ya Afrika Mashariki kwenye semina ya masuala ya mtangamano wa EAC inayofanyika Pemba, Afisa wa Ushirikiano wa Kimataifa kutoka Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Bw. Suleima Haji alitoa ufafanuzi wa kina kuonesha namna Zanzibar inavyoshiriki katika EAC.


Bw. Haji alieleza kuwa licha ya Zanzibar kuwa sehemu ya muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ushiriki wake umedhihirika katika mgawanyo wa miradi ya maendeleo ya EAC, hususan miradi ya Miundombinu. Alisema Zanzibar iliwasilisha mapendekezo ya miradi 10 kwenye Sekretarieti ya EAC na kutokana na vipaumbe vilivyowekwa miradi 3 imekubaliwa na mchakato wa kuitekeleza unaendelea. Miradi hiyo ni ujenzi wa Bandari ya Marhubi kisiwani Pemba, upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Pemba na ununuzi wa meli kubwa zitakazosafirisha abiria na mizigo kwenye nchi wanachama wa EAC.




Aidha, kwenye miradi inayofadhiliwa na washirika wa maendeleo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Zanzibar haijasahaulika. Zanzibar inanufaika na miradi inayofadhiliwa na taasisi inayojihusisha na masuala ya kukuza biashara na kupunguza umasikini katika nchi za EAC inayoitwa "East Africa Trademark" (TMEA). TMEA ambayo ni mdau mkubwa wa EAC inafadhili mradi ambao unawawezesha Wazanzibari kufanya maombi kwa njia ya mtandao ili kupata cheti cha uasili wa bidhaa. Cheti hicho ni muhimu kwa wafanyabiashara kwani kinatambulisha bidhaa yako ilipotengenezwa na kupata msamaha wa kodi ya forodha inapoingia nchi nyingine za EAC.


Mradi mwingine unaofadhiliwa na TMEA huko Zanzibar ni ule wa kuwasilisha malamiko kwa njia ya mtandao au ujumbe mfupi wa simu pale inapotokea mfanyabiashara amekumbana na vikwazo visivyo vya forodha katika kusafirisha bidhaa zake ndani ya Jumuiya. Ujumbe huo utakapopokelewa, kikwazo kilicholalamikiwa kitafanyiwa kazi na taasisi husika mara moja.


Benki ya dunia pia inaendesha mradi wa kutathmini utekelezaji wa Soko la Pamoja kwa upande wa Zanzibar. Kama inavyotambulika soko la pamoja lina vipengele vingi vikiwemo; usafirishaji huru wa bidhaa, huduma, mtaji na watu. Hivyo kuna umuhimu wa kupima namna nchi wanachama zinavyotekeleza vipengele hivyo.


Ushiriki wa Zanzibar unapatikana pia kwenye uenyeji wa taasisi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Zanzibar imebahatika kuwa mwenyeji wa Kamisheni ya Kiswahili ya EAC. Kuwa mwenyeji wa taasisi kuna faida kubwa zikiwemo kujitangaza na ajira. Kwa upande wa ajira, Bw. Haji alisema sio tu Wazanzibari wanafaidikia na ajira za Kamisheni ya Kiswahili, bali wanapata ajira hata katika Sekretarieti ya EAC na kutolea mfano kuwa Mhasibu Mkuu wa kwanza wa Sekretarieti hiyo alikuwa Mzanzibari.


Vile vile, Zanzibar imekuwa mwenyeji wa vikao mbalimbali vya taasisi za Jumuiya. Mwaka 2010 Mahakama ya Afrika Mashariki ilifanya kikao chake Zanzibar, Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) lilifanya kikao chake Zanzibar mwaka 2016 na mwezi Agosti mwaka huu utafanyika mkutano mkubwa wa masuala ya Kiswahili mjini Zanzibar. Aliendelea kusema kuwa katika Bunge la EALA la kipindi hiki, Zanzibar ina wabunge watatu, wawili wakitokea CCM na mmoja CUF.


Alihitimisha mada yake kwa kuwasihi Wazanzibari waache fikra potofu za kujihisi kubaguliwa badala yake waunganishe nguvu kuchangamkia fursa lukuki za kibiashara zilizopo kwenye mtangamano wa EAC. Alisema Serikali ya Zanzibar inashiriki katika kila jambo ikiwemo kushiriki mikutano ya Marais. Mawaziri na Wataalamu ili kutetea maslahi ya Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.




Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,


Dar es Salaam, 18 Mei, 2017

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad