Matukio :Operesheni ya Viroba Yaibua Wafanyabiashara Wasiokuwa na Vibali vya TFDA. - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


8 Mar 2017

Matukio :Operesheni ya Viroba Yaibua Wafanyabiashara Wasiokuwa na Vibali vya TFDA.






Na: Lilian Lundo – MAELEZO.


Operesheni ya kuondoa pombe kali zilizofungwa katika vifungashio vya plastiki (viroba) inayoendelea nchi nzima imeibua wafanyabiashara wanaofanya biashara ya pombe bila kuwa na vibali vya Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA).


Hayo yamebainishwa na Afisa Afya na Mratibu wa Masuala ya Chakula wa Manispaa ya Temeke Rehema Sadick, leo Jijini Dar es Salaam wakati wa operesheni hiyo inayoendelea nchini.


“Katika operesheni hii ya kuondoa pombe za viroba tumegundua wafanyabiashara wengi wanaojihusisha na uuzaji wa pombe kutokuwa na kibali cha TFDA ambacho hutolewa katika Halmashauri husika,” alifafanua Rehema Sadick.


Aidha amebainisha kuwa katika msako uliofanyika leo Kigamboni, ambapo wamekagua zaidi ya maduka matano yanayouza pombe kwa jumla, ni duka moja tu la Mangale Store lililoko Tuangoma ndilo lililokutwa na kibali cha TFDA.


Aliongeza kuwa, maduka yote ambayo hayakuwa na vibali hivyo yameamuliwa kufungwa na kufuatilia vibali katika Halmashauri husika na taarifa za maduka hayo ikiwemo jina la duka, majina ya mmiliki eneo lilipo pamoja na namba za mawasiliano vimechukuliwa kwa ajili ya kuchukua hatua.


Afisa Afya huyo ametoa rai kwa wafanyabiashara wote kuacha kufanya biashara kwa mazoea na kuhakikisha wanakuwa na vibali vyote muhimu pamoja na leseni za biashara, kwani kutofanya hivyo ni kukiuka sheria na kanuni za nchi.


Operesheni ya kuondoa viroba ilianza rasmi Machi 01, 2017 kufuatia agizo la Waziri Mkuu Kassim Majaliwa la kutaka kusitishwa kwa utengenezaji, usambaaji, uuzaji na utumiaji wa pombe hizo kali maarufu kama viroba.ifikapo Machi mosi mwaka huu ambapo mpaka sasa operesheni hiyo imeingia siku ya tano tangua kuanza kwake.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad