Matukio : Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Atangaza kiama kwa wala Rushwa hasa Watumishi wa Umma - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


26 Jan 2016

Matukio : Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Atangaza kiama kwa wala Rushwa hasa Watumishi wa Umma

 Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (Takukuru), Kamishna Valentino Mlowola akizungumza na wanahabari.
 Kaimu Mkurugenzi Mkuuwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (Takukuru), Kamishna Valentino Mlowola (kushoto), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari ofisini jijini Dar es Salaam leo asubuhi kuhusu mikakati mbalimbali ya taasisi hiyo ya kupambana na rushwa nchini hasa kwa watendaji wa Umma na kesi zinazochunguzwa ili watuhumiwa wafikishwe mahakama wakati wowote baada ya kukamilika kwa uchunguzi wake.
 Wanahabari wakichukua taarifa hiyo. Kulia ni John David wa Gazeti la Majira.
 Mwendeshaji wa Mtandao wa Fullshangwe, John Bukuku (kulia), akiuliza swali katika mkutano huo.
Baadhi ya wakurugenzi wa Taasisi hiyo wakiwa katika mkutano huo.

Na Dotto Mwaibale

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (Takukuru), imetoa onyo kwa taasisi nyeti nne hapa nchini ikiwemo wanaohusika na matumizi ya fedha za Umma kufuata sheria, taratibu na kanuni.

Pia,Takukuru inashughulikia kukamilisha kesi kubwa 36, zinazowahusu watumishi wenye ushawishi na hadhi kubwa hapa nchini ambapo kati ya hizo zipo zilizokamilika na kupelekwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo , Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo, Valentino Mlowola alisema kumekuwepo na malalamiko mengi kwa wananchi kuwajulisha matendo ya rushwa na ufisadi yanayoendelea hapa nchini.

Alisema kutokana na hali ya wananchi kuona nia ya serikali ya awamu ya tano katika kushughulikia matatizo ya rushwa na ufisadi hapa nchini ametoa ovyo kwa maofisa wa umma wanaofanya rushwa na ufisadi kuwa sehemu yao ya kazi na miradi ya kuwaingizia kipato.

"Natoa onyo kwa maofisa wa umma ambao wamefanya rushwa na ufisadi kuwa ni sehemu ya kazi zao na miradi ya kuwaingizia kipato, wajitafakari kabla hawajaamua kujihusisha na vitendo vya rushwa,"alisema.

Alisema  hawatasita kuchukua hatua kali za kisheria kwa watumishi watakaojiingiza katika kulihujumu taifa na wananchi kwani wananchi wanakiu ya kupata maendeleo na maisha bora na kuwataka watambue wananchi wa jana si wa leo kwani wamedhamiria kuunga mkono juhudi za serikali yao.

Mlowola alitoa ovyo kwa maofisa maduhuli na watekelezaji wa jukumu la kukusanya kodi za wananchi kwa kutomuonea mtu haya kwa atakayejihusisha na ubadirifu wa fedha na mali ya umma.

"Wakusanye kodi halali ya serikali kwa kufuata sheria, taratibu na Kanuni zinazowaongoza kukusanya kodi, tutachukua hatua stahiki pale kutakapokuwa na ukiukwaji wa sheria, taratibu na kanuni zilizopo,"alisema.

Pia, Mlowola alitoa ovyo kwa watakaohusika kwenye matumizi ya fedha za umma kwamba wafuate sheria, taratibu na kanuni  zinazowaongoza kwani taasisi hiyo haitawavumilia watakaokiuka fedha za serikali isiyo halali.

Mbali na hilo, pia Kaimu huo alitoa onyo kwa watumishi wa umma wenye jukumu la kuhudumia mahitaji ya umma kwa kutojihusisha na rushwa kwa kutekeleza majukumu yao katika muda uliotakiwa, weledi na uaminifu.

Alisema taasisi hiyo haipo kwa lengo la maslahi ya watu wabadhilifu wa mali ya umma kwani uchunguzi wa kesi ya kuisababishia hasara serikali shilingi bilioni 8.5 kutokana na ukwepaji wa kodi wa kampuni ya Mafuta ya Lake Oil kwa kufanya udanganyifu kuuza mafuta ndani ya nchi Petrol lita 17,461,111.58 kwa kudanganya zilisafirishwa umefikia hatua nzuri.

"Takukuru imekamilisha shauri la hili na mtuhumiwa wamepewa miezi miwili kurejesha mikononi fedha zote na kuwarudisha mahakamani endapo watashindwa kurejesha kiasi hicho,"alisema.

Alisema mbali na shauri hilo, wapo kwenye hatua nzuri ya kukamilisha uchunguzi wa kesi ya hati fungani ya malipo yaliyolipwa na kampuni ya Enterprise Growth Markert Advisor(EGMA), kiasi cha dola 6,000,000 kwa lengo la kuisaidai Tanzania kupata mkopo wa dola 600,000,000.

"Takukuru imebaini fedha hizo dola 6,000,000 zilitakatishwa na watumishi wa umma wasio waaminifu wakishirikiana na baadhi kutoka sekta binafsi huku wakijua fedha hizo wamezipata kwa njia haramu,"alisema.

Akizungumzia hatua aliyochukua rais, Dk. John Magufuli kwa kutengua uteuzi wa aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa RAHCO, Mhandisi Benhadard Tito kwa tuhuma zinazomkabili tayaari wanachunguza shirika hilo la reli.

Alisema kulikuwepo na ukiukwaji wa kuwapata wazabuni kwenye ujenzi wa reli ya kisasa ya kimataifa(Standard Gauge) unaosimamiwa na Shirika la Hodhi la Reli Nchini(RAHCO), wanamekamatwa ikiwemo raia wa Kenya aliyekuwa kwenye mchakato huo, Kanji Muhando.

Kaimu huyo alisema shauri la kesi ya mabehewa ya kokoto 25 ya shirika la reili nchini (TRL), ya kukiuka sheria ya manunuzi ya umma Na.21/2004 pamoja na kanuni zake kutoka kampuni ya Hindustha Engineering and Industries Limited limekamilika.

"Uchunguzi umekamilika na tumeshapeleka kwa mkurugenzi wa Mashtaka kuomba kibali cha kuwafikisha watuhumiwa waliobainika kujihusisha na matendo ya rushwa na ukiukwaji wa sheria, taratibu na kanuni za ununuzi wa umma mahakamani,"alisema. 

Alisema rais alijipa kazi ya kutumbua majipu hivyo aliwasihi watumishi wa taasisi hiyo kutumikia wananchi kwa eledi huku akibainisha tayari wanatekeleza azma na dhamira ya rais ya kupambana na rushwa.

Akitolea ufafanuzi swala la kumsubiri rais kutumbua majipu ndio taasisi hiyo ifanye ufafanuzi, Mlowola alisema taasisi hiyo imejipanga vilivyo tangu Novemba 20 mwaka jana wakati rais alipohutubia bungeni alipoonesha dhamira ya na nia ya dhati ya kupambana na rushwa na ufisadi bila kumuonea mtu haya.

"Nitoe rai kwa wananchi kutoa taarifa ili tuweze kujua kabla hatujapigwa, tukiweza kuisaidia serikali kuokoa fedha kabla hatujapigwa zitasaidia wananchi  kutoa elimu bure, upatikanaji wa dawa na mishahara mizuri,"alisema.

Alisema tayari wameshaanza kuchunguza madai ya aliyekuwa mkurugenzi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), kwani tayari wapo hata viongozi wakubwa.

"Siwezi kusema kuwa kulikuwa na ulegevu, na hatua zimechukuliwa nchini imefikisha mhakamani mawaziri ila nchi ipo kwenye ufagio mpya hivyo tumeweka nguvu zaidi na hali zaidi,"alisema. 

Akizungumzia maofisa takukuru waliofukuzwa kazi a rais baada ya kukiuka maagizo ya rais ya kupata kibali cha kusafiri nje, alisema maofisa hao walikwenda kwenye mkutano wa taaisis za kupambana na rushwa uliofanyika Congo-Kinshasa.
(Imeandaliwa na mtandao wa www.habari za jamii.com-simu namba 0712-727062)



No comments:

Post a Comment

Post Top Ad