Mgeni rasmi wa mpambano wa fainali kugombea pikipiki Gongo la Mboto, Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Slaa (mwenye miwani) akikabidhi zawadi ya mshindi wa kwanza wa kombe la pikipiki lililoandaliwa na Lucas Lutanilwa.
Na Mwandishi Wetu
MEYA wa Manispaa ya Ilala, Jerry Slaa jana alilazimika kutoa zawadi ya pikipiki baada kuvutiwa na ushindani mkubwa uliokuwepo katika mchezo wa fainali wa mpira wa miguu kugombea pikipiki aina ya Boxer.
Meya Slaa alilazimika kutoa pikipiki hiyo baada ya timu za Mazombi FC na Sobibo FC zote za Gongo la Mboto kuonesha ushindani mkali katika mchezo wa fainali uliofanyika katika Uwanja wa Kampala Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam.
Slaa ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mchezo huo ameahidi kuwakabidhi pikipiki mpya timu ya Sobibo FC ambayo ilishika nafasi ya pili katika mchezo huo wa fainali ambapo timu ya Mazombi FC iliibuka mshindi na kukabidhiwa pikipiki mpya aina ya Boxer iliyotolewa na muandaaji wa mashindano hayo Lucas Lutanilwa.
"...Kutokana na ushindani mkubwa uliooneshwa na timu zote mbili natamka kwamba hata washindi wa pili Sobibo FC nao ninawazawadia pikipiki kama waliopata wenzao ili kuleta kiu ya kupenda michezo zaidi kwa vijana wetu," alisema Slaa akizungumza alipokuwa akikabidhi pikipiki kwa mabingwa Masombi FC.
Katika mchezo huo uliokuwa na ushindani kwa pande zote mbili timu ya Mazombi imefanikiwa kutwaa ubingwa na kukabidhiwa pikipiki mpya baada ya kuifunga Sobibo FC goli 1-0 lilipatikana dakika 70 ya kipindi cha pili cha mchezo huo.
Timu zote mbili pia zilikabidhiwa seti mojamoja ya jezi kwa kuweza kufika fainali, hata hivyo washindi wa nne na tatu wa Mashindano hayo yaliyopewa jina la Luta Cup walipewa zawadi za fedha taslimu kama pongezi. Timu ya Vijana Jogging Club walifanikiwa kutwaa ushindi wa tatu na kujinyakulia fedha taslimu katika mashindano hayo.
No comments:
Post a Comment