Matukio : Rais wa Namibia Bw. Lucas Pohamba Ashinda tuzo ya Kiongozi Bora Afrika 2014 na Kujinyakulia Mamilioni ya Fedha - Wazalendo 25 Blog

Glory to Story.

Habari Mpya

PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0784 643 633


PRINTING / GRAPHICS / DESIGN : 0676 643 633

Thursday 12 March 2015

Matukio : Rais wa Namibia Bw. Lucas Pohamba Ashinda tuzo ya Kiongozi Bora Afrika 2014 na Kujinyakulia Mamilioni ya Fedha


Hifikepunye Lucas Pohamba
Rais wa Namibia anayeondoka Hifikepunye Lucas Pohamba kwenye picha iliyopigwa Agosti 17, 2010 mjini Windhoek. Picha/AFP 
Na JOHN NJAGI

Kwa Mukhtasari
Rais wa Namibia anayeondoka Bw Hefikepunye Pohamba, ameibuka mshindi wa tuzo ya 2014 ya kiongozi bora barani Afrika na kumwangusha aliyekuwa rais wa Kenya Mwai Kibaki aliyestaafu 2013. Atapokea Sh460 milioni.


RAIS wa Namibia anayeondoka Bw Hefikepunye Pohamba, ameibuka mshindi wa tuzo ya 2014 ya kiongozi bora barani Afrika iliyotolewa na wakfu wa Mo Ibrahim na kumwangusha aliyekuwa rais wa Kenya Mwai Kibaki aliyestaafu 2013.
Bila kutoa sababu zozote, mwenyekiti wa kamati ya kusimamia tuzo hiyo ambaye alikuwa katibu wa uliokuwa Umoja wa Afrika (OAU)  kwa sasa Muungano wa Afrika (AU) Dkt Salim Ahmed Salim alitangaza kwamba Bw  Pohamba  alimshinda Bw Kibaki na viongozi wengine waliostaafu miaka mitatu iliyopita.
“Ninawahakikishia kuwa Rais Kibaki alikuwa miongoni mwa walioteuliwa kwa tuzo hiyo lakini alishindwa,” akasema.
Kwa kutoa mamlaka kwa amani, kuanzisha mabadiliko muhimu chini ya uongozi wake kama vile elimu ya bure katika shule za msingi na upili na miradi mikubwa ya miundo misingi pamoja na kupanua demokrasia nchini, ilitarajiwa kuwa Rais Kibaki, angetwaa tuzo hiyo.
Hata hivyo, aliangushwa na Bw Pohamba ambaye licha ya kutawala moja ya nchi changa kidemokrasia barani Afrika kwa mwongo mmoja, hakujulikana mno.
Bw Pohamba alivutia kamati kwa kuleta mageuzi katika nchi yake kwa muda mfupi, kukumbatia demokrasia na utawala bora.
Kufuatia ushindi huo, Rais huyo atatia kibindoni zawadi ya dola 5 milioni (Ksh460 milioni) atakazolipwa kwa kipindi cha miaka 10 na baadaye dola 200,000 (Ksh18 milioni) kila mwaka katika maisha yake yote.
Mwanzilishi wa tuzo hiyo, Bw Mo Ibrahim, alisema Rais Pohamba aliyeondoka mamlakani Desemba mwaka jana lakini hajatoa mamlaka bado kwa sababu mrithi wake hajaapishwa, ni kiongozi wa kuigwa barani Afrika.
Unyenyekevu
“Afrika sio tu kuhusu viongozi wabaya kama  Mobutu Seseseko na wengine. Kuna viongozi wanyenyekevu wanaoendelea kujitolea mhanga kwa ajili ya watu wa nchi zao,” akasema Bw Ibrahim.
Bw Salim Ahmed Salim alisema Namibia  imepiga hatua kwa kutoa elimu ya bure, kupunguza viwango vya ukimwi, kuimarisha usawa wa jinsia na kadhalika  kwa kuwa na asilimia 48 ya wabunge wanawake ingawa kuna changamoto za kiuchumi  na usawa wa kijamii.
Waliowahi kushinda tuzo hiyo awali ni aliyekuwa rais wa Musumbiji
Joaquim Chissano, (2007) Festus Mogae wa Botswana (2008) na Pedro Pires, Cape Verde (2011).
Aliyekuwa rais wa Afrika Kusini Nelson Mandela alitangazwa mshindi wa heshima tuzo ilipozinduliwa  2007.  Hakukuwa na washindi 2009, 2010, 2012 na 2013 baada ya kamati kusema hakuna aliyestahiki kuipata.

No comments:

Post a Comment