Matukio : Wataalam waagizwa kuandaa Ripoti ya Kumaliza Mgogoro wa Bwawa la Uluwa Sikonge - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


28 May 2017

Matukio : Wataalam waagizwa kuandaa Ripoti ya Kumaliza Mgogoro wa Bwawa la Uluwa Sikonge



Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe

Na Tiganya Vincent, Sikonge

Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe ameteua timu ya Maafisa watano wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge kwa ajili ya kuandaa taarifa(ripoti) itakayowasilishwa kwake Jumatano(wiki inayoanza kesho) ili imwezeshe kutoa maamuzi yatakaondoa kuondoa mgogoro uliosababisha ujenzi Mradi wa Bwawa la Umwagiliaji la Uluwa ushindwe kuendelea kwa sababu ya maji yake kuelekezwa katika Msitu wa Hifadhi wa Ipembampazi.

Hatua hiyo itasaidia kuokoa zaidi ya shilingi milioni 313 ambazo hadi hivi sasa zimeshatumika katika ujenzi wa mradi huo ambao ni kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji wa mpunga katika vijiji viwili vya Mtakuja na Kiloleni kama mradi utaendelea. Profesa Maghembe alichukua uamuzi huyo jana wilayani Sikonge baada ya kutembelea Mradi huo huku akiongozana na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri ili kujionea hatua ulipokuwa umefikia na hiyo mifereji ilijengwa kuelekea katika Msitu wa Hifadhi.

Alistaja wataalam hao kuwa ni Ofisa wa Maliasili, Misitu, Kilimo na Mhandisi wa Maji, Mhandishi wa Ujenzi kutoka Ofisi ya Mkurugenzi Mteandaji wa Halmashauri ya Sikonge ambao aliwapa jukumu la kuandaa taarifa itakayoonyesha mambo mbalimbali ikiwemo kupima na kuonyesha kiasi cha eneo ambalo wananchi wanalohitaji kwa ajili ya kilimo hicho na eneo lilobaki katika Msitu huo wa Hifadhi.

Profesa Maghembe aliwaambia kuwa uharaka na ubora wa ripoti ya Halmashauri ndio utakaoisaidi Wizara ya Maliasili na Utalii kufikia maamuzi haraka ambayo baada ya wataalam wake kuipitia atawalisha mapendekezo na hatua waliofikia kwa Mkuu wa Mkoa kwa ajili ya hatua zaidi.

Aliongeza kuwa wakati hatua za kupata eneo hilo zikiendelea ni vema uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge ukaanza kujipanga kwa kuandika andiko la mradi wa kuomba fedha kutoka Wizara ya Maji ili kazi ya ujenzi huo ikamilike na ianze kuwanufaisha wananchi.

Aidha , Waziri huyo wa Maliasili na Utalii alitoa wito kwa wananchi wote watakaopata maeneo karibu na Hifadhi mbalimbali kuwa walinzi wa kwanza wa rasilimali hizo na kuwakemea wale wote watakaonekana kutaka kuzihujumu kwa faida binafsi. Kwa upande wa Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri alisema kuwa sehemu kubwa ya ardhi ya Halmashauri ya Sikonge ni mistu ya hifadhi ambayo inafikia asilimia 95 na asilimia tano tu ndio inatumika kwa matumizi mengine ya binadamu ikiwemo kilimo.

Kufuatia hali hiyo aliwaasa viongozi wa Halmashauri hiyo kuwa makini wakati wanaendesha zoezi hilo la kuomba eneo hilo lenye ukubwa wa hekta 500 kwa kuangalia mahitaji yao halisi ili isije ikatokea wameshapewa wanaanza tena kuomba nyongeza.

Aidha , Mkuu huyo wa Mkoa alimweleza Waziri Maghembe, Ofisi yake itatuma Wataalam wiwili waungane na wa Halmashauri kwa ajili ya kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa haraka na umakini ili wananchi waanze kufanikisha mradi huo.

Akisoma taarifa ya mradi huo Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Sikonge Abel Busalama alisema kuwa mradi huo uliogharimu hadi sasa milioni 313 .8 ambao ungevinufaisha vijiji vya Mtakuja na Kiloleni ulishindwa kuendelea baada mjenzi kujenga mifereji ya umwagiliaji akielekeza katika Msitu wa Hifadhi wa Ipembampazi jambo lililopelekea wananchi wa vijiji hivyo kuvamia msitu na kuanzisha mashamba ya mpunga na wengine kuingiza mifugo kwa ajili ya malisho.

Hivyo alimwomba Waziri huyo mwenye dhamana ya Maliasili na Utalii kutoa ruhusa ya eneo la hekta 500 katika Msitu wa Hifadhi ya Ipembampazi liweze kupima na kutumika kwa shughuli za kilimo cha umwagiliaji .


Ujenzi wa mradi huo ulifika hatua ya pili ambapo ilibaki hatua ya tatu ili uanze kutumika na ndipo ulisimamishwa.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad