Matukio: Makamu wa Rais , Mhe. Samia Suluhu Hassan Ahudhuria Mkutano wa SADC, Swaziland - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


17 Mar 2017

Matukio: Makamu wa Rais , Mhe. Samia Suluhu Hassan Ahudhuria Mkutano wa SADC, Swaziland




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akikagua gwaride la Heshima lililoandaliwa kwa ajili yake mara baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa kimataifa wa Mfalme Mswati wa III mjini Mbabane Swaziland leo march 16,2017 kwa ajili ya kuhudhuria mkutano wa wakuu wa nchi na serikali wa Jumuiya ya maendeleo kusini mwa Afrika (SADC) ambapo Makamu wa Rais amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amewasili mjini Mbabane - Swaziland leo 16-Mar-2017 kwa ajili ya kuhudhuria mkutano wa Wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

Mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Kimataifa wa Mfalme Mswati III mjini Mbabane – Swaziland, Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan amepokelewa na Viongozi mbalimbali ambao wameongozwa na Waziri wa Utumishi wa Umma wa Serikali ya Swaziland Owen Nxumalo.

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan baada ya kuwasili uwanjani hapo amekagua gwaride la heshima lililoandaliwa kwa ajili yake na kushuhudia vikundi mbalimbali vya burudani uwanjani hapo.

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan atamuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania Dakta JOHN POMBE MAGUFULI ambaye pia ni Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama inayojulikana kama SADC DOUBLE TROIKA kwenye mkutano huo.

Hapo kesho tarehe 17-Marchi-2017, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan atahudhuria mkutano wa Wakuu na Serikali wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama unaojulikana kama SADC Double Troika ambao utajadili kwa kina hali ya ulinzi na usalama katika nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC)na Falme ya Lesotho.

Mkutano huo wa SADC Double Troika utafanyika kwa kuzingatia mapendekezo ya mkutano wa Mawaziri wa Kamati Ndogo ya Siasa na Diplomasia uliofanyika Dar es Salaam tarehe 24 februari 2017 ambapo mawaziri hao walionyesha ipo haja ya kuitisha mkutano huo ili kujadili kwa kina hali ya ulinzi na usalama kwenye hizo.

Mkutano wa SADC Double Troika utahusisha nchi Sita wanachama wa asasi hiyo ambazo ni Tanzania,Swaziland, Afrika Kusini, Angola, Botswana na Msumbiji.



Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan katika msafara wake amefuatana na Waziri wa Mambo ya nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,Kikanda na Kimataifa Dakta Augustine Mahiga, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Charles Mwijage na Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Balozi Amina Salum Ali.

Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais wa

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mbabane – SWAZILAND.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad