Afya : Mafunzo ya Msaada Huduma za Saikolojia kwa Wahudumu Vituo vya Huduma, Tiba Yafungwa, Mwanza. - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


17 Feb 2018

Afya : Mafunzo ya Msaada Huduma za Saikolojia kwa Wahudumu Vituo vya Huduma, Tiba Yafungwa, Mwanza.




Mratibu wa Kudhibiti Ukimwi mkoa wa Mwanza Dk. Pius Masele amefunga mafunzo ya siku tano kuhusu msaada na huduma za kisaikolojia kwa wahudumu wa jamii wanaosaidia kazi katika vituo vya huduma na tiba kwa watu wanaoishi na Maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) vilivyopo katika halmashauri 7 za wilaya mkoa wa Mwanza.


Mafunzo hayo yalikuwa yanafanyika katika ukumbi wa mikutano wa Midland Hotel jijini Mwanza kuanzia Jumatatu Februari 12,2018 hadi Ijumaa 16 Februari ,2018 yakiendeshwa na Shirika la Ariel Glaser Pediatric AIDS Healthcare Initiative (AGPAHI) kwa ufadhili wa watu wa Marekani kupitia Centres for Disease Control (CDC).


Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo Dk. Masele aliwataka wahudumu hao wa jamii kutumia vyema ujuzi na elimu waliyopewa ili wakaboreshe huduma za afya kwenye vituo vyao. "Nawashukuru AGPAHI kwa kutoa mafunzo haya,naamini mafunzo mliyopata yawatasaidia pia katika kuwaelimisha na kuwafuatilia wateja waliopotea katika huduma",aliongeza Dk. Masele.


Nao washiriki wa mafunzo hayo, Hawa Radhamani kutoka hospitali ya wilaya ya Misungwi Kija Robert kutoka kituo cha afya Nyamilama halmashauri ya wilaya ya Kwimba walisema wamepata uelewa mkubwa kuhusu masuala ya VVU na Ukimwi yatawasaidia kuboresha zaidi huduma za afya kwenye vituo vyao na jamii kwa ujumla.


Jumla ya wahudumu wa jamii 45 kutoka halmashauri za wilaya za Ilemela,Kwimba, Magu,Buchosa,Misungwi,Sengerema na Nyamagana wameshiriki mafunzo hayo na kupatiwa vyeti vya ushiriki. Miongoni mwa mada zilizofundishwa katika mafunzo hayo ni msaada wa kisaikolojia,Ukweli kuhusu VVU na Ukimwi na huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.


Mada zingine ni kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto,jinsi ya kuwa wazi,kuishi kwa matumaini,uelimishaji rika,ushauri nasaha,kuanzisha na kuongoza vikundi,tabia hatarishi kwa vijana balehe, mawasiliano na mabadiliko yake na stadi za maisha.


Mambo mengine yaliyofundisha ni mtandao wa huduma zilizopo katika jamii,unyanyapaa na ubaguzi,kubadilishana uzoefu,uzazi wa mpango,matumizi ya vileo na madhara yake,magonjwa ya zinaa,kifua kikuu na Ukimwi,makundi maalumu,mto wa maisha,afya ya akili na changamoto zake katika ufuasi sahihi wa dawa pamoja na ukatili wa kijinsia na mawasiliano kwa watoto na vijana.

Mratibu wa Kudhibiti Ukimwi mkoa wa Mwanza Dk. Pius Masele akifunga mafunzo ya siku tano kuhusu msaada na huduma za kisaikolojia kwa wahudumu wa jamii kutoka halmashauri za wilaya mkoa wa Mwanza.

Dk. Masele akikabidhi cheti cha ushiriki kwa Sospeter Lameck kutoka halmashauri ya wilaya ya Buchosa.Wa kwanza kulia ni Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa Jamii AGPAHI mkoa wa Mwanza, Cecilia Yona. Wengine wawezeshaji wakati wa mafunzo hayo Dk. Joseph Musagasa (wa kwanza kushoto) akifuatiwa na Gaston Kakungu ambaye ni Afisa Muuguzi Mstaafu.

Chausiku Sitta kutoka halmashauri ya wilaya ya Kwimba akipokea cheti.

Godbertha Godrey kutoka hospitali ya Mwananchi halmashauri ya manispaa ya Nyamagana akipokea cheti.

Waziri Musa kutoka halmashauri ya manispaa ya Ilemela akipokea cheti.

Picha ya pamoja Dk. Masele na washiriki wa mafunzo hayo.

Picha ya pamoja

Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa Jamii AGPAHI mkoa wa Mwanza, Cecilia Yona akifundisha namna ya kujaza taarifa katika daftari la mtoa huduma za VVU na Ukimwi katika jamii.
Washiriki wa mafunzo hayo wakijaza fomu ya namna ya kufuatilia wateja waliopotea katika huduma.

Washiriki wa mafunzo hayo wakichora 'mto wa maisha' kuelezea changamoto na mafanikio waliyopata katika maisha yao.

Washiriki wakiendelea na zoezi la kuchora mto wa maisha.

Sospeter Lameck akielezea kuhusu mto wake wa maisha.

Washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia historia ya wahudumu wa afya ngazi ya jamii kupitia mti wa maisha uliochorwa na kila mmoja.

Washiriki wa mafunzo hayo wakifanya zoezi la kuanisha sifa kwa kila mshiriki wa mafunzo wakati wa mada ya utambuzi wa tabia. Picha zote na Kadama Malunde- Malunde1 blog

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad