Matukio : Kiwanda cha SUNFLAG cha Arusha Chapigwa Faini Kufadhili Uvuvi Haramu - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


22 Jan 2018

Matukio : Kiwanda cha SUNFLAG cha Arusha Chapigwa Faini Kufadhili Uvuvi Haramu




Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Sunflag cha mjini Arusha, Ajay Shah, akiongoza zoezi la kuchoma nyavu haramu za dagaa zilizo chini ya sentimita 8 (marobota 584) zenye jumla ya shilingi milioni mia moja zilizokamatwa kwenye Kiwanda chake na Kikosi Kazi Maalum cha Kutokomeza Uvuvi Haramu nchini kilichoundwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Joelson Mpina kwenye dampo la takataka nje kidogo ya jiji la Arusha leo.(Na John Mapepele)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Joelson Mpina (mwenye kofia) akikagua chumba cha baridi cha kuhifadhia samaki (Cold room) cha kampuni ya Alpha Choice mjini Arusha leo akiwa katika operesheni maalumu ya kudhibiti uvuvi haramu kulia ni mmliki wa kampuni hiyo Yussuf Khatry.
Marobota 584 ya nyavu haramu yaliyotengenezwa na Kiwanda cha Sunflag cha mjini Arusha yenye thamani ya shilingi milioni 100 wakitekea kwenye dampo nje ya jiji la Arusha leo. Marobota hayo alikamatwa na Kikosi Kazi Maalum cha Kutokomeza Uvuvi Haramu nchini kilichoundwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Joelson Mpina ambapo uteketezaji huo uliongozwa na mmliki wa kiwanda hicho Ajey Shah.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Joelson Mpina (mwenye kofia) akisikiliza taarifa ya ukamataji wa marobota 584 ya nyavu haramu yaliyotengenezwa na Kiwanda cha Sunflag cha mjini Arusha yenye thamani ya shilingi milioni 100 kutoka kwa kiongozi wa Kikosi Kazi Maalum cha Kutokomeza Uvuvi Haramu nchini West Mbembati aliye kulia, kushoto mwakilishi wa Afisa Tawala wa Mkoa wa Arusha David Lyamongi.






Na John Mapepele


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Luhaga Mpina amekitoza faini ya Shilingi milioni mia moja Kiwanda cha Sunflag Tanzania Limited cha jijini Arusha baada ya kukutwa na makosa mawili ambayo ni kuzalisha na kuuza nyavu bila kuwa na leseni kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na kuzalisha na kuuza nyavu ambazo ziko kinyume na matakwa ya Sheria ya Uvuvi namba 22 ya mwaka 2009.


Kulingana na maelezo ya Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda hicho Ajay Shah, kiwanda kimekuwa kikitengeneza vyavu hizo haramu kwa miaka mitatu mfululizo sasa ambapo inakadiliwa kuwa tayari kimeshatengeneza tani 1296 nyavu hizo zenye thamani ya shilingi bilioni nne.


Akitoa taarifa kwa Waziri Mpina, Kiongozi wa kikosi kazi cha kutokomeza uvuvi haramu katika kanda ya Ziwa Victoria, West Mbembati amesema kuwa tarehe 17/1/2018 walifika kwenye kiwanda hicho na kukamata marobota 584 yenye thamani ya milioni mia kufuatia maelekezo ya Waziri Mpina yaliyotolewa Mjini mwanza hivi karibuni baada ya mfanyabiashara Dastan Venanti kukamatwa na nyavu hizo zenye thamani ya milioni sitini na tano ambazo nyaraka zilionyesha alinunua katika kiwanda hicho.


Akipokea taarifa hiyo Waziri Mpina alisema mkakati uliopo kwa sasa ni kuwabaini watengenezaji na wasambazaji wote wa zana haribifu za uvuvi ikiwa ni pamoja na vyavu zisizoruhusiwa kisheria ambapo amesema hatua za kali za kisheria dhidi yao zitatumika ili kudhibiti uvuvi haramu kwenye maji(mito,maziwa na bahari) ya nchi yetu.


“Operesheni ya kuwabaini na kuwachukulia hatua wafanya biashara wakuu wanaofadhili na kuendeleza biashara ya uvuvi haramu ni ya kudumu ambapo mkakati uliopo sasa ni kuwanyang’anya na kuwafutia lesseni zao za biashara” alisisitiza Mpina


Aliwaonya wafanyabiashara wanaosafirisha samaki na mazao yake katika nchi za jirani za Uganda, Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kongo wanaotishia kugoma ambapo amesisitiza kwamba hatua waliyoichukuwa ni ndogo badala yake waachane kabisa na biashara hiyo kwa kuwa wamekuwa wakikwepa kodi na kuikosesha Serikali mapato yake kwa muda mrefu.


Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho, Ajay Shah alikiri kutenda makosa hayo na kueleza kuwa kiwanda kimekuwa kikiendelea kutengeneza vyavu hizo bila kujua kuwa kilikuwa hakizingatii sheria za Uvuvi ambapo alisema kimekuwa kinauza nje ya nchi hususan kwenye soko la Nairobi nchini Kenya na Mwanza


Aliwataja baadhi ya wateja wake wakuu wa mkoani Mwanza kuwa ni pamoja na Dastan Venant, Morice Otieno na Majani Masagati ambao wote walikamatwa hivi karibuni na nyavu zisizoruhusiwa kisheria na kikosi kazi cha kudhibiti uvuvi haramu kilichoundwa na Waziri Mpina na kutozwa faini ya jumla ya shilingi milioni 120 huku vyavu hizo zikitaifishwa na kuteketezwa mara moja.


Katika hatua nyingine Mkurugenzi huyo aliongoza zoezi la kuteketeza nyavu hizo haramu kwa kushirikiana na Waziri na Watendaji mbalimbali wa Serikali katika dampo la kuwekea takataka nje kidogo ya jiji la Arusha huku akikiri kuwa atazingatia taratibu zote za Serikali katika kutengeneza nyavu zinazoruhusiwa kisheria ambapo alisema tayari wameshapeleka barua Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili kupata kibali cha kutengeneza nyavu.


Aidha Waziri Mpina ametoa siku tatu kwa Watendaji wa Wizara yake kumempatia kibali cha kutengeneza nyavu hizo kwa mujibu wa sheria za nchi. Kulingana na Sheria ya Uvuvi namba 22 ya Mwaka 2003 kibali hicho kinatolewa na Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Uvuvi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad