Matukio : Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa Ahutubia Baraza la Eid Kitaifa Mkoani Kilimanjaro - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


27 Jun 2017

Matukio : Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa Ahutubia Baraza la Eid Kitaifa Mkoani Kilimanjaro



*Ahimiza nyumba za ibada zisaidie vita ya dawa za kulevya


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepiga marufuku usafirishaji wa chakula kwenda nje ya nchi kuanzia leo. “Kuanzia leo, ni marufuku kwa mtu yoyote kusafirisha mazao ya chakula kwenda nje ya nchi bila ya vibali. Serikali inahamasisha uwekezaji kwenye ujenzi wa viwanda nchini. Kama tutatoa vibali, ni lazima mtu alazimike kusaga nafaka ili kutoa ajira nchini,” amesema.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumatatu, Juni 26, 2017) wakati akitoa nasaha kwenye Baraza la Eid lililofanyika kitaifa kwenye msikiti wa Masjid Riadha, mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro mara baada ya kuswali sala ya Eid.
“Jana nimeona kwenye televisheni taarifa kuhusu malori 10 yaliyokamatwa Tarakea yakiwa na mahindi tayari kuvushwa mpaka. Mheshimiwa RC akasema chakula hicho ni lazima yarudishwe kwa ajili ya usagaji.”


“Mimi nasema kuanzia leo, yeyote atakayekamatwa akitorosha chakula kwenda nje ya nchi, chakula hicho kitataifishwa na kupelekwa ghala la Taifa na gari lake tutalitaifisha na litaishia Jeshi la Polisi. Tunafanya hayo kwa lengo la kuwalinda Watanzania tusikumbwe na baa la njaa.”


Akitoa tahadhari kuhusu uuzwaji wa chakula nje ya nchi, Waziri Mkuu amesema kumekuwa na wimbi kubwa la usafirishaji wa chakula kwenda nje ya nchi bila kibali. “Hilo ni kosa kubwa kwa sababu litasababisha nchi yetu kupata baa la njaa huko mbele,” amesema.


Amesema mipaka ya Tarakea, Holili, Mwanga, Horohoro, Siha, Namanga na Sirari imekuwa inapitisha kiasi kikubwa cha mazao ya chakula kwenda nje ya nchi jambo ambalo ni hatari sana. “Hii ni kwa sababu chakula cha ndani hakitoshelezi mahitaji. Kwa sababu nchi zote za jirani hazina chakula cha kutosha. Tusipokuwa makini, tutabaki tunalia njaa.”


Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasihi wafanyabiashara wa ndani, wachukue mahindi kutoka maeneo yenye mavuno mengi na kuyapeleka kwenye sehemu zenye mavuno kidogo. “Watanzania tushirikiane, kama ni biashara tutoe huku kwenye mavuno mengi na tuyapeleke Shinyanga na Geita ambako wanayahitaji au tukanunue Sumbawanga na kuyapeleka kwenye mikoa mingine yenye upungufu,” alisisitiza.


Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka viongozi wa dini waisadie Serikali katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya kwa kupitia kwenye nyumba za ibada. “Naomba tuendelee kushirikiana kupambana na janga hili la dawa za kulevya kwa ustawi wa nchi yetu. Naamini viongozi wa dini mnayo nafasi kubwa katika mapambano haya, kwa kuwafunda vijana wetu kuishi katika maadili ya kidini na kutojiingiza kwenye janga hilo.”


Alisema Serikali kwa upande wake itaendeleza mapambano hayo bila ajizi wala mzaha. “Tunaomba wananchi wote watuunge mkono kwa kutoa taarifa sahihi za wanaojihusisha na uzalishaji, utengenezaji, usambazaji na utumiaji wa dawa za kulevya pindi tu wanapowabaini.”


Wakati huo huo, akitoa tafsiri ya Qur’aan tukufu kwenye Baraza la Eid, Sheikh wa Mkoa wa Arusha, Sheikh Shaaban Juma alisema kila nguzo katika Uislamu inapaswa kufuatwa na kwamba mtu akiharibu nguzo moja tu anakuwa ameharibu nguzo zote tano.


Alisema siku ya kiyama, watatokea watu wenye thawabu kama milima ya Usambara ama Upareni na akawataka Waislamu wote nchini wadumu katika kutenda mema ili wapate thawabu.


Mapema, akitoa khutba katika swala ya Eid el Fitr iliyoswaliwa kwenye msikiti huohuo wa Masjid Riadha, Sheikh Mlewa Shaban alisema sikukuu ya Eid ni siku ya kujiepusha na madhambi kama ulevi, kamari na lugha chafu, bali aliwataka waumini wote waitumie siku hiyo kuwapa furaha maskini, yatima na wajane.


“Mtu asiseme mwezi wa Ramadhan umepita, sasa narudia mambo yangu ya zamani. Adhabu za Mwenyezi Mungu hazina mipaka na wale waliotulizana watapata thawabu yao, kumbukeni neema na Mwenyezi Mungu na mcheni Mwenyezi Mungu.”


“Kitu tunachopaswa kufanya kila wakati ni kumcha Mwenyezi Mungu. Lazima tupendane, tuondoe tofauti zetu na tuujenge Uislam. Hatuwezi kuujenga uislam kama hatupendani. Lazima tuilinde ibada yetu kwa sababu hatuna garantii, ni lini tutaondoka,” alisema.


Sherehe hizo zilihudhuriwa na Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir bin Ally; Wajumbe wa Baraza la Ulamaa, Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe; Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mama Anna Mghwira; IGP Mstaafu, Bw. Said Mwema; Mbunge wa Moshi Mjini, Bw. Jaffary Michael; Wakuu wa Wilaya za Mkoa huo na viongozi mbalimbali wa dini na Serikali.


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akitoa nasaha kwa waumini (hawapo pichani) waliohudhuria Swala ya Eid el Fitr na Baraza la Eid Kitaifa kwenye msikiti wa Masjid Riadha mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro tarehe 26 Juni, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waumini wa dini ya Kiislamu waliohudhuria Swala ya Eid el Fitr na Baraza la Eid Kitaifa kwenye msikiti wa Masjid Riadha mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro wakimsikiliza Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati akitoa nasaha za Eid, tarehe 26 Juni, 2017.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiteta jambo na Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir bin Ally wakati wa stafutahi kwenye Ikulu ndogo ya Moshi, mara baada ya Swala ya Eid el Fitr na Baraza la Eid Kitaifa mkoani Kilimanjaro tarehe 26 Juni, 2017.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiagana na Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir bin Ally mara baada ya stafutahi kwenye Ikulu ndogo ya Moshi, mkoani Kilimanjaro tarehe 26 Juni, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisaini kitabu cha maombolezo, nyumbani kwa marehemu Dk. Philemon Ndesamburo, eneo la Kiboriloni, Moshi, mkoani Kilimanjaro tarehe 26 Juni, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akitoa pole na neno la faraja kwa wanafamilia, nyumbani kwa marehemu Dk. Philemon Ndesamburo, eneo la Kiboriloni, Moshi, mkoani Kilimanjaro tarehe 26 Juni, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akimpa pole mjane wa marehemu, mama Ndehorio P. Ndesamburo alipofika nyumbani kwao eneo la Kiboriloni, Moshi, mkoani Kilimanjaro kuwafariji kutokana na msiba wa Dk. Philemon Ndesamburo, leo tarehe 26 Juni, 2017.

Kaka wa marerehemu Dk. Philemon Ndesamburo, Bw. Zablon Sindato Kihwelu akimshukuru Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliyefika nyumbani kwao eneo la Kiboriloni, Moshi, mkoani Kilimanjaro kuwafariji kutokana na msiba wa Dk. Philemon Ndesamburo, leo tarehe 26 Juni, 2017.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Bibi Anna Mgwira (wa tatu kushoto), mjane wa marehemu na Kaka wa marehemu wakiomba dua na wanafamilia kwenye kaburi la Dk. Philemon Ndesamburo, aliyezikwa nyumbani kwake eneo la Kiboriloni, Moshi, mkoani Kilimanjaro. Wa kwanza kulia ni mtoto wa marehemu.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad