TZUK : Taarifa kwa Watanzania wote waishio UK ( Tujumuike UK ). - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


3 May 2016

TZUK : Taarifa kwa Watanzania wote waishio UK ( Tujumuike UK ).



Kikosi kazi cha watanzania wanaoishi Falme za UINGEREZA na EIRE YA KASKAZINI (TZUK Diaspora Taskforce, kwa kifupi, TZUK-DTF) kiliasisiwa na Mheshimiwa Balozi Peter Kallaghe mwaka 2014, kutokana na kutokuwepo na chombo/Jumuiya madhubuti ya kuwaunganisha Watanzania waishio hapa Uingereza

TZUK-DTF ilianza na wajumbe 11 wakiwemo maofisa wa ubalozi 2 kikiwa na majukumu makubwa ya kuwa kiunganishi kati ya watanzania na ubalozi wao hapa Uingereza pamoja na kupanga na kuratibu ufufuaji wa Jumuiya ya watanzania ambayo itakuwa shirikishi zaidi na endelevu. Mnamo mwishoni mwa mwaka 2015, chini ya Naibu Balozi, Mheshimiwa Msafiri Marwa, ilikubaliwa kwamba ili kutimiza malengo yake kwa ufanisi zaidi yaliyohusisha kuratibu ufufuaji wa Jumuiya ya watanzania Uingereza na kuhakikisha kwamba Jumuiya hiyo inakuwa na Katiba iliyo bora zaidi, ilionekana ni vyema TZUK-DTF ikawa na wajumbe zaidi watakaojumuisha watanzania wa kada mbalimbali walioko Uingereza wakiwemo waliokuwa viongozi wa mikoa wa Jumuiya na baadhi ya wale walioshiriki katika michakato ya uasisi wa katiba na uundwaji wa Jumuiya ya watanzania Uingereza. 

Kikosi Kazi hiki kipya kilikutana rasmi tarehe 05 Mwezi wa Kumi na Mbili, 2015, chini ya uongozi na ulezi wa Mheshimiwa Naibu Balozi, Msafiri Marwa, ambapo kiliainishiwa majukumu yake kama ifuatavyo:
1. Kujadili na kuziwekea mikakati ya ufumbuzi changamoto mbalimbali zilizokabiliwa na TZUK-DTF katika kutimiza majukumu yake ikiwemo na zile ambazo ziliikabili Jumuiya ya watanzania iliyokuwepo.
2. Kupitia maoni ya watanzania yaliyokuwa yamekusanywa tayari, ikiwemo na katiba za Jumuiya ili Jumuiya iwe na katiba bora zaidi itakayoongeza ufanisi katika shughuli zaJumuiya.
3. Kuhakiki na kuboresha muundo wa Jumuiya utakaokidhi mahitaji ya sasa ya watanzania waishio Uingereza.
4. Kuzikusanya na kuzipitia taarifa zote zitakazopatikana za fedha za Jumuiya enzi za uhai wake na kuzijumuisha kwenye Jumuiya mpya itakayoundwa
5. Kutengeneza na kuratibu njia bora zamawasiliano miongoni mwa wanajumuiya.
6. Kusimamia kipindi cha mpito kitakachopelekea kuundwa kwa Jumuiya ya watanzania Uingereza ikiwemo kuratibu uanzishaji/uimarishaji wa Jumuiya za watanzania za mikoani kwa mujibu wa katiba mpya, na 
7. Kuandaa na kusimamia mkutano mkuu wa watanzania wote wa Uingereza wenye madhumuni ya kutoa ripoti nzima ya TZUK-DTF, kupitisha katiba mpya, kutambulisha Kamati Kuu na uongozi mpya wa Jumuiya, kujadili na kuhakiki mipango na mikakati ya shughuli mbalimbali za Jumuiya kwa mwaka ujao, na Kikosi Kazi kuvunjwa rasmi na kukabidhi madaraka ya  usimamiaji na uendeshaji wa Jumuiya ya watanzania kwa uongozi mpya wa Jumuiya.

Kama watanzania wa  Uingereza mlivyoshiriki  katika upendekezaji wa katiba mpya na kutoa maoni juu ya Jumuiya yenu, tunaendelea kuwatia moyo kushiriki kwa moyo mmoja na wa kizalendo pindi tutakapoitisha mikutano ya watanzania kwenye mikoa mliyoko mwezekuhakikisha safari hii ya kuwa na Jumuiya iliyo/zilizo imara inafikia mwisho ulio mwema

Ahsanteni

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad